Monday, April 17, 2023

TANZANIA - WADAU WAMAENDELEO KUENDELEA KUSHIRIKIANA


Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) ameeleza utayari wa Serikali ya Awamu ya Sita chini na usimamizi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wa kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo katika kuboresha maisha ya wananchi. 

Waziri Tax ameeleza hayo leo tarehe17 Aprili 2023 alipokutana na kufanya mazungumzo kwa nyakati tofauti na Balozi wa Ireland nchini Mhe. Mary O’Neill, na Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa Bw. Zlatan Milisic jijini Dodoma. 

Waziri Tax akizungumza Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa Bw. Milisic ameeleza kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita yamefayika madiliko na maboresho makubwa yanayolenga kukuza Demokrasia na Utawala Bora na Haki za Binadamu. 

Waziri Tax sambamba na kumshukuru Bw. Malisic kwa kuendelea kusaidia programu mbalimbali za maendeleo nchini, aliongeza kusema mafanikio yaliyopatikana katika kuboresha maeneo hayo yameendelea kuwavutia wadau wa maendeleo kuwekeza na kusaidia katika sekta mbalimbali za maendeleo nchini. 

“Dunia imeendelea kushuhudia kazi nzuri inayoendelea kufanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi mahiri wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha hali ya Demokrasia na Utawala Bora nchini, hali hii imeendelea kuwavutia wadau wengi wa maendeleo kushirikiana na Tanzania; na Serikali ya Tanzania inaahidi kuendelea kushikiana na wadau wote katika kuondoa umaskini na kuboresha maisha ya Wananchi” ameeleza Dkt. Tax.

Kwa upande wake Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa Bw. Milisic amepongeza juhudi zilizofanywa na Serikali ya Tanzania katika kuboresha hali ya Demokrasia na Utawala Bora nchini, huku akiahidi kuendelea kufanya kazi kwa ukaribu na Serikali kupitia nyanja mbalimbali ili kuendelea kuboresha hali ya maisha ya Wananchi.

Wakati huohuo Waziri Tax ameipongeza na kuishukuru Serikali ya Ireland kupitia Balozi wake nchini Mhe. O’Neil kwa kuendelea kufadhili programu na miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya kuondoa umaskini kupitia TASAF. 

Kwa upande wake Balozi O’Neil ametoa pongezi na kueleza kuridhishwa kwake na namna Serikali ya Tanzania inavyojidhatiti katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijami kwa wananchi huku ikizingatia na kufuata misingi ya Utawala Bora, huku akitolea mfano usimamizi mzuri wa progamu na miradi ya kuondoa umaskini nchini kupitia TASAF. 

Kadhali Waziri Tax alitumia fursa hiyo kumweleza Balozi wa Ireland Mhe. O’Neill kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea kuwakaribisha wawekezaji kutoka nchini Ireland kuwezekeza nchini katika sekta mbalimbali kama vile kilimo, viwanda na uchumi wa buluu. 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.