Thursday, January 30, 2020

BALOZI IBUGE AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA MKUU WA ITIFAKI WA ZIMBABWE

Mkuu wa Itifaki, Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Huduma za Itifaki na Kitengo cha Utafiti wa Zimbabwe Mhe. Balozi Chipo Zindoga leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Pamoja na mambo mengine, mazungumzo hayo yalilenga kubadilishana uzoefu wa masuala ya itifaki baina ya Tanzania na ZImbabwe.

Mhe. Zindoga amekuja nchini kujifunza jinsi  Tanzania inavyoratibu masuala ya iitifaki ikiwemo kufanikisha kwa mafanikio makubwa ya Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika mwezi Agosti, 2019 jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi Mkuu wa Huduma za Itifaki na Kitengo cha Utafiti, Ofisi ya Rais, Zimbabwe Mhe. Balozi Chipo Zindoga akimueleza jambo Mkuu wa Itifaki, Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge wakati walipokutana na kufanya mazungumzo jijini Dar es Salaam
Mkuu wa Itifaki, Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge akiongea na Mkurugenzi Mkuu wa Huduma za Itifaki na Kitengo cha Utafiti, Ofisi ya Rais, Zimbabwe Mhe. Balozi Chipo Zindoga wakati wa mazungumzo baina yao jijini Dar es Salaam
Mkuu wa Itifaki, Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge akiagana na Mkurugenzi Mkuu wa Huduma za Itifaki na Kitengo cha Utafiti, Ofisi ya Rais, Zimbabwe Mhe. Balozi Chipo Zindoga mara baada ya kukamaliza mazungumzo yao

BALOZI DKT. DAU, BALOZI WA INDONESIA WAKUBALIANA KUTANGAZA UTALII WA TANZANIA


Balozi wa Tanzania nchini Malaysia Mhe Dkt Ramadhani Kitwana Dau, ambaye pia anawakilisha Indonesia amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Indonesia nchini Malaysia Mhe Rusdi Kirana na kukubaliana kutangaza fursa za utalii wa Tanzania.

Mara baada ya mazungumzo hayo, Balozi Dau alipata fursa ya kumkabidhi Mhe Balozi Kirana filamu za kutangaza utalii wa Tanzania ambapo filamu hizo zitaoneshwa kwenye ndege bila malipo yoyote kutoka ya Serikali ya Tanzania.

Mhe. Balozi Kirana ni mfanyabiashara mkubwa anaemiliki Mashirika ya ndege ya Lions Group, Batik na Malindo. Kwa pamoja, mashirika hayo yana ndege zaidi ya 300 na limeajiri wafanyakazi 43,000.

Aidha mashirika hayo yanahudumia abiria milioni 60 kwa Mwaka (wastani wa abiria 160,000 kwa Siku) na ina Safari 3,400 za kwenda na kurudi kwa Siku. Mashirika hayo yanatoa Huduma za Safari kwenye nchi zaidi ya 50 duniani.

Ubalozi wa Tanzania umemshawishi na amekubali kutangaza utalii wa Tanzania kwenye ndege zake kupitia inflight entertainment bure ambapo pamoja na mambo mengine filamu hizo zitasaidia kutangaza fursa za utalii wa Tanzania.

Katika mazungumzo yao, Mabalozi hao wamekubaliana umuhimu wa kutangaza utalii katika ukanda wa Kusini Mashariki ya Asia ambapo Balozi Kirana ameahidi kuanzisha Safari za ndege kwenda Tanzania baada ya kufanya mazungumzo na Mawakala wa utalii wa Tanzania. Balozi huyo pia ameonesha utayari wake wa kukutana na kujadiliana na mawakala wa utalii wa Tanzania kuhusu kuanzisha Safari za ndege baina ya Indonesia na Tanzania. Mkutano huo Utafanyika mwezi Februari 2020 katika Kongamano la Uwekezaji baina ya Tanzania na Indoensia (Tanzania/Indoensia Investment Forum) litakalofanyika Jijini Jakarta Indoensia tarehe 24-26 Septemba 2020.

Aidha katika mazungumzo hayo, Mhe Dkt Dau alimwalika Mhe Balozi Kirana kutembelea Tanzania Mwaliko ambao ameukubali na ameahidi kuja Tanzania katikati ya mwezi Septemba 2020.

kwa upande wake, Mhe. Balozi Kirana amemkabidhi Mhe. Balozi Dkt Dau mfano wa ndege zake kwa ajili ya kupamba ofisi.


Balozi wa Tanzania nchini Malaysia Mhe Dkt. Ramadhani Kitwana Dau akimuonesha moja kati ya filamu ya utalii Balozi wa Indonesia nchini Malaysia Mhe. Balozi Rusdi Kirana


Balozi wa Tanzania nchini Malaysia Mhe. Dkt. Ramadhani Kitwana Dau akimkabidhi moja kati ya filamu za utalii Balozi wa Indonesia nchini Malaysia Mhe Balozi Rusdi Kirana 



Wednesday, January 29, 2020

WAZIRI PROF. KABUDI AKUTANA, KUFANYA MAZUNGUMZO NA MTENDAJI MKUU WA NORFUND



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) amekutana na kufanya mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Uwekezaji wa Norway kwa nchi zinazoendelea (Norwegian Investment Fund for Developing Countries - Norfund), Bw. Tellef Thorleifsson.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo katika ofisi ndogo za wizara Jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine, Mhe. Waziri Prof. Kabudi pamoja na Bw. Thorleifsson wamejadili masuala yanayohusu fursa za uwekezaji na biashara kati ya Tanzania na Norway.

"Kwa kweli sisi tunafurahishwa na mradi wa Africado ambao umewekezwa katika Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro kwani umekuwa ukizalisha maparachichi yanayopelekwa nchi mbalimbali za Ulaya kama vile Uholanzi, Uingereza, Ufaransa, Hispania, Ureno, na Mashariki ya Kati, na kuisaidia serikali kukuza pato lake la taifa," Amesema Prof. Kabudi na kuongeza kuwa mradi huo umetoa fursa za ajira takribani 600 kwa wananchi wa Tanzania.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Uwekezaji wa Norfund, Bw. Thorleifsson amesema kuwa lengo la mkfuko huo ni kuwekeza katika miradi mbalimbali ndani ya nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara ili kuzisaidia nchi hizo kukuza uchumi wake.

"Lengo letu ni kuwekeza katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara ambapo hadi kufika mwishoni mwa 2018 tayari mfuko ulikuwa umewekeza nchini Tanzania kiasi cha Dola za Marekani milioni 160 katika miradi mbalimbali katika sekta za nishati, fedha, chakula na kilimo. Uwekezaji huo umeifanya Tanzania kuwa nchi ya nne katika nchi zinazonufaika na miradi ya Norfund," amesema Bw. Thorleifsson

Norfund ni taasisi iliyo chini ya Serikali ya Norway yenye jukumu la kuwekeza mitaji na utaalamu katika uanzishwaji wa miradi mbalimbali endelevu kwenye nchi zinazoendelea kwa lengo la kuchangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Ziara imetoa fursa kwa pande zote mbili kuweza kujadili namna bora ya kuboresha maeneo ya vipaumbele katika sekta ya uwekezaji.

Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Uwekezaji wa Norway (Norfund), Bw. Tellef Thorleifsson akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) wakati alipomtembelea ofisini kwake na kufanya nae mazungumzo leo jijini Dar es Salaam

Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mfuko wa Uwekezaji wa Norway (Norfund), Bw. Erik Sandersen akiongea na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) (hayupo pichani)  wakati ujumbe huo ulipomtembelea ofisini kwake na kufanya nae mazungumzo leo jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) akiongea na Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Uwekezaji wa Norway (Norfund), Bw. Tellef Thorleifsson katika ofisi ndogo za wizara jijini Dar es Salaam

Balozi wa Norway nchini, Mhe. Baalozi, Ms. Elisabeth Jacobsen akifafanua jambo mbele ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb) pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Uwekezaji wa Norway (Norfund), Bw. Tellef Thorleifsson






Monday, January 27, 2020

WAZIRI PROF. KABUDI AKUTANA NA KUPOKEA HATI ZA UTAMBULISHO WA MABALOZI WASIO NA MAKAZI NCHINI


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb)  amekutana na kupokea hati za utambulisho kutoka kwa Mabalozi Wateule wasio na makazi hapa nchini leo Jijini Dar es Salaam.

Mabalozi waliowasilisha nakala za hati za utambulisho ni Balozi wa Ureno Mhe. Balozi Maria Amelia Maio de Paiva mwenye makazi jijini Maputo, Balozi wa Ufilipino, Mhe. Balozi Alex G. Chua ambae makazi yake yapo jijini Nairobi, Balozi wa Jamaica Mhe. Balozi Angela Veronica Comfort mwenye makazi jijini Pretoria na Balozi wa Austria, Mhe. Balozi Dkt. Christian Fellner ambae makazi yake ni Nairobi.

Wengine ni Balozi wa Ghana Mhe. Fransisca Ashietey-Odunton mwenye makazi Jijini Nairobi, Balozi wa Venezuele, Mhe. Jesús Agustin Manzanilla Puppo ambae makazi yake yapo Jijini Nairobi pamoja na Balozi wa Djibouti Mhe. Balozi Yacin Elmi Bouh mwenye makazi Nairobi.                                             
Awali kabla ya kukabidhi hati za utambulisho kwa Mhe. Waziri, Mabalozi wateule walipata semina kutoka kwa Mkuu wa Itifaki, wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb)  akiangalia nakala ya hati ya utambulisho ya Balozi wa Ureno Mhe. Balozi, Maria Amelia  Maio de Paiva

Balozi wa Ghana Mhe. Fransisca Ashietey-Odunton akimkabidhi Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) nakala ya hati ya utambulisho


Balozi wa Ufilipino, Mhe. Balozi Alex G. Chua akimsikiliza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) wakati alipokuwa akipatiwa ufafanuzi wakati wa mazungumzo mara baada ya kumkabidhi Waziri nakala ya hati ya utambulisho
   Balozi wa Jamaica Mhe. Balozi Angela Veronica Comfort akimkabidhi nakala ya utambulisho Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi (Mb)
  Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) akikagua nakala ya hati ya utambulisho ya Balozi wa Austria, Mhe. Balozi, Dkt. Christian Fellner
   Balozi wa Venezuele, Mhe. Jesús Agustin Manzanilla Puppo akimfafanulia baadhi ya maneno  yaliyopo kwenye nakala ya hati ya utambulisho Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi (Mb)
  Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba Kabudi (Mb) akiangalia nakala ya hati ya utambulisho kutoka kwa Balozi wa Djibouti Mhe. Balozi Yacin Elmi Bouh
 
   Mkuu Mkuu wa Itifaki, wa Wizara hiyo Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge (mwenye tai ya rangi ya chungwa) akiwapa Semina Mabalozi wateule kabla ya kuwasilisha nakala za Hati zao kwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
   Mkuu Mkuu wa Itifaki, wa Wizara hiyo Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge (mwenye tai ya rangi ya chungwa) akiwapa Semina Mabalozi Wateule









Sunday, January 26, 2020

TANZANIA, INDIA ZAAHIDI KUENDELEZA UHUSIANO WA KIDIPLOMASIA, KUKUZA MAENDELEO


Tanzania na India zimeahidi kuendeleza uhusiano wa kidiplomasia pamoja na  kushirikiana katika kuhakikisha kuwa na maendeleo endelevu baina ya nchi hizo mbili. 

Akihutubia sherehe za maadhimisho ya 71 ya Jamhuri ya India, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) amesema kuwa Tanzania na India ni ndugu na nchi hizo zitaendelea kushikiana katika kuhakikisha kuwa maendeleo ya diplomasia ya uchumi baina ya nchi hizo yanakuwa kila wakati.

"Nchi ya Tanzania na India zina uhusiano mzuri, imara na wa muda mrefu ulianzishwa na baba wa Taifa Mwl. Julias Nyerere pamoja na Mahatma Gandhi. Na uhusiano huu umekuwa ukisaidia kuimarisha maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kisiasa" alisema Dkt. Ndumbaro 

Dkt. Ndumbaro aliongeza kuwa "sisi Tanzania na India ni ndugu, kwa hiyo basi tunawatakia sana kila la kheri katika kuiletea India maendeleo…lakini pia tukumbuke kuwa maendeleo ya India ni maendeleo ya Tanzania pia,"  

Kwa sasa uchumi wa India na Tanzania umezidi kukuwa na kuendelea kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia baina ya mataifa hayo. India imekuwa msharika mzuri wa maendeleo nchini Tanzania katika sekta mbalimbali ikiwemo utalii, maji, afya, teknolojia na elimu. Msaada wa India katika sekta ya maji hadi sasa, imeweza kusaidia kusambaza maji safi na salama katika kwa jiji la Dar es Salaam pamoja na upanuzi na uboreshaji wa mitambo ya maji Zanzibar.

Aidha, kwa upande wa sekta ya elimu, Tanzania na India zimeshasaini makubaliano ya kushirikiana kujenga kituo cha ufundi na pia msaada wa kuendeleza vyuo vikuu vya Zanzibar ambavyo vinatoa ujuzi unaolengwa kuwaendeleza wanawake walio na elimu ndogo au isiyo rasmi.

Kwa upande wake, Balozi wa India chini Tanzania, Mhe. Balozi Shri Sanjiv Kohli ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa umoja na mshikamano ambao imekuwa ikionesha kwa India na kusema kuwa umoja huo umekuwa ni chachu ya maendeleo kwa Tanzania na Taifa la India.

"Napenda kuwafahamisha kuwa umoja na mshikamano wetu umekuwa chachu ya maendeleo baina ya mataifa haya mawili…..tukumbuke kuwa umoja ni nguvu na dhamira yetu ni kushirikiana na mataifa yote duniani. Na dhamira yetu ni kuishi kwa amani umoja na mshikamano ili kukuza uchumi wetu," Alisema Balozi Kohli

Aidha, Balozi Kohli amebainisha kuwa Tanzania itaendelea kuwa ya kipekee kwa taifa la India kutokana na mshikamano ambao imekuwa ikionesha kwa nchi ya India kijamii, kisiasa na kiuchumi.

"India inajivunia kuwa na uhusiano na mzuri na Tanzania ambao umewezesha mataifa haya kufanya biashara, uwekezaji, kujenga uwezo, ujenzi wa miundiombinu pamoja na maendeleo ya kiuchumi," ameongeza Balozi Kohli.


Balozi wa India nchini Tanzania, Mhe. Balozi Shri Sanjiv Kohli akihutubia wageni waalikwa (hawapo pichani) wakati wa maadhimisho ya miaka 71 ya Jamhuri ya India  yaliyofanyika mwishoni mwa wiki katika ofisi za Ubalozi wa India jijini Dar es Salaam. Kulia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Damas Ndumbaro.    

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Damas Ndumbaro (Mb) akiwasilisha hotuba yake wakati wa maadhimisho ya miaka 71 ya Jamhuri ya India yaliyofanyika katika ofisi za Ubalozi wa India mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam. Kulia kwake ni Balozi wa India nchini Tanzania, Kohli
Baadhi ya wageni waalikwa wakifuatilia/kusikiliza hotuba ya mgeni rasmi (Dkt. Ndumbaro) hayupo pichani wakati wa sherehe za maadhimisho ya miaka 71 ya Jamhuri ya India yaliyofanyika mwishoni mwa wiki katika ofisi za Ubalozi wa India jijini Dar es Salaam  





Thursday, January 23, 2020

BALOZI KANALI IBUGE AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA MABALOZI MBALIMBALI, WAKUU WA MASHIRIKA YA KIMATAIFA YALIPO NCHINI


 Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert A. Ibuge amekutana na kufanya mazungumzo na Mabalozi mbalimbali wanaowakilisha nchi zao hapa nchini pamoja na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa tarehe 22 na 23 Januari 2020 katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Pamoja na mambo mengine, mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia baina ya Tanzania na nchi hizo na mashirika hayo.

Mabalozi hao ni Balozi wa Visiwa vya Comoro, Mhe. Balozi Ahamada Elbadaour Mohamed, Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Balozi Frederic Clavie, Balozi wa Denmark nchini Mhe. Balozi Mette Norgaard, Balozi wa Iran nchini, Mhe. Balozi Mousa Farhang, Balozi wa Ethiopia nchini, Mhe. Balozi Yonas Yosef Sanbe, pamoja na Balozi wa Italia nchini, Mhe. Balozi Roberto Mengoni.

Mbali na Mabalozi, Mkuu wa Itifaki, Balozi Kanali Ibuge amekutana na Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa ambao ni Naibu Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) Bw. James Gitau na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Aga Khan (AKDN) Bw. Amin Kurji.



Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akimfafanulia jambo Balozi wa Comoro nchini Tanzania Mhe. Balozi Ahamada Elbadaour Mohamed wakati wa mazungumzo yaliyofanyika 22 Januari 2020 katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Balozi wa Comoro nchini Tanzania Mhe. Balozi Ahamada Elbadaour Mohamed akiongea na Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati wa mazungumzo yaliyofanyika 22 Januari 2020 katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Balozi Frederic Clavie akimweleza jambo Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati wa mazungumzo yaliyofanyika leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibugea kiongea na Balozi wa Ethiopia nchini, Mhe. Balozi Yonas Yosef Sanbe
Balozi wa Ethiopia nchini, Mhe. Balozi Yonas Yosef Sanbe akiongea na Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Wilbert Ibuge  
Balozi wa Iran nchini, Mhe. Balozi Mousa Farhang akimsikiliza Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa ajili ya mazungumzo leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Denmark nchini Mhe. Balozi Mette Norgaard akimsikiliza Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa ajili ya mazungumzo leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Italia nchini Meh. Balozi Roberto Mengoni akimsikiliza Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge wakati walipokutana kwa ajili ya mazungumzo leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akiongea na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Aga Khan (AKDN) Bw. Amin Kurji

Naibu Rais wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) Bw. James Gitau, akiwa katika mazungumzo na Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge.  Mazungumzo yaliyofanyika leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

Mkuu wa Itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Kanali Wilbert Ibuge akimfafanulia Naibu Rais wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) Bw. James Gitau wakati wa mazungumzo yaliyofanyika leo katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam





Monday, January 20, 2020

WIZARA YAWASILISHA TAARIFA YA UTEKELEZAJI KWA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA MAMBO YA NJE, ULINZI NA USALAMA JIJINI DODOMA



Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (aliyevaa miwani) akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Wizara kwa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama katika ukumbi wa Bunge jijini Dodoma, kulia ni Naibu Katibu Mkuu wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Ramadhan Mwinyi.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (aliyevaa miwani) akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Wizara kwa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama katika ukumbi wa Bunge jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Mussa Azzan Zungu  (kushoto) akisikiliza taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki iliyokuwa ikiwasilishwa na Mhe. Dkt. Ndumbaro.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) Mhe. Mussa Azzan Zungu na baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo wakisikiliza taarifa ya Wizara iliyokuwa ikiwasilishwa na mhe. Dkt. Ndumbaro
====================================================================================================

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imewasilisha taarifa ya utendaji kazi wake kwa kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na kusema Serikali ina mpango wa kujenga bandari ndogo katika ziwa Tanganyika mpakani mwa Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema hayo alipowasilisha taarifa  taarifa ya Utekelezaji wa Wizara ya mwezi Juni hadi Desemba 2019 mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama katika ukumbi wa Bunge jijini Dodoma.

“Mhe. Mwenyekiti, ili kunufaika kiuchumi kupitia DRC, tumepanga kujenga bandari ndogo katika Ziwa Tanganyika na kufungua Ubalozi mdogo katika mji wa Lubumbashi, mji huu uko umbali wa kilomita 3000 kutoka jijini Kinshasa,” alisema Dkt. Ndumbaro.

Amesema ujenzi wa bandari ndogo eneo la mpakani katika Ziwa Tanganyika kutawezesha bidhaa zinazozalishwa Tanzania kwenda nchini humo kiurahisi kuliko ilivyo sasa ambapo wafanyabiashara wanapitisha biashara zao nchini Zambia hadi kufika nchini DRC.

Aidha amesema Serikali inachukua hatua mbalimbali katika maeneo ya mpaka na nchi hiyo ikiwemo  kuhakikisha amani na usalama vinaimarishwa ili wananchi wa pande zote mbili wafanye biashara bila hofu yoyote.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Mussa Azzan Zungu imekutana na Menejimenti ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dodoma na kupata taarifa mbalimbali za utendaji wa Wizara.

Mhe. Zungu amesisitiza umuhimu wa Tanzania kushirikiana na DRC katika kuhakikisha amani na usalama vinaimarika hata baada ya Jeshi la Kulinda Amani la Umoja wa Mataifa (MONUSCO) kumaliza muda wake nchini humo.