Sunday, September 2, 2018

Waziri Mkuu akutana na Watendaji wa Kampuni kubwa za China

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Kampini ya NORINCO ya nchini China, Bw. Zhang Gaunjie alipokutana naye kwa mazungumzo kuhusu uwekezaji nchini Tanzania.Mhe. Waziri Mkuu yupo nchi China kwa ajili ya kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya Afrika  na China (FOCAC) unaotarajiwa kufanyika tarehe 3 na 4 Septemba, 2018 jijini Beijing
Mhe. Waziri Mkuu akimkabidhi Bw. Gaunjie kitabu chenye taarifa kuhusu uwekezaji nchini Tanzania



Mhe. Waziri Mkuu akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Kampuni ya Zinjin Gold Mine ya nchini China, Bw. George Fang ambayo imewekeza katika uchimbaji na uchakataji wa madini ya dhahabu, shaba na zinki katika nchi tisa duaniani. Kampuni hiyo imeonesha nia ya kuja kuwekeza nchini kwenye sekta ya madini.
Ujumbe wa Tanzania ukifatilia mazungumzo kati ya Waziri Mkuu na Rais wa Kampuni ya Zinjin Gold Mine 


Mazungumzo yakiendelea
Mhe. Waziri Mkuu akiwa kwenye mazungumzo na Mwenyekiti wa Kampuni ya GNSG ambao wana nia ya kuwekeza katika maeneo ya viwanda (Industrial Parks)
Balozi wa Tanzania nchini China, Mhe. Mbelwa Kairuki akiteta jambo na Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania, Bw. Geofrey Mwambe. Pembeni ni Bibi Justa Nyange, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia


Mhe. Waziri Mkuu akizungumza na Mwenyekiti wa Kampuni ya Syngning Guangzhou ya nchini China, Bw. WU Haineng. Kampuni ambao wana nia ya kufanyabiashara na Tanzania katika zao la mhogo


========================================================
WAZIRI MKUU AKUTANA NA WATENDAJI WA KAMPUNI KUBWA ZA CHINA

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na Watendaji Wakuu wa Kampuni kubwa za China kwa lengo la kujadiliana nao kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na Kampuni hizo.

Mhe. Majaliwa ambaye yupo nchini China akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwenye Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jukwaaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) utakaofanyika tarehe 3 na 4 Septemba, 2018, ametumia fursa hiyo kukutana na  Watendaji hao katika hatua za kuhamasisha uwekezaji, biashara na maendeleo nchini.

Katika mkutano wake na Rais wa Kampuni ya NORINCO (China North Indust Bw. Zhang Gaunjie, Mhe. Waziri Mkuu amepongeza uwekezaji wa Kampuni hiyo nchini hususan kwa kuwa na miradi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania na kuikaribisha kuwekeza zaidi katika maeneo mengine hususan ujenzi wa miundombinu hasa ya Makao Makuu ya nchi. Mhe. Waziri Mkuu alimweleza Rais huyo kuwa, Tanzania inahitaji teknolojia ya kisasa ili kuwezesha ujenzi wa nyumba za gharama nafuu kwa ajili ya makazi hususan kwa Watumishi wa Serikali ambapo sasa Serikali imehamishia Makao Makuu Dodoma.

Kwa upande wake Bw. Zhang Ghaujie alieleza kuwa  Kampuni ya NORINCO ambayo imewekeza kwa kiasi kikubwa katika miradi ya Jeshi la Wanachi Tanzania, sasa ipo tayari kushiriki kwenye miradi mingi Zaidi nchini hususan ile ya ujenzi na kwamba kutokana na  uwezo na uzoefu mkubwa wa Kampuni hiyo katika sekta ya ujenzi itashirikiana na Tanzania kwenye miradi ya ujenzi wa makao makuu na bomba la mafuta.

“NORENCO  ipo tayari kuongeza maeneo ya ushirikiano na Tanzania na inao uwezo wa kushiriki katika kazi za ujenzi hususan kwenye miradi kama bomba la mafuta na Makao Makuu ya nchi” alisema Rais huyo.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amekutana na kufanya mazugumzo na Mwenyekiti wa Kampuni ya HEGNYA Cement, ambayo imeonesha nia ya kuja nchini kuwekeza kwenye ujenzi wa Kiwanda kikubwa cha saruji na Eneo la Viwanda (Indusrial Park) Mkoani Tanga. Kukamilika kwa mradi huo kutaongeza uzalishaji wa saruji nchini kwa tani milioni 7 kwa mwaka na kuzalisha ajira kwa Watanzania 4000.

Waziri Mkuu pia alipata fursa ya kukutana na Rais wa Kampuni ya Zinjin Gold Mine, Bw. George Fang. Katika mazungumzo yao, Mhe. Waziri Mkuu alimkaribisha kuja kuwekeza kwenye uchimbaji na viwanda vya uchakataji wa madini hususan Tanzanite. Mhe. Waziri Mkuu alimweleza kuwa madini ya Tanzanite ambayo yanapatikana Tanzania pekee yanahitaji mwekezaji makini ambaye atachimba, kuchakata na kuongeza thamani madini hayo kwa faida ya Tanzania.

“Tanzanite inapatikana Tanzania pekee. Tunatafuta mwekezaji makini wa kuchimba na kuchakata madini hayo ili kuona faida ya madini hayo muhimu kwa Tanzania” alisema Waziri Mkuu.

Kwa upande wake, Bw. Fang alimweleza Waziri Mkuu kuwa, kampuni ya Zijin ambayo imewekeza kwenye uchimbaji mkubwa wa madini ya dhahabu, shaba na zinki ipo tayari kuja nchini kuwekeza kwenye uchimbaji wa madini hayo chini ya Sheria Mpya ya Madini ya Tanzania. Pia alifurahishwa na taarifa ya Waziri Mkuu kuhusu uchimbaji wa madini ya Tanzanite na kumhakikishia kuwa kampuni yake inao uwezo wa kutafiti, kuchimba, kuchakata, kuongeza thamani na kutafuta masoko kwa madini yoyote ikiwemo Tanzanite.

“Kampuni ya Zijin Gold Mine ni Kampuni kubwa, inamiliki migodi katika majimbo 20 nchini China na imewekeza kwenye nchi 9 duniani. Ni ya pili katika uzalishaji wa  madini ya Zinki na inashikilia nafasi ya tatu katika uzalishaji wa shaba. Tunaona ni fursa muhimu kuja kuwekeza katika sekta ya madini nchini Tanzania. Tunahitaji ushirikiano wa kimkakati katika sekta ya madini ambao utafuata misingi ya uwazi kwa faida ya kila mmoja” alisisitiza Rais huyo.

Wakati huohuo, Mhe. Waziri Mkuu alizungumza na kumshukuru kwa kazi nzuri Rais wa Kampuni ya CCECC, ambayo inatekeleza miradi ya maendeleo nchini ukiwemo mradi wa Ubungo Interchange, ukarabati wa Reli ya Kati na Mradi mkubwa wa maji kwenye Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro. Pia alimtaka kukamilisha miradi haraka na kuongeza miradi zaidi kwenye ujenzi wa maeneo ya viwanda kwa ajili ya uwekezaji kwenye sekta ya kilimo hususan kwenye zao la korosho. Rais huyo alimhakikishia Waziri Mkuu kuwa, Kampuni yake itakamilisha miradi yote kwa wakati kama ilivyokubaliana na Serikali ukiwemo Mradi wa Ubungo, ambao utakamilika ifikapo mwezi Juni 2020.

Aidha, kampuni hiyo imeahidi kuongeza uwekezaji Tanzania huku wakitoa kipaumbele cha ajira kwa Watanzaia na kutumia rasilimali za Tanzania ili kutoa mchango mkubwa wa maendeleo ya nchi. Kampuni ya CCECC imewekeza Tanzania miradi yenye thamani ya takribani dola za Marekani bilioni 1.5 na kutoa fursa za ajira kwa Watanzania zaidi ya 4000.


Katika mkutano wake na Mwenyekiti wa Kampuni ya GNSG (Guangdong New South Group) ambayo ina nia ya kuwekeza kwenye ujenzi wa Eneo ya Viwanda (Industrial Parks) nchini,  Mhe. Waziri Mkuu alimhakikishia kuwepo kwa maeneo ya uwekezaji wa aina hiyo katika mikoa yote ya Tanzania na kumwagiza Mkurugenzi Mkuu wa Ukanda Maalum wa Uwekezaji (EPZA), Bw. Joseph Simbakalia kuhakikisha anaipatia Kampuni hiyo taarifa kamili za maeneo ya uwekezaji wa viwanda nchini ili kuwawezesha kufanya maamuzi haraka ya kuja nchini.

-Mwisho-

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.