Sunday, September 2, 2018

Waziri Mkuu afungua Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na China

Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa akitoa hotuba wakati wa ufunguzi wa Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na China ambapo zaidi ya Kampuni 80 kutoka nchi hizi mbili zilishiriki. Wakati wa Kongamano hilo Mhe. Waziri Mkuu alizialika kampuni za biashara na uwekezaji kutoka China kuja kuwekeza Tanzania na kusisitiza kuwa mazingira ya uwekezaji ni mazuri. Mhe. Waziri Mkuu yupo nchini China kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika utakaofanyika tarehe 3 na 4 Septemba, 2018 jijini Beijing.


Sehemu ya wageni waalikwa wakfuatilia hotuba ya Mhe. Waziri Mkuu

Sehemu ya wageni kutoka Tanzania akiwemo Mzee John Cheyo wakifuatilia mkutano

Balozi wa Tanzania nchini China Mhe. Mbelwa Kairuki akitoa neno wakati wa Kongamano hilo
Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Bw. Geofrey Mwambe akiwa pamoja na wageni wengine walioshiriki kongamano hilo

Mkurugenzi Mkuu wa Eneo Maalum la Uwekezaji (EPZA), Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia naye akifuatilia Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na China

Balozi wa China nchini Tanzania, Mhe. Wwang Ke naye alishiriki kongamano hilo

Sehemu nyingine ya wageni waalikwa

Mshereheshaji kwenye kongaano hilo Bw. Laizer Mollel akitoa ratiba kabla ya kuanza kwa kongamano

Mhe. Balozi Kairuki akihojiwa na Mwandishi kutoka TBC, Bi. Anna Mwasyoke kuhusu umuhimu wa kongamano hilo kwa Tanzania
====================================================
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa amewakaribisha wafanyabiasha na wawekezaji kutoka China kuja Tanzania kuwekeza kutokana na  mazingira rafiki ya uwekezaji na hali ya amani na utulivu iliyopo nchini.

Waziri Mkuu alitoa rai hiyo wakati akifungua  Kongamano la Biashara kati ya Tanzania na China lililowashirikisha wafanyabiashara zaidi ya 80 kutoka nchi hizi mbili. Mhe. Majaliwa ambaye yupo nchini China kwa ajili ya kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya Afrika na China (FOCAC) alitumia fursa hiyo kukutana na wafanyabiashara hao ili kuwaeleza hali ya uwekezaji nchini katika

Mhe. Majaliwa alisema kuwa, Tanzania imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za kuvutia wawekezaji ambazo kwa kiasi kikubwa  zimezaa matunda ambapo katika Ripoti ya uwekezaji duniani kwa mwaka 2018 imeitaja Tanzania kuwa kitovu cha uwekezaji kwa ukanda wa Afrika Mashariki ambapo imewekeza takribani dola za marekani bilioni 1.2.

Mhe. Majaliwa aliongeza kuwa, Tanzania inamazingira mazuri sana ya uwekezaji ikiwemo ardhi nzuri kwa kilimo cha mazao mbalimbali kama miwa, mpunga, ngano, mahindi, Mhogo na katani. Alisema kuwa, jumla ya hekta milioni 44 za ardhi zinafaa kwa kilimo na zaidi ya hekta milioni 29 zinafaa kwa kilimo cha umwagiliaji.

Akizungumzia sekta ya madini, Mhe. Majaliwa alisema kuwa ni moja ya sekta muhimu inayochangia pato la taifa na kuwahamashisha wawekezaji kuchangamkia sekta hiyo hususan kwenye uchimbaji na uchakataji wa madini ya chuma na uchimbaji wa madini ya urani.

Kuhusu utalii, Mhe. Waziri Mkuu alisema kuwa Tanzania imekuwa ikifaidika kwa kiasi kikubwa kutokana na kujaliwa vivutio vingi vya utalii ikiwemo fukwe zilizopo Zanzibar, Mlima Kilimanjaro na Hifadhi ya Ngororngoro. Hata hivyo alisema bado sekta hii inahitaji wawekezaji hususan kwenye ujenzi wa miundombinu ya utalii kama vile hoteli na sekta ya huduma kwa watalii kwa ujumla.

Masuala mengine aliyowaeleza wawekezaji hao ambayo ni fursa kwao ni pamoja na eneo la teknolojia ya habari na mawasiliano ambapo kwa sasa soko ni kubwa  kutokana na ongezeko la watumiaji wa simu na mitandao hususan watu wanaoishi vijijini. Aliwakaribisha wawekezaji kuwekeza katika sekta hii katika maeneo ya ukarabati na utengenezaji wa vifaa vya mawasiliano na kujenga viwanda vya kuunganisha simu.

Mhe. Waziri Mkuu alihitimisha kwa kuhimiza wawekezaji kuja nchini na kusisitiza kuwa, “ukitaka kuwekeza Afrika karibu Tanzania”


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.