Tuesday, September 25, 2018

SALAMU ZA RAMBIRAMBI KUTOKA KWA VIONGOZI WA MASHIRIKA YA KIMATAIFA NA KIKANDA


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

SALAMU ZA RAMBIRAMBI KUTOKA KWA VIONGOZI WA MATAIFA MBALIMBALI NA MASHIRIKA YA KIMATAIFA NA KIKANDA


Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeendelea kupokea salamu za rambirambi kutoka kwa viongozi wa mataifa na mashirika mbalimbali ya kikanda na kimataifa kwenda kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kufuatia ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere iliyotokea kwenye Ziwa Victoria, Mkoani Mwanza tarehe 20 Septemba, 2018 na kusababisha vifo, majeruhi na upotevu wa mali.

Baadhi ya salamu zilizopokelewa zinatoka kwa Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Mheshimiwa Dkt. Stergomena Lawrence Tax na Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyopo Kisumu, Mheshimiwa Dkt. Ali Said Matano

Salamu zingine zimetoka kwa Waziri wa Nchi wa Uingereza, Mheshimiwa Harriett Baldwin na Ofisi ya Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) nchini kwenda kwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga.

Viongozi hao wameeleza kusikitishwa kwao na taarifa za vifo vilivyosababishwa na  ajali hiyo na kuwatakia majeruhi kupona haraka.

Sehemu ya nukuu za salamu hizo zinasema “Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, kwa niaba ya Sekretarieti ya SADC na mimi binafsi naomba kwa dhati upokee salamu zetu za pole kwako wewe Mheshimiwa Rais, Serikali, Wananchi wa Tanzania na familia zilizopoteza wapendwa wao. Tunaomboleza na Watanzania na tunaomba Mungu awape nguvu familia zilizoathirika na tukio hilo na roho za marehemu zipate pumziko la amani milele. Ninawaombea majeruhi uponyaji wa haraka” ni sehemu ya nukuu ya salamu kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. Stergomena.

Naye Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria Kisumu, Mhe. Dkt. Matano, ametoa pole kwa Watanzania na kukumbusha umuhimu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kujenga  Kituo cha Uratibu na Uokoaji Majini (MRCC) iliyokubalika ijengwe jijini Mwanza.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dodoma.
25 Septemba, 2018


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.