Tuesday, January 23, 2024

TANZANIA YANADI SEKTA YA UCHUMI WA BULUU KWA CHINA

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa amewaalika wafanyabiashara na wawekezaji kutoka China kuwekeza katika Sekta ya Uchumi wa Buluu na sekta nyingine za kimkakati.

Waziri Mkuu ametoa mwaliko huo alipokutana kwa mazungumzo na Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong ofisini kwake Jijini Dar es Salaam.

Mhe. Majaliwa amesema kuwa Tanzania ina rasilimali za kutosha ambazo wawekezaji kutoka China wanaweza kuja kuwekeza kwa manufaa ya pande zote mbili kiuchumi hususan katika sekta ya uchumi wa buluu. 

“Kupitia uhusiano uliopo  nchi hizo mbili, Tanzania imedhamiria kuongeza thamani ya mazao ya biashara ili kuiwezeesha kuhimili ushindani katika soko la kikanda na kimataifa,” Alisema Mhe. Majaliwa

Wakati huohuo, Mhe. Majaliwa ameishukuru China kwa kuiondolea Tanzania ushuru katika mazao ya kilimo ambayo ni maharage ya soya, mihogo, parachichi na pia ameiomba China kuangalia uwekezano wa kuongeza mazao mengine ya biashara katika utaratibu huo mfano asali, mahindi ya njano na Maharage mabichi (Green Beans).

Kwa upande wake, Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong amesema Tanzania ni rafiki wa China kwa miaka takribani 60 hivyo, China itaendelea kuwekeza zaidi Tanzania katika sekta mbalimbali za kimkakati.

“China itaendelea kushirikiana na Tanzania kuhakikisha kuwa mazao ya biashara yanaingia katika masoko yake,” alisema Guozhong.

Kuhusu uchumi wa buluu, kiongozi huyo ameahidi kuwa atawaeleza wafanyabiashara na wawekezaji kutoka China juu ya fursa zinazopatikana katika ukanda wa pwani na furza za kuwekeza kwenye sekta ya uchumi wa buluu.

Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko,Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (Mb.), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.), Naibu Waziri wa Kilimo, David Silinde (Mb) pamoja na viongozi waandamizi wa Serikali kutoka Tanzania na China.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipokutana kwa mazungumzo na Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong ofisini kwake Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko



Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong akifuatilia mazungumzo ya kikao baina yake na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa akifuatilia mazungumzo ya kikao chake na Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong. Kulia ni Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk 

Mazungumzo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa na Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong yakiendelea 

Mazungumzo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong 


Mazungumzo ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa na Naibu Waziri Mkuu wa China, Mhe. Liu Guozhong, Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Dotto Biteko (Mb.) katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali waandamizi wa Serikali 


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.