Saturday, October 21, 2023

WAZIRI MAKAMBA APOKEA HATI ZA UTAMBULISHO ZA MWAKILISHI MKAZI WA UNDP

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) akipokea Hati za Utambulisho za mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) akipeana mikono na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara baada ya kupokea Hati za Utambulisho za mwakilishi huyo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) akizungumza na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara baada ya kupokea Hati za Utambulisho za mwakilishi huyo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

 

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) baada ya kukabidhi Hati zake za Utambulisho katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) katika picha na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara baada ya kupokea Hati za Utambulisho za mwakilishi huyo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) na ujumbe wake (kulia) katika picha na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara na ujumbe wake (kushoto) baada ya kupokea Hati za Utambulisho za mwakilishi huyo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.





 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. January Makamba (Mb.) amepokea Hati za Utambulisho za mwakilishi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) nchini, Bw. Shigeki Komatsubara katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

 

Mara baada ya kupokea nakala za hati hizo, Mhe. Waziri Makamba amemhakikishia Bw. Komatsubara kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na UNDP ili kusogeza mbele agenda yake ya maendeleo na hivyo kuinua maisha ya watanzania kisiasa, kijamii na kiuchumi.

 

Mhe. Waziri amesema Tanzania na UNDP zimekuwa zikishirikiana kutekeleza mipango ya maendeleo kwa kuwa zina lengo la kuboresha maisha ya watu kupitia maeneo ya utawala wa demokrasia, ukuaji uchumi, maendeleo endelevu  mazingira endelevu na uhimilivu wa mabadiliko ya tabia nchi.

 

Waziri Makamba ameongeza kuwa Tanzania inathmini na kutambua jitihada za UNDP katika kukabiliana na madhara yaliyotokana na janga la UVIKO 19

 

Kwa upande wake Mwakilishi wa UNDP nchini, Bw. Komatsubara ameahidi kufanya kazi kwa bidii ili kuendeleza jitihada za UNDP nchini na kuongeza kuwa atakuwa sio tu Balozi mzuri wa Tanzania bali pia atakuwa mtangaza mazuri ya Tanzania kupitia kazi zake.

 

Bw. Komatsubara ameongeza kuwa ofisi yake ina nia ya kusaidia Tanzania kujenga uwezo kwa watu wake ili kutekeleza kwa ufanisi mipango ya maendeleo na kwamba atahakikisha UNDP inaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha kuwa ajenda ya maendeleo inafanikishwa.


Friday, October 20, 2023

RAIS DKT. MWINYI AFUNGUA KIKAO CHA 77 CHA TUME YA AFRIKA YA HAKI ZA BINADAMU NA WATU

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea na jitihada mbalimbali katika kuhakikisha haki za binadamu zinalindwa na kutekelezwa kwa mujibu wa mikataba ambayo Tanzania ni mwanachama.

 

Kauli hiyo imetolewa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi wakati akifungua Kikao cha 77 cha Kawaida cha Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kilichofanyika jijini Arusha tarehe 20 Oktoba 2023.

 

Mhe. Dkt. Mwinyi ambaye alimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye ufunguzi  wa kikao hicho amesema kuwa jitihada za Serikali za kulinda na kuimarisha haki za binadamu zimewezesha kwa kiasi kikubwa kuboresha hali ya upatikanaji wa haki mbalimbali zikiwemo haki ya usawa mbele ya sheria, uhuru wa kutoa maoni, uhuru wa kuabudu, haki ya kumiliki mali, na uhuru wa vyombo vya habari.

 

“Kwa taarifa ni kwamba kutokana na uhuru huo wa vyombo vya habari, hivi sasa Tanzania ina vyombo vya habari vingi ikiwemo Radio 210,Televisheni 56, Magazeti 288 pamoja na mitandao mbalimbali ya kijamii. Pia tumefikia hatua kubwa ya kuimarika kwa uhuru wa kidemokrasia, haki za wanawake, watoto na watu wenye ulemavu kwa kuzingatia usawa wa kijinsia,” amesema Mhe. Rais Dkt. Mwinyi.

 

Kadhalika ameongeza kusema,  Tanzania na Afrika kwa ujumla  inaheshimu haki za binadamu na watu kwa kuzingatia utamaduni, maadili na tunu kama waafrika ambapo katika kutekeleza jukumu hili Serikali ya Tanzania inasimamia haki za binadamu kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na pia kanuni na taratibu zilizopo.

 

“Katika Katiba yetu, haki za binadamu zimeainishwa kuanzia Ibara ya 12 hadi 24 lakini pia Katiba yetu kuanzia Ibara ya 25 hadi 30 imeanisha wajibu wa kila raia” amesisitiza Mhe. Rais Dkt. Mwinyi.

 

Pia ameeleza kuwa katika kuhakikisha haki za binadamu na watu zinalindwa na kutetewa kikamilifu hapa nchini, Serikali ilianzisha Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ambayo ni Taasisi ya Kitaifa yenye jukumu la kulinda, kutetea na kuhifadhi haki hizo.

 

Akizungumzia hali ya ulinzi wa haki za binadamu barani Afrika amesema bado jitihada za pamoja zinahitajika ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazorejesha nyuma jitihada hizo ikiwemo mapinduzi ya Serikali zilizo madarakani, vita vya wenyewe kwa wenyewe, mila na desturi zisizofaa, ukatili wa kijinsia, athari hasi za utandawazi na uelewa mdogo wa wananchi kuhusu haki zao.

 

Mhe. Rais Dkt. Mwinyi alitumia fursa hiyo pia kuwahamasisha washiriki kutenga muda wao na kutembelea vivutio vya utalii vinavyopatikana kote nchini pamoja na Zanzibar.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, Mhe. Prof. Remy Ngoy Lumbu ameipongeza Tanzania kwa kuendelea kuheshimu haki za binadamu na kuitaja  amani iliyopo kama alama na kielelezo cha ulinzi wa haki  hizo za binadamu.

“Nchi hii inaheshimu haki za binadamu na amani inatawala. Tanzania ina utamaduni wa kutatua changamoto zao kwa njia ya amani na katika hili tunapaswa kujifunza” alisisitiza Mhe. Lumbu.

 

Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Zanzibar, Mhe. Haroun Ali Suleiman amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar chini ya Uongozi wa Mhe. Dkt. Mwinyi imeendelea kulinda na kuheshimu haki za binadamu kwa kuboresha mazingira na huduma za kijamii ikiwemo afya, maji, miundombinu na elimu.

 

Awali akimkaribisha Mhe. Dkt. Mwinyi kuzungumza, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana amesema anamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kikao hicho muhimu kufanyika nchini na kwamba kikao hicho pamoja na mambo mengine kitajadili namna bora ya kuendelea kusimamia masuala ya haki za binadamu na watu barani Afrika.

 

Pia Mhe. Dkt. Chana amesema kikao hicho ambacho kilitanguliwa na vikao viwili vya Asasi za kiraia na Taasisi za Haki za Bianadamu, kimehudhuriwa na takribani wadau 1,000 kutoka Serikalini, Umoja wa Afrika, Umoja wa Mataifa, Umoja wa Ulaya, Asasi za Kiraia, waandishi wa habari na wananchi kwa ujumla.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akifungua rasmi Kikao cha 77 cha Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kilichofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha tarehe 20 Oktoba 2023. Mhe. ais Dkt. Mwinyi alimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye ufunguzi huo. Kikao hicho kitafanyika kuanzia tarehe 20 Oktoba 2023 hadi 09 Novemba 2023
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kikao cha 77 cha Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu kinachofanyika jijini Arusha kuanzia tarehe 20 Oktoba 2023 hadi 09 Novemba 2023.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora Zanzibar, Mhe. Haroun Ali Suleiman akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kikao cha 77 cha Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu

Mwenyekiti wa Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, Mhe. Prof. Remy Ngoy Lumbu naye akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kikao cha Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu
Sehemu ya Viongozi na wageni waalikwa wakishiriki Kikao cha 77 cha Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu
Sehemu nyingine ya washiriki

Picha ya pamoja




 

Thursday, October 19, 2023

BALOZI ULANGA AKUTANA NA BALOZI WA UBELGIJI

 

 

Mkurugenzi wa Biashara za Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi John Ulanga (kulia) akizungumza na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Huyghebaert (kushoto) alipomtembelea katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salam.

Mazungumzo yakiendelea

 

Mkurugenzi wa Biashara za Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi John Ulanga na ujumbe wake (kulia) akizungumza na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Huyghebaert na ujumbe wake (kushoto) walipokutana katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salam.

 
Mkurugenzi wa Biashara za Kimataifa na Diplomasia ya Uchumi Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi John Ulanga amekutana na kuzungumza na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Huyghebaert katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salam.

Mazungumzo ya viongozi hao yamelenga kujadiliana na kuangalia uwezekano wa kuimarisha uwekezaji wa makampuni ya Tanzania nchini Ubelgiji na makampuni ya Ubelgiji hapa nchini.

Wednesday, October 18, 2023

WATANZANIA WALIOKUWA ISRAEL WAREJEA NYUMBANI

 

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) (wa tatu kutoka kushoto) akizungumza na vijana wa Kitanzania waliorejeshwa nyumbani na Serikali kutoka nchini Israel kufuatia changamoto za kiusalama nchini humo wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) (wa pili kushoto) akizungumza na vijana wa Kitanzania waliorejeshwa nyumbani na Serikali kutoka nchini Israel kufuatia changamoto za kiusalama nchini humo wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo



Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akizungumza na vijana wa Kitanzania waliorejeshwa nyumbani na Serikali kutoka nchini Israel kufuatia changamoto za kiusalama zilizoikumba nchini hiyo katika uwanja wa ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam kuwapokea vijana hao

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akisalimiana na Bw. Lucas Malaki ambaye ni mmoja wa  vijana wa Kitanzania waliorejeshwa nyumbani na Serikali kutoka nchini Israel kufuatia changamoto za kiusalama  zilizoikumba nchini hiyo

Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akizungumza na vijana wa Kitanzania (hawapo pichani ) ambao wamerejeshwa nyumbani na Serikali kutoka nchini Israel kufuatia changamoto za kiusalama zilizoikumba nchini hiyo, nyuma yake ni Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo na Mkurugenzi wa Idara ya Mashariki ya Kati wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Abdallah Kilima walipofika uwanja wa ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam kuwapokea vijana hao
Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) akimsikiliza kijana Lucas Malaki aliyerejea nchini kutoka Israel  kufuatia changamoto za kiusalama zilizoikumba nchini hiyo




Watanzania 9 waliokuwa nchini Israel wamerejea nyumbani leo tarehe 18 Oktoba 2023 na kulakiwa na Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza katika mapokezi ya Watanzania hao Naibu Waziri Byabato amesema kurejea nyumbani kwa Watanzania hao kunatokana na utekelezaji wa uamuzi wa Serikali ya Tanzania wa kuwarejesha nyumbani raia wake walioko nchini Israel ili waendelee kuwa salama.

 

Amesema Serikali kupitia Ubalozi wake wa nchini Israel iliweka utaratibu wa kuwarejesha Watanzania wote ambao wangetaka kurudi nyumbani na kuongeza kuwa Serikali itaendelea kuwashawishi Watanzania walioko nchini humo ili waone haja ya kurudi nyumbani hadi pale hali itakapotengemaa.

 

Amesema Serikali imefarijika kwa Watanzania hao kuitikia wito wa kuokoa maisha yao na anaamini kuwa Watanzania waliobaki nchini humo busara zao zitawaongoza na kuamua kurejea nyumbani ili wawe salama na kuongeza kuwa Serikali itawarejesha nyumbani watakapokuwa tayari kufanya hivyo.

 

Akizungumza baada ya mapokezi hayo mmoja wa Watanzania hao Bw. Lucas Malaki ameishukuru Serikali kwa kitendo cha kuwarejesha nyumbani na kusema kuwa kitendo hicho kimewafanya wajisikie fahari kuwa watanzania na kuwaondolea unyonge na kuongeza kuwa wanakichukulia kitendo hicho kuwa ni cha upendo na cha kizalendo na kuahidi kuwa wataendelea kuwa raia wema.

 

Watanzania hao wamerejeshwa nyumbani na Serikali kufuatia kuendelea kuzorota kwa  hali ya amani na usalama nchini Israel na maeneo mengine ya jirani tangu kikundi cha HAMAS kilipoishambulia Israel tarehe 7 Oktoba, 2023.