Thursday, February 21, 2019

Tanzania na Umoja wa Ulaya waazimia kuimarisha Uhusiano

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Tanzania na Umoja wa Ulaya waazimia kuimarisha Uhusiano

Tanzania na Umoja wa Ulaya (EU) wamekubaliana kuimarisha uhusiano na ushirikiano kwa kufanya majadiliano ya mara kwa mara yatakayojengwa katika misingi ya kuaminiana, usawa, uwazi na kuheshimiana ili kujenga uelewa wa pamoja katika maeneo mbali mbali yenye changamoto kwa manufaa  mapana ya watu wa pande zote mbili.

Makubaliano hayo yamefikiwa wakati wa mazungumzo kati ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (Mb) na Mkurugenzi wa Idara ya Pembe ya Afrika na Afrika Mashariki, Huduma za Nje katika Umoja wa Ulaya, Bw. Patrick Simonnet wakati wa ziara yake iliyofanyika nchini kuanzia tarehe 17 hadi 20 Februari 2019.

Katika mazungumzo hayo, Mhe. Waziri aliushukuru Umoja wa Ulaya kwa misaada ambayo umekuwa ukiipatia Tanzania kwa ajili ya utekelezji wa miradi mbalimbali ya maendelea katika sekta za kilimo, nishati na ujenzi wa miundombinu ya barabara na viwanja vya ndege. “Umoja wa Ulaya ni mbia muhimu wa Tanzania katika shuguli za maendeleo tokea mahusiano rasmi ya kidiplomasia yalipoanzishwa mwaka 1975; baada ya kusainiwa kwa mkataba wa kwanza wa Rome baina ya kundi la nchi za Afrika, Caribbean na Pasifiki (ACP) na nchi wanachaama wa Umoja wa Ulaya”; alisema Mhe. Mahiga.

Viongozi hao walihitimisha mazungumzo yao kwa kuazimia kuendelea kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya pande mbili hizi katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na biashara, uwekezaji, ushirikiano wa maendeleo na usalama wa majini, hususan katika pwani ya Bahari ya Hindi. 
Aidha, walikubaliana kuimarisha ushirikiano katika nyanja za kimataiafa ikiwa ni pamoja na kusaidia juhudi za kudumisha na kuimarisha hali ya amani, usalama na utulivu katika eneo la Maziwa Makuu.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.
21 Februari 2019


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.