Monday, December 5, 2022

DKT. TAX: WANAWAKE KUJIAMINI, KUJITUMA NDIYO SIRI YA MAFANIKIO

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) amewataka wanawake kujiamini, kujituma, kujiendeleza, kuwa waungwana na waadilifu wanapotekeleza majukumu yao kwani hiyo ndiyo siri ya mafanikio yao kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Dkt. Tax ametoa wito huo alipofungua programu ya mafunzo ya uongozi kwa viongozi wanawake Tanzania, yanayotolewa na Taasisi ya Uongozi, Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Tax ameongeza kuwa wanawake wanapswa kuimarisha uwezo wao, kutumia weledi, busara na werevu wa kushawishi, kutiana moyo, kujadili kwa umakini na kufanya maamuzi kwa umahiri na kujiamini, ili nafasi ya mwanamke katika uongozi ithaminiwe na kuthibitisha kuwa watoto wa kike na wanawake wanao uwezo.

Aidha, Waziri Dkt. Tax amesema kuwa uwakilishi wa wanawake katika nafasi za uongozi na ngazi za maamuzi umekuwa ukikua kwa kasi ndogo duniani kote licha ya jitihada mbalimbali za kitaifa na kimataifa zinazoendelea.  

Amesema Idadi ya wanawake viongozi katika taasisi za umma, asasi za kiraia na sekta binafsi imekuwa ikiongezeka ikilinganishwa na miongo iliyopita, lakini bado kasi ni ndogo.

“Tanzania imekuwa ya mfano katika suala hili kwani karibu kila sekta ina wanawake katika nafasi za uongozi na idadi imekuwa ikiongezeka. Tunao viongozi wanawake ambao wanatia hamasa kwa wanawake wanaochipukia katika masuala ya uongozi,” alisema Dkt. Tax 

Waziri Tax amesema ripoti ya Umoja wa Mataifa na Chama cha Mabunge Duniani inaonyesha kuwa hadi Januari 2021, nchi za Bara la Ulaya zikiwemo Norway, Finland, Iceland na Denmark, zinaongoza kwa kuwa na idadi ya wanawake viongozi kwa zaidi ya asilimia 50 kwenye nyadhifa za uwaziri na watendaji wakuu serikalini huku idadi ya wanawake wanaosimamia Wizara nchini Marekani imeongezeka kutoka asilimia 17 mwaka 2020 hadi asilimia 46 mwaka 2021. 

Kwa upande wa Tanzania, “takwimu zinaonesha kuwa tuna asilimia 26 ya wanawake viongozi. Idadi ya Mawaziri wanawake imeongezeka kutoka asilimia 21 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 35 mwaka 2022. Idadi ya Wakurugenzi wanawake imeongezeka kutoka asilimia 19 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 26 mwaka 2022. Idadi ya Majaji wanawake imeongezeka kutoka asilimia 39 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 40 mwaka 2022. Vilevile, idadi ya Wabunge Wanawake kwa mwaka 2022 ni asilimia 36.7 na walioteuliwa ni asilimia 57. Licha ya ongezeko hili, bado tuna kazi ya kuendelea kuwawezesha Wanawake katika sekta mbalimbali ili tuweze kufikia taifa lenye usawa wa kijinsia katika masuala ya Uongozi,” alieleza Waziri Tax .

Waziri Tax aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuandaa na kuboresha, sera, sheria, kanuni na miongozo ambayo ni rafiki na wezeshi kwa jinsia zote ili kuiwezesha jamii hususan mwanamke kukabiliana na changamoto. 

Awali akiongea kabla ya ufunguzi wa mafunzo hayo, Balozi wa Finland nchini, Mhe. Theresa Zitting amesema kuwa Serikali yake itaendelea kushirikiana na Taasisi ya Uongozi kutoa elimu kwa jamii kuhusu masuala ya usawa.

“Taasisi ya uongozi bado ina jukumu la kufundisha zaidi watu wengi katika jamii za kitanzania hususan kuwajengea uwezo wanawake ili kuwawezesha kuondokana na unyanyasaji wa kijinsia, kuwapa nafasi ya kutoa maamuzi na kuwaweseha kutekeleza majukumu yao vyeme kwenye jamii zao,” alisema Balozi Theresa.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la Wanawake la Umoja wa Mataifa (UN – Women) nchini, Bi. Hodan Addou amesema mwanamke anahitaji msaada na mafunzo ya uongozi ili kumuimarisha na kumwezesha kufanya maamuzi sahihi katika jamii. 

“Ni matumaini yangu kuwa kupitia mafunzo haya mtapata ujuzi ambao utawafanya kuwa viongozi bora katika jamii na kuwawezesha kufika malengo yenu kwa weledi zaidi ya sasa,” alisema Bi. Hodan

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akitoa hotuba ya ufunguzi wa programu ya mafunzo ya uongozi kwa viongozi wanawake Tanzania, yanayotolewa na Taasisi ya Uongozi, Jijini Dar es Salaam

Balozi wa Finland nchini, Mhe. Theresa Zitting akielezea fursa na changamoto za uongozi kwa mwanamke katika programu ya mafunzo ya uongozi kwa viongozi wanawake Tanzania, yanayotolewa na Taasisi ya Uongozi, Jijini Dar es Salaam

Mwakilishi wa Shirika la Wanawake la Umoja wa Mataifa (UN – Women) nchini, Bi. Hodan Addou akielezea masuala ya wanawake katika mafunzo ya uongozi kwa viongozi wanawake Tanzania, yanayotolewa na Taasisi ya Uongozi, Jijini Dar es Salaam

Meza kuu ikiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa mafunzo ya uongozi kwa viongozi wanawake Tanzania, yanayotolewa na Taasisi ya Uongozi, Jijini Dar es Salaam 



Saturday, December 3, 2022

BALOZI FATMA ASAINI KITABU CHA MAOMBOLEZO UBALOZI MDOGO WA CHINA

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab amesaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi wa Mdogo wa China uliopo Mazizini - Zanzibar, kufuatilia kifo cha Rais Mstafu wa Jamhuri ya Watu wa China, Jiang Zemin kilichotokea Novemba 30, 2022. 

Baada ya kusaini kitabu cha maombolezo, Balozi Fatma ametoa salamu za pole kwa Serikali ya Watu wa China na kuwasihi kuendelea kuwa wavumilivu wakati huu wa msiba wa kuondokewa na kiongozi wao mpenda amani, maendeleo na ustawi wa jamii yake.

Rais huyo wa zamani alifariki dunia akiwa na umri wa miaka 96, Pia Jiang aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Kikomunisti cha China kuanzia 1989 mpaka 2002 alichukua madaraka kutoka kwa Zhao Ziyang. Jiang atakumbukwa kwa kuwa kiongozi hodari na kuwa mwanzilishi wa kutaka kufanya mapinduzi ya kiuchumi hatua ambazo zimezaaa matunda na kupatikana kwa China moja na yenye maendeleo.

Serikali ya Tanzania na Watanzania wake kwa ujumla wanaungana na Serikali ya Watu wa China kuombeleza musiba huo mzito.

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akisaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi wa Mdogo wa China uliopo Mazizini - Zanzibar, kufuatilia kifo cha Rais Mstafu wa Jamhuri ya Watu wa China, Jiang Zemin


Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab akizungumza na Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China anayefanyika Kazi zake Zanzibar Mhe. Zhang Zhisheng baada ya kumaliza kutia saini kitabu cha maombelezi kufuatilia kifo cha Rais Mstafu wa Jamhuri ya Watu wa China Jiang Zemin
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma Rajab katika picha ya pamoja na Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China anayefanyika kazi zake Zanzibar Mhe. Zhang Zhisheng pamoja na Mkurugenzi wa Ofisi za Mambo ya Nje Zanzibar, Bi. Mariam Mrisho baada ya kumaliza kutia saini kitabu cha maombelezi kufuatilia kifo cha Rais Mstafu wa Jamhuri ya Watu wa China Jiang Zemin





RAIS DKT. SAMIA AWATAKA WANAWAKE KUFANYA KAZI KWA BIDII

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewasihi viongozi wanawake vijana kufanya kazi kwa bidii ili kufikia utekelezaji wa Ajenda 2030 ya Maendeleo Endelevu na Ajenda ya Umoja wa Afrika ya mwaka 2063. 

Mhe. Dkt. Samia ametoa wasaa huo wakati akifungua Kongamano la nne la Wanawake Vijana wa Mtandao wa Viongozi Wanawake Barani Afrika (AWLN) lililofanyika visiwani Zanzibar na kuwataka wanawake kufanya kazi kwa bidii ili kuendelea kuchangia maendeleo katika sekta mbalimbali kwenye jamii zao.

Pamoja na mambo mengine, Dkt. Samia amebainisha kuwa Tanzania inatambua na kuzingatia uwezo wa kitaaluma wa wanawake katika kufanya kazi na hivyo kupelekea idadi ya viongozi wanawake kuongezeka katika vyombo vya maamuzi (Bunge) kutoka asilimia 21.5 kwa mwaka 2005 hadi kufikia asilimia 37 mwaka 2020. 

“Idadi ya Majaji wanawake imeongezeka kutoka aslimia 34 mwaka 2005 hadi aslimia 39 mwaka 2022, Mabalozi wanawake na Makamishna Wakuu kutoka asilimia 3 mwaka 2005 hadi asilimia 21 mwaka 2022, Wakuu wa Mikoa Wanawake wamepanda kutoka aslimia 10 mwaka 2005 hadi asilimia 23 mwaka 2022, pamoja na Wakuu wa Wilaya Wanawake wameongezeka kutoka asilimia 19 mwaka 2005 hadi 29 mwaka 2022,” alisema Dkt. Samia

“Tunataka kuhakikisha kwamba wanawake wanaingia kwenye masoko ya kikanda na kuyatumia masoko hayo kama hatua ya kwenda mbali zaidi hadi kwenye masoko ya nje,” aliongeza Rais Dkt. Samia

Kwa Upande wake Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la watu wa Ethiopia, Mhe. Sahle-Work Zewde amesema kuwa ni wakati muafaka kwa Bara la Afrika kufanya mabadiliko ya uongozi kwa kuwapa nafasi za uongozi wanawake vijana ili waweze kuchangia maendeleo katika katika jamii zao pamoja na kuwahamasisha wengine kuwa wanawake wanaweza.

“Tunaamini kuwa wanawake vijana wakiendelezwa na kupatiwa mafunzo na ujuzi wa taaluma mbalimbali wataongoza vyema zaidi kuliko ilivyo kwa sasa, mfano wakipatiwa mafunzo ya usuluhishi wa migogoro watakuwa na msaada mkubwa wa kuchagiza amani katika jamii zetu,” alisema Mhe. Zewde

Awali akiongea katika kongamano hilo, Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini, Bw. Zlatan Milisic, amesema ni muhimu katika jamii wanawake kujumuishwa katika nafasi za maamuzi ili kupunguza migogoro katika jamii.

“Endapo wanawake vijana watashirikishwa katika hatua rasmi na zisizo rasmi za kufanya maamuzi ili kushughulikia changamoto mbalimbali katika jamii zetu itasaidia kuwajengea uwezo na kuwapatia maendeleo yao wenyewe,” alisema Bw. Millisci.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akitoa hotuba ya ufunguzi wakati wa  Kongamano la nne la Wanawake Vijana wa Mtandao wa Viongozi Wanawake Barani Afrika (AWLN) lililofanyika visiwani Zanzibar 

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Shirikisho la watu wa Ethiopia, Mhe. Sahle-Work Zewde akizungumza na washiriki wa Kongamano la nne la Wanawake Vijana wa Mtandao wa Viongozi Wanawake Barani Afrika (AWLN) lililofanyika visiwani Zanzibar  

Viongozi waandamizi wa Serikali wakifuatilia Kongamano

Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini (UN), Bw. Zlatan Milisic akiwasilisha salamu za UN kwa washiriki wa Kongamano la AWLN 





CFR YATAKIWA KUONGEZA WIGO WA PROGRAMU KUKIDHI MAHITAJI

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo cha Diplomasia alipowatunuku vyeti wahitimu 990 katika ngazi ya Astashahada ya Juu, Shahada, Stashahada na Astashahada katika fani ya diplomasia yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) (katikati) katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Chuo cha CFR wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo hicho  yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) (katikati) katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Chuo cha CFR na wahitimu wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam


Baadhi ya Wahitimu wa Chuo cha Diplomasia (CFR) wakiimba Wimbo wa Taifa wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam
Baadhi ya Wahitimu wa Chuo cha Diplomasia (CFR) wakiimba Wimbo wa Taifa wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Chuo cha Diplomasia (CFR) Balozi Ramadhan Mwinyi (aliyekaa) akiwa na wahitimu ambao walishinda tuzo za kuwa wanafunzi bora katika moja ya kozi zinazotolewa na chuo hicho wakati wa mahafali ya 25 ya chuo hicho yaliyofanyika jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (aliyekaa) akiwa na wahitimu ambao walishinda tuzo za kuwa wanafunzi bora katika moja ya kozi zinazotolewa na chuo hicho wakati wa mahafali ya 25 ya chuo hicho yaliyofanyika jijini Dar es Salaam
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (aliyekaa) akiwa na wahitimu ambao walishinda tuzo za kuwa wanafunzi bora katika moja ya kozi zinazotolewa na chuo hicho wakati wa mahafali ya 25 ya chuo hicho yaliyofanyika jijini Dar es Salaam
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) akiaga wahitimu aliowatunuku vyeti wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo cha Diplomasia baada ya kumalizika kwa mahafali hayo yaliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam

 

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb) amekitaka Chuo cha Diplomasia (CFR) kuongeza wigo wa program zake ili kukidhi mahitaji ya sasa na ya baadae. 

Dkt. Tax ametaka ongezeko hilo la wigo lifanyike kwa kuwatumia wataalamu wa ndani na nje ya chuo ambao wana uwezo na maono mapana. 

Waziri Dkt. Tax ametoa kauli hiyo leo Jijini Dar es Salaam wakati wa mahafali ya 25 ya Chuo hicho ambapo aliwatunuku vyeti wahitimu 990 katika ngazi ya Astashahada ya Juu, Shahada ya kwanza, Stashahada na Astashahada katika fani ya diplomasia. 

 “Mahitaji ya utaalamu katika Diplomasia yanaendelea kupanuka, kulingana na mahitaji yanayoendelea kujitokeza Kitaifa na Kimataifa,hususan katika Diplomasi ya Uchumi. Hivyo ni muhimu kwa Chuo kupanua progamu zake ili kukidhi mahitaji ya sasa, na siku za usoni. Hatua hii iende sanjari na kuwatumia wataalamu ndani ya Chuo, na nje ya Chuo, wenye uwezo na maono mapana,” alisema Dkt. Tax. 

Dkt. Tax amekipongeza Chuo cha CFR kwa kazi nzuri wanayoifanya na kutoa wahitimu wenye ueledi na mahiri wanaotambulika kitaifa na kimataifa na kuwataka wahakikishe wanatekeleza mikakati yao kikamilifu na hivyo kukamilisha lengo la kuanzishwa kwa chuo hicho

Amewataka kuhakikisha wanashirikiana na taasisi nyingine ili kuongeza elimu na ujuzi na hivyo kunufaisha wanafunzi wao hasa ikizingatiwa kuwa dunia ya sasa inahitaji ushirikiano na taasisi nyingine. 

 Amesema CFR kimetoa wahitimu mahiri na ni matarajio ya Serikali kuwa kila mtumishi atatimiza wajibu wake kwa kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzingatia maadili ya kiutumishi ili kuendelea kutoa wahitimu wenye ubora wa kitaaluma wenye maadili mema na mwenendo mwema. 

Amewataka wanachuo wanaobaki kuendelea kujifunza kwa bidii na kuiga mfano wa wanaohitimu wa tabia njema na mwenendo mwema na kujituma katika masomo yao ili kuendelea kuilinda sifa nzuri ya chuo tangu kuanzishwa kwake. 

Amekitaka chuo kuongeza mafunzo ya strategia, kufanya tafiti mahsusi na kutoa ushauri kwa serikali na wadau wengine katika sehemu ya strategia na diplomasia na kuweka mikakati ya pamoja na kutoa ushauri kwa Serikali na wadau wake jinsi ya kuwa na mwelekeo sahihi wa kukabiliana na changamoto zinazoikabili Tanzania na dunia kwa ujumla. 

“Chuo lazima kiongeze mafunzo ya strategia, kifanye tafiti mahsusi na kutoa ushauri kwa serikali na wadau wengine katika sehemu ya strategia na diplomasia. Tafiti kama hizo zitachangia kuimarisha diplomasia na kuweka mikakati ya pamoja ya jinsi ya kukabiliana na changamoto zinazoikabili Tanzania na dunia kwa ujumla,’ alisema Dkt. Tax 

Amekitaka chuo cha CFR kuhakikisha kinaelimisha taifa kupitia mijadala na makongamano ili kupanua uelewa na kujenga uzalendo kwa kujumuisha jamii katika masuala ya strategia na diplomasia na kuongeza kuwa diplomasia na strategia ni vitu vipana, na vyote vinagusa kila eneo na kwamba ni vizuri Chuo kikajipanga kwendana na dunia inavyokwenda. 

“Chuo hiki hakina budi kuendelea kuelimisha taifa kwa mijadala na makongamano kwa lengo la kupanua uelewa kujenga uzalendo na kujumuisha jamii katika masuala ya strategia na diplomasia, haya hayako nje ya wigo wa shughuli zenu, diplomasia ni kitu kipana na strategia ni kitu kipana pia na vyote vinahusu karibu kila eneo, kwa hiyo ni vizuri tukaenda na dunia inavyokwenda, sasa tunaongelea diplomasia ya uchumi lakini pia ipo diplomasia ya ulinzi na katika maeneo mbalimbali, tujipange vyema kwa kujua dunia inaenda namna gani na mafunzo tunayotoa yanaendaje katika kukabiliana na changamoto tulizonazo katika eneo hili,” alisisitiza Dkt. Tax

Friday, December 2, 2022

FURSA ZA AJIRA



 

DKT. TAX AWATUNUKU SHAHADA MBALIMBALI WAHITIMU 7,777 WA CHUO KIKUU CHA DODOMA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma leo tarehe 02 Desemba 2022 ametunuku Shahada mbalimbali Wahitimu wa fani mbalimbali katika Mahafali ya 13 yaliyofayika katika Ukumbi wa Chimwaga jijini Dodoma.

Dkt. Tax amewapongeza wahitimu wote kwa kuhitimu masomo yao kwa mafanikio na kuwataka kusherehekea ushindi wa kumaliza chuo kwa kiasi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mahafali hayo, Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Lugano Kusiluka amesema anapongeza jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha elimu nchini na kuwataka watanzania kuendelea kumuunga mkono na kumuombea ili aendelee kuwa na maono makubwa ya kuliinua Taifa katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu.

“Kwa niaba ya Menejimenti, Watumishi na Wanafunzi wote wa Chuo Kikuu cha Dodoma natoa pongezi kwa Mhe. Rais Samia kwa mageuzi makubwa ya kijamii na kiuchumi hapa Tanzania. Wajibu wetu ni kuendelea kumuunga mkono na kumuombea ili Mungu amlinde na kumpa maono makubwa zaidi kwa ajili ya Taifa hili” alisema Prof. Kusiluka.

Pia amesema anampongeza Mhe. Rais Samia kwa kumteua Dkt. Tax kuwa Mkuu wa Chuo hicho kwani tangu kuteuliwa kwake Chuo hicho kinakwenda mbele katika masuala mbalimbali ikiwemo uboreshaji elimu.

Amesema Chuo hicho kinaendelea kujiimarisha ili kutimiza lengo la kutoa elimu bora kwa Watanzania ambapo hivi sasa chuo kinaendelea kutekeleza maboresho mbalimbali kupitia mpango unaoratibiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi ambao pamoja na mambo mengine umejikita katika kuboresha mitaala, teknolojia na kujenga madarasa ya kutosha.

Ameongeza kusema kuwa, Chuo hicho kinaendelea kutoa wahitimu bora ambapo hivi karibuni Chuo hicho kimeshika nafasi ya kwanza kwa wanafunzi wa sheria kushinda kwenye mashindano ya Kimataifa ya Sheria katika masuala ya Kibinadamu kwa Kanda ya Afrika.

Aidha, amesema Chuo hicho kinaendelea kukamilisha usajili wa wanafunzi kwa mwaka wa masomo wa 2023/2024 na kwamba usajili huo ukikamilika Chuo kitakuwa na jumla ya wanafunzi 34,574 wa fani mbalimbali sawa na asilimia 94 ya lengo la Chuo hicho la kudahili wanafunzi 40,000.

Kadhalika aliwapongeza wahitimu wote na kuwaasa kuwa makini na kutumia taaluma waliyoipata kujiendeleza na kuliendeleza Taifa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Chuo hicho Prof. Rwekaza Mukandala amesema Baraza hilo ambalo ni chombo muhimu cha kusimamia utekelezaji wa sera na mikakati mbalimbali ya maendeleo ya Chuo, linayo nia thabiti ya kutekeleza Mpango Mkakati wa Chuo hicho wa Mwaka 2021/2025 pamoja na kukamilisha miradi yote ya maendeleo ya Chuo hicho.

Pia amewaasa wahitimu kuwa mabalozi na taswira ya Chuo hicho popote wanapokwenda kwa kuzingatia yale yote waliyojifunza na kuwapongeza kwa elimu waliyoipata ambayo alisema ni rasilimali yao ya kudumu ambayo hakuna wa kuwapokonya.

Mhe. Dkt. Tax ametunuku Shahada za Awali, Uzamili, Uzamivu, Stashahada na Astashahada kwa wahitimu takribani 7,777 wa fani mbalimbali wa Chuo hicho katika mahafali ya 13 yaliyofanyika kwa siku mbili Chuoni hapo kuanzia tarehe 01 hadi 02 Desemba 2022.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma akitangaza kuwatunuku Shahada mbalimbali wahitimu wa Chuo hicho wakati wa sherehe ya Mahafali ya 13 yaliyofanyika chuoni hapo tarehe 1 na 2 Disemba 2022
Meza Kuu wakiwa wamesimama wakati wimbo wa Taifa ukiibwa kwenye sherehe ya mahafali ya 13 ya Chuo Kikuu cha Dodoma
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (katikati), Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Lugano Kusiluka (kushoto) na Mwenyekiti wa Baraza la Chuo hicho Prof. Rwekaza Mukandala (kulia) wakiwa katika maandamano ya Kitaaluma kwenye Mahafali ya 13 ya Chuo Kikuu cha Dodoma.
Sherehe za Mahafali ya 13 ya Chuo Kikuu cha Dodoma yakiwa yanaendelea
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma akiingia katika ukumbi wa Chimwaga wa Chuo Kikuu cha Dodoma kushiriki Mahafali ya 13 ya Chuo hicho
Sherehe za Mahafali ya 13 ya Chuo Kikuu cha Dodoma yakiwa yanaendelea

VACANCY ANNOUNCEMENT


 

VACANCY ANNOUNCEMENT


 

FURSA ZA UFADHILI WA MASOMO NCHINI ISRAEL


 

Wednesday, November 30, 2022

SERIKALI YAZINDUA MFUMO WA KIDIGITALI WA KUAINISHA FURSA ZA UWEKEZAJI






Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akiwasilisha hotuba ya ufunguzikwa niaba ya Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa katika hafla ya uzinduzi wa mfumo wa kidigitali unaoainisha fursa za uwekezaji zinazogusa malengo ya maendeleo endelevu 
Naibu Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Mhe. Exaud Kigahe akitoa salamu za Wizara katika hafla ya uzinduzi wa mfumo wa kidigitali unaoainisha fursa za uwekezaji zinazogusa malengo ya maendeleo endelevu

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP), Bi. Christine Musisi akieleza mkakati wa UNDP katika kuisaidia Tanzania kufikia malengo ya Maendeleo Endelevu


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akizindua mfumo wa kidigitali unaoainisha fursa za uwekezaji zinazogusa malengo ya maendeleo endelevu 





 

Tuesday, November 29, 2022

SERIKALI, UNAIDS WAZINDUA RIPOTI YA HALI YA UKIMWI DUNIANI 2022

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya Ukimwi (UNAIDS) wamezindua Ripoti ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2022 leo Jijini Dar es Salaam.

Hafla ya Uzinduzi wa ripoti hiyo imeongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Mhe. George Simbachawene kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa 

Wakati wa uzinduzi huo Mhe. Simbachawene amesema idadi ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) nchini yamepungua kwa asilimia 50 kutoka 110,000 mwaka 2010 hadi 54,000 mwaka 2021. 

Waziri Simbachawene amesema pia idadi ya vifo vinavyotokana na Virusi vya Ukimwi kupungua kwa zaidi ya asilimia 50 kutoka 64,000 mwaka 2010 hadi 29,000 mwaka 2021.

“Tanzania imeongeza juhudi za kuzuia maambukizi ya VVU ambapo maambukizi mapya katika miaka minne (2017-2021) iliyopita yalipungua kwa asilimia 38,” alisema Simbachawene. 

“Kama nchi tunaungana na kukubaliana na kaulimbiu ya Siku ya UKIMWI Duniani ya mwaka 2022 ya ‘kukusekana kwa usawa ni hatari’ ili kuhakikisha kuwa kila mtu nchini Tanzania anapata huduma bora za afya na VVU. Ili kukabiliana na tofauti katika upatikanaji na utumiaji wa huduma za afya, Tanzania imeandaa muswada wa bima ya Afya kwa Wote kwa lengo la kuhakikisha Huduma ya Afya kwa Wote. Dhamira ya Mkakati wa Kitaifa wa Afya wa 2021 - 2026 ni kutoa huduma za afya endelevu zenye viwango vinavyokubalika kwa wananchi wote bila vikwazo vya kifedha, kwa kuzingatia usawa wa kijiografia na kijinsia, aliongeza Mhe. Simbachawene.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UKIMWI (UNAIDS), Bi. Winnie Byanyima amesema kwa mujibu wa ripoti mpya ya UNAIDS iliyozinduliwa inabainisha kuwa hatua za haraka zinahitajika ili kukabiliana na kukosekana kwa usawa katika mapambano dhidi ya UKIMWI duniani. 

“Tunahitaji kushughulikia changamoto ya kukosekana kwa usawa kwa wanawake hasa wenye VVU. Asilimia 50 ya wanawake wanaofanyiwa ukatili wa kijinsia wanauwezekano wa kupata VVU. Katika nchi 33 duniani tangu mwaka 2015 - 2021 sawa na asilimia 41 ya wanawake walioolewa wenye umri wa miaka 15 - 24 wanaweza kufanya maamuzi yao wenyewe juu ya afya ya ngono. Njia pekee yenye ufanisi wa kukomesha unyanyasaji kwa waathirika wa UKIMWI na kufikia malengo ya maendeleo endelevu ni kuhakikisha afya, haki na ustawi wa pamoja vinapatikana kwa wakati,” alisema Bi. Byanyima

Tanzania imekuwa imefanikiwa kupunguza maambukizi na vifo vitokanavyo na ukimwi kwa asilimia 50, jitihada hizo zimeifanya Tanzania kuwa nchi ya mfano duniania katika udhibiti wa ugonjwa huu, ameongeza Bi. Byanyima 

Bi. Byanyima ameongeza viongozi wa mataifa mbalimbali dunia wanapaswa kuhakikisha usawa katika upatikanaji wa haki, huduma, sayansi bora na dawa, kwani kwa kufanya hivyo hakutasaidia tu waliotengwa bali pia kusaidia kila mmoja.

Nae mwakilishi wa Baraza la watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi Tanzania (Nacopha), Bi. Bahati Haule amesema kuna umuhimu wa jamii kupewa elimu dhidi ya masuala ya usawa na unyanyapaa kwa waathirika wa VVU kwa kuwa wengi wa walioathirika wamekuwa wakitengwa na kunyanyapaliwa katika jamii zinazowazunguka.

“Ni wakati muafaka kwa dunia na jamii zetu zinazotuzunguka kuungana pamoja katika kupinga unyanyasji dhidi ya waathirika wa VVU pamoja na kuhakikisha usawa katika haki na huduma vinapatikana, alisema Bi. Bahati 

Ripoti ya Siku ya Ukimwi Duniani 2022 inaongozwa na kauli mbiu ambayo ni kukusekana kwa usawa ni hatari.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Mhe. George Simbachawene akizungumza wakati wa uzinduzi wa Ripoti ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2022 leo Jijini Dar es Salaam. Wengine pichani ni Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel (kulia) na Mkurugenzi Mkaazi wa UNAIDS nchini Tanzania Bw. Martin Odiit 

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UKIMWI (UNAIDS), Bi. Winnie Byanyima, akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa Ripoti ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2022. Kulia ni Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel na kushoto ni mwakilishi wa Baraza la watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi Tanzania (Nacopha), Bi. Bahati Haule.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Mhe. George Simbachawene akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Ripoti ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2022 Jijini Dar es Salaam

Viongozi mbalimbali wakiongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Mhe. George Simbachawene pamoja naMkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UKIMWI (UNAIDS), Bi. Winnie Byanyima katika  uzinduzi wa Ripoti ya Ukimwi Duniani kwa Mwaka 2022 Jijini Dar es Salaam









Monday, November 28, 2022

MKURUGENZI MTENDAJI UNAIDS AWASILI NCHINI KWA ZIARA YA KIKAZI

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UKIMWI (UNAIDS), Bi. Winnie Byanyima amewasili nchini tarehe 27 Novemba , 2022. 

Mkurugenzi huyo atakuwepo nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi kuanzia Tarehe 28 Novemba hadi 6 Desemba, 2022.  Mara baada ya kuwasili nchini, Bi. Byanyima alipokelewa na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel

Akiwa nchini Bi. Byanyima atashiriki Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yatakayofanyika Mkoani Lindi pamoja na kushiriki uzinduzi wa taarifa ya Hali ya Ukimwi nchini pamoja na kukutana na Baraza la watu wanaoishi na VVU (Nacopha). 

Aidha, Bi. Byanyima, anatarajia kukutana kwa mazungumzo na viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Mapinduzi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UKIMWI (UNAIDS), Bi. Winnie Byanyima akiwasili nchini kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Novemba , 2022

Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel akiongozana na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UKIMWI (UNAIDS), Bi. Winnie Byanyima baada ya kuwasili nchini kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Novemba , 2022





Saturday, November 26, 2022

DKT. TAX AWAASA VIJANA KUIGA FALSAFA ZA UONGOZI WA NYERERE

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax amewaasa vijana kutumia vyema Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation kujifunza, kubadilishana mawazo juu ya falsafa za Mwalimu Nyerere pamoja na kuimarisha amani na umoja katika jamii. 

Dkt. Tax ametoa wito huo alipokuwa akifungua mafunzo yanayotolewa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation kwa kundi la kwanza la viongozi vijana 60 kutoka nchi zaidi ya 40 Barani Afrika tarehe 25 Novemba, 2022 usiku Jijini Dar es Salaam. Pamoja na mambo mengine, Dkt. Tax aliwasisitiza vijana hao kutumia mafunzo hayo kuinufaisha jamii inayowazunguka.

“Napenda kutumia fursa hii kuwasihi vijana wa kizazi kipya cha Viongozi wa Afrika na watu wa Afrika, kufanya kazi kwa umoja, ushirikiano, na imani thabiti, kwani bila kufanya hivyo ni vigumu kuwa na mustakabali wa Afrika tunayoitaka,” alisema Dkt. Tax.

Dkt. Tax aliongeza kuwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Uongozi Imara wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, imejipanga kuhakikisha vijana wanawezeshwa ili kuendeleza amani, usalama na maendeleo ya kijamii na kiuchumi. 

“Katika kuenzi mchango mkubwa wa Mwalimu Nyerere katika kukuza umoja, amani na maendeleo ya watu nchini Tanzania na Afrika kwa ujumla, Serikali inaendelea kuunga mkono mipango ya amani kwa kuchangia Misheni za ulinzi wa amani Barani Afrika na Kikanda. Leo hii Tanzania ni nchi ya 13 kwa ushiriki katika Operesheni za Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa Duniani,” aliongeza Dkt. Tax

Bara la Afrika limebarikiwa rasilimali nyingi, tuchanganye maarifa, ujuzi wa uongozi, na maliasili ilizonazo ili kupeleka bara la Afrika katika ngazi za juu zaidi. Kwa kufanya hivyo, vijana mtakuwa mmeenzi falsafa za uongozi za Mwalimu Nyerere, aliyeongoza mapambano ya kupigania uhuru, umoja, na kujenga misingi imara ya Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Awali akizungumza kabla ya ufunguzi wa mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation, Bw. Joseph Butiku alisema kuwa programu ya Mafunzo ya Uongozi kwa Vijana yanayotolewa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere ni mpango unaolenga kushirikisha viongozi vijana katika kutoa mafunzo, changamoto, kufafanua na kubadilisha mtazamo wa kizazi kipya cha Afrika kuwa viongozi wanaowajibika, wanaojitolea na wapenda amani. 

“Malengo ya taasisi yetu ni kutafiti na kueneza falsafa ya uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere, amani, umoja na maendeleo ya watu. viongozi wazuri na wenye tija wa sasa na wa siku zijazo wa bara hili,” alisema Bw. Butiku.

Mafunzo hayo yametolewa kwa vijana 60 kutoka mataifa mbalimbali ambayo ni Botswana, Burundi, Cameroon, Djibouti, Misri, Ethiopia, Gabon, Guinea, Kenya, Libya, Liberia, Namibia, Nigeria, Rwanda, Sudani, Sudani Kusini, Afrika Kusini, Tanzania, Uganda, na Zambia.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akiwasilisha hotuba ya ufunguzi katika hafla ya ufunguzi wa mafunzo yanayotolewa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation Jijini Dar es Salaam

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akiwasilisha hotuba ya ufunguzi katika hafla ya ufunguzi wa mafunzo yanayotolewa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation Jijini Dar es Salaam

Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation, Bw. Joseph Butiku akielezea mkakati wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere wa kuwaendeleza na kuwajengea vijana viongozi uwezo 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akipokea tuzo ya heshima kutoka kwa Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation, Bw. Joseph Butiku baada ya kufungua mafunzo kwa viongozi vijana. Mafunzo hayo yanayotolewa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation Jijini Dar es Salaam  

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation, Bw. Joseph Butiku na baadhi ya viongozi vijana walioshiriki katika mafunzo yanayotolewa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere Foundation Jijini Dar es Salaam