Wednesday, January 24, 2024

MAKAMU WA RAIS WA CUBA ATEMBELEA TAASISI YA MWALIMU NYERERE NA KUMJULIA HALI MAMA MARIA NYERERE

Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa ametembelea Makao Makuu ya Taasisi ya Mwalimu Nyerere yaliyopo jijini Dar es Salaam na kuzungumza na Wafanyakazi wa Taasisi hiyo pamoja na Wajumbe wa Umoja wa Urafiki wa Tanzania na Cuba.


Mara baada ya kuwasili, Mhe. Mesa alipokelewa na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Bw. Joseph Butiku pamoja na Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi hiyo, Mhe. Stephen Wasira.


Pamoja na mambo mengine Mhe. Mesa alipokea taarifa kuhusu utendaji wa Taasisi hiyo isiyo ya Serikali ambayo ilianzishwa mwaka 1996 kwa lengo la kuhamasisha  amani, umoja na maendeleo ya watu pamoja na kuenzi mchango wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika utu na maendeleo ya watu pamoja na kutunza kumbukumbu mbalimbali za kazi zake ikiwemo vitabu, majarida, machapisho na picha.



Wakati huohuo, Mhe. Mesa amemtembelea, Mjane wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mama Maria Nyerere kwenye makazi yake jijini Dar es Salaam kwa lengo la kumsalimia na kumjulia hali.



Katika mazungumzo yao, Mhe. Mesa amemweleza Mama Maria kuwa amewiwa kumtembelea kama ishara ya kuenzi urafiki wa Tanzania na Cuba ulioasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Hayati Fidel Castro na mchango mkubwa wa Mwalimu Nyerere katika kujenga amani, umoja na mshikamano na kuwa mstari wa mbele kwenye harakati za ukombozi kusini mwa Afrika. Kadhalika amemtakia afya njema na maisha marefu Mama Maria.


Kwa upande wake Mama Maria amemshukuru Mhe. Mesa kwa kutenga muda na kumtembelea.


Mazungumzo kati yao yalihudhuriwa pia na Watoto wa Hayati Baba wa Taifa akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Makongoro Nyerere.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Bw. Joseph Butiku akimpokea Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa alipotembelea Taasisi hiyo tarehe 24 Januari 2024. Mhe. Mesa alifanya ziara ya siku tatu nchini kuanzia tarehe 23 hadi 25 Januari 2024

Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa akizungumza alipotembelea Taasisi ya Mwalimu Nyerere wakati wa ziara yake nchini
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Bw. Joseph Butiku akimzawadia Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa vitabu na machapisho mbalimbali ya Hayati Mwalimu Nyerere alipotembelea Taasisi hiyo tarehe 24 Januari 2024.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Bw. Joseph Butiku akizungumza wakati wa ziara ya Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa (kushoto) alipotembelea Taasisi hiyo tarehe 24 Januari 2024. Wengine katika picha ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki (wa pili kushoto) na Balozi wa Tanzania nchini Cuba. Mhe. Humphrey Polepole.
Mhe. Mesa akiwa katika meza kuu na Mhe. Kairuki na Mhe. Polepole
Mkutano ukiendelea
Mkutano ukiendelea. Kulia ni Mhe. Stephen Wasira, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere na kushoto ni Prof. Shivji
Sehemu ya wanafunzi
Wageni waalikwa wakimsikiliza Mhe. Mesa
Mkutano ukiendelea


...............ZIARA YA MHE. MESA KWA MAMA MARIA NYERERE

Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa akisalimiana na Mjane wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mama Maria Nyerere alipomtembelea kwenye makazi yake jijini Dar es Salaam kwa lengo la kumsalimia na kumjulia hali. Mhe. Mesa yupo nchini kwa ziara ya siku tatu kuanzia tarehe 23 hadi 25 Januari 2024
Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe. Makongoro Nyerere ambaye pia ni mtoto wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mama Maria Nyerere alipowatembelea kwenye makazi yao jijini Dar es Salaam kwa lengo la kumsalimia na kumjulia hali Mama Maria Nyerere. Mhe. Mesa yupo nchini kwa ziara ya siku tatu kuanzia tarehe 23 hadi 25 Januari 2024
Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Salvador Mesa akizungumza na Mjane wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mama Maria Nyerere alipomtembelea kwenye makazi yake jijini Dar es Salaam kwa lengo la kumsalimia na kumjulia hali. Mhe. Mesa yupo nchini kwa ziara ya siku tatu kuanzia tarehe 23 hadi 25 Januari 2024
Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Angellah Kairuki akiwa na Balozi wa Tanzania nchini Cuba, Mhe. Humphrey Polepole pamoja na Balozi wa Cuba nchini Tanzania, Mhe. Yordenis Vera
Mhe. Mesa akiwa katika picha ya pamja na Mama Maria Nyerer alipomtembelea nyumbani kwake jijini Dar es Salaam
Mhe. Makongoro akiwa na Wanafamilia wengine wa Hayati Mwalimu Julius Nyerere wakati wa ziara ya Makamu wa Rais wa Cuba, Mhe. Mesa alipowatembelea
Mhe. Makongoro akizungumza 
Picha ya pamoja kati Mhe. Mesa, Mama Maria Nyerere na wanafamilia wa Hayati Mwalimu Julius Nyerere






 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.