Sunday, August 28, 2016

Tanzania kushirikiana na Japan katika mafunzo kwa Wahandisi wa Gesi


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiwa kwenye Kongamano la Biashara kati ya Afrika na Japan lililofanyika Nairobi, Kenya wakati wa Mkutano wa TICAD VI. Kongamano hilo pia lilifuatiwa na hafla ya baadhi ya nchi za Afrika ikiwemo Tanzania kuingia makubaliano na Makampuni na Mashirika ya Japan katika kuimarisha biashara na uwekezaji. Mhe. Majaliwa alimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Mkutano wa TICAD VI uliofanyika tarehe 27 na 28 Agosti, 2016.
Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta ambaye ni mwenyeji na Mwenyekiti Mwenza wa Mkutano wa TICAD VI akizungumza wakati wa Kongamano la Biashara kati ya Afrika na Japan. Kushoto ni Waziri Mkuu wa Japan, Mhe. Shinzo Abe na kulia ni Naibu Rais wa Kenya, Mhe. William Ruto
Waziri Mkuu wa Japan, Mhe. Shinzo Abe nae akizungumza kwenye Kongamano hilo
Baadhi ya Marais, Mawaziri Wakuu na Makamu wa Rais wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya Kongamano la Biashara la Afrika na Japan. Kushoto ni Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Viongozi akiwemo Mhe. Majaliwa wakiwa katika picha ya pamoja na ujumbe wa Tanzania na Mjumbe kutoka Chiyoda kuashiria Makubaliano kati ya Tanzania na Shirika la Chiyoda ambalo litashirikiana na Tanzania katika kutoa mafunzo kwa Wahandisi kwenye masuala ya gesi na mafuta. Waliosimama kutoka kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Prof. James Mdoe; Bw. Francis Mossongo, Afisa Mwandamizi wa Dawati la Japan, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mkurugenzi wa Shirika la Chiyoda.
============================================

Tanzania kushirikiana na Japan katika mafunzo kwa Wahandisi

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ameshiriki hafla iliyoashiria kusainiwa kwa makubaliano kati ya baadhi ya nchi za Afrika na Makampuni mbalimbali ya Japan iliyofanyika wakati wa Mkutano TICAD VI jijini Nairobi.

Hafla hiyo ambayo ilitanguliwa na Kongamano la Biashara kati ya Afrika na Japan ilihusisha nchi 20 za Afrika ambazo zimeingia makubaliano ya kuimarisha uwekezaji na biashara na Makampuni makubwa 22 ya Japan.

Kwa upande wa Tanzania, Serikali imeingia Makubaliano na Shirika la CHIYODA kwa ajili ya kuwajengea uwezo Wahandisi wa Tanzania kwa kuwapitia mafunzo kwenye masuala ya teknolojia ya gesi na mafuta.

Akizungumza wakati wa Kongamano hilo Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta alisema kuwa Kongamano hilo ni jukwaa muafaka wakati Afrika ikiwa katika jitihada za mageuzi ya kiuchumi. Hivyo aliziomba nchi za Afrika kutumia ujuzi na uzoefu mkubwa wa Japan katika kuiimarisha Sekta Binafsi ambayo kwa kiasi kikubwa inachangia maendeleo.

Aidha, aliongeza kuwa Kenya ikiwa nchi mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki itaendelea kushirikiana na nchi wanachama wenzake kuhakikisha kunakuwepo mazingira mazuri ya kuvutia wawekezaji kutoka nje hususan Japan. Pia aliishukuru Serikali ya Japan kwa ushirikiano mkubwa inaotoa kwa Afrika na kukaribisha uwekazaji kutoka sekta binafsi ya Japan kwenye maeneo ya uzalishaji wa nishati ya umeme na maeneo mengine.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu wa Japan, Mhe. Shinzo Abe alisema kuwa Japan itaendelea kushirkiana na Afrika katika kuhakikisha inapiga hatua zaidi ya maendeleo. Aliongeza kuwa kwa kutambua umuhimu wa ushirikiano kati ya Afrika  na Japan Kampuni 22 na Vyuo Vikuu vya Japan zimefuatana nae ili kukamilisha mikataba 73 na nchi za Afrika. 

Aidha,  alieleza kuwa Kampuni za Japan zimetumia fursa ya Mkutano wa TICAD  VI kutangaza Azimio la Biashara ikiwa ni katika kuelezea nia na madhumuni yao katika kuchangia maendeleo ya Afrika.

Mbali na Tanzania nchi zingine za Afrika zilizoingia Makubaliano na Kampuni na Mashrika kutoka Japan ni pamoja na Kenya, Angola, Cameroon, Congo, Cote d’ Ivoire, DRC, Ethiopia, Misri, Ghana, Madagascar, Morocco, Msumbiji, Namibia, Nigeria, Rwanda, Seychelles, Afrika Kusini, Uganda na Zambia.

Wakati huohuo, Mkutano wa Sita wa Kilele wa Kimataifa kuhusu Ushirikiano wa Maendeleo kati ya Japan na Afrika (Tokyo International Conference on African Development-TICAD VI) umemalizika   Jijini Nairobi leo huku Wakuu wa Nchi na Serikali wakipitisha kwa kauli moja Azimio la Nairobi na Mpango Kazi  wa utekelezaji wake.

Azimio la Nairobi pamoja na mambo mengine linalenga katika kutekeleza mambo makuu matatu  ambayo ni: Kufanya mabadiliko ya mifumo ya uchumi ili kuwa na vyanzo mbadala vya kuendesha uchumi huku mkazo ukiwekwa kwenye uanzishwaji wa viwanda vitakavyozalisha ajira kwa wingi kwa vijana wa Afria; Kujenga mifumo ya Huduma za Afya ambazo ni endelevu kwa maisha bora ikiwemo kuboresha huduma za afya, kuweka mikakati ya kukabiliana na magonjwa kama Ebola, kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto na jamii nzima; na Kukuza na kuimarisha Utulivu na Ustawi wa Jamii.

Mbali na Mkutano wa Kilele wa TICAD VI, shughuli zingine zilizoenda sambamba na mkutano huo ni Kongamano la Biashara kati ya Afrika na Japan; Maonesho ya Biashara ya Afrika na Japan; na Mkutano wa Majadilino ya Kibiashara kati ya Viongozi Wakuu wa Serikali na Wakurugenzi Wakuu wa Makampuni Binafsi.

Mkutano wa TICAD VI ambao ulihudhuriwa na Wakuu wa Nchi na Serikali zaidi ya 30 kutoka Afrika, Wakuu wa Mashirika ya Kimataifa na Kikanda pia uliyashirikisha Makampuni zaidi ya 100 kutoka Serikali ya Japan, Sekta Binafsi na kuhudhuriwa na zaidi ya Wajumbe 10,000 kutoka sehemu mbalimbali duniani.

-Mwisho-



Waziri Mkuu akutana na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Sudan Jijini Nairobi

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akimsikiliza Makamu wa Kwanza wa Rais wa Sudan, Mhe. Luteni Jenerali Barki Hassan Salih walipokutana Jijini na Nairobi wakati wa Mkutano wa TICAD VI kwa mazungumzo ya ushirikiano baina ya nchi hizo mbili.
Mhe. Majaliwa akiwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba(kushoto) na Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Bi. Talha Waziri (wa pili kulia) na Bi. Irene Bwire, Mwandishi wa Waziri Mkuu wakifuatilia mazungumzo  kati yake na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Sudan, Mhe. Lt. Gen. Salih na ujumbe wake hawapo pichani)
Mhe. Salih (wa tatu kushoto) akiwa na ujmbe aliofuatana nao wakati wa mazungumzo yake na Mhe. Majaliwa (hayupo pichani)



Saturday, August 27, 2016

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje akutana na Naibu Waziri wa Marekani masuala ya Afrika

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba akisalimiana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani anayeshughulikia masuala ya Afrika, Mhe. Linda Thomas-Greenfield walipokutana wakati wa Mkutano wa TICAD VI Jijini Nairobi na kuzugumzia masuala ya ushirikiano. Wakati wa mazungumzo hayo Mhe. Dkt. Kolimba alimshukuru Mhe. Greenfield kwa ushiriano uliopo kati ya Tanzania na Marekani ambapo nchi hiyo imekuwa ikishirikiana na Tanzania katika kuboresha huduma za afya na miradi mingine ya maendeleo.
Mhe. Naibu Waziri akizungumza na Mhe. Greenfield 
Mazungumzo yakiendelea kati ya Mhe. Dkt. Susan na Mhe. Greenfield (hayupo pichani). Wengine katika picha ni Bi. Talha Waziri (kushoto), Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Kenya na Bi. Bertha Makilagi (kulia), Afisa Mambo ya Nje.
Mhe. Greenfield akiwa na ujumbe wake nae akichangia jambo wakati wa mazungumzo yake na Mhe. Dkt. Susan (hayupo pichani)
Mhe. Dkt. Susan aiagana na mgeni wake Mhe. Greenfield  mara baada ya mazungumzo huku Bi. Makilagi (katikati) akishuhudia
Mhe. Naibu Waziri (mwenye gauni la bluu) akiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Bi Talha Waziri (wa pili kutoka kulia), Bw. Adam Isara, Msaidizi wa Naibu Waziri na Bi. Bertha Makilagi (kushoto), Afisa Mambo ya Nje.

Banda la Maonesho la Tanzania lang'ara kwenye mkutano wa TICAD VI

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba akipokelewa  na Kaimu Mkurugenzi wa TanTrade, Bw. Edwin Rutageruka mara baada ya kuwasili kwenye Banda la Maonesho la Tanzania yanayofanyika wakati wa Mkutano wa TICAD VI Jijini, Nairobi. Makampuni na Taasisi mbalimbali kutoka nchi za Afrika ikiwemo Tanzania na Japan yanashiriki maonesho hayo yanayolenga kuvutia wawekezaji na wafanyabishara.
Mhe. Naibu Waziri akipata maelezo kuhusu bidhaa mbalimbali zinazozalishwa Tanzania zilizokuwepo kwenye Banda hilo. Bidhaa hizo ni pamoja na Kahawa, Majani ya Chai na Viungo vya chakula
Banda la Tanzania kama linavyoonekana
Mhe. Waziri akipata maelezo ya namna watu wa makampuni mbalimbali walivyovutiwa na kahawa ya Tanzania
Mhe. Naibu Waziri akikaribishwa na Bi. Latifa Kigoda, Afisa Mwandamizi kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) alipotembelea banda la Tanzania
Mhe. Naibu Waziri akisaini kitabu cha wageni bandani hapo
Mhe. Naibu Waziri akisikiliza maelezo kutoka kwa Bi. Kigoda kuhusu namna TIC ilivyojipanga kutangaza fursa za uwekezaji kwa wawekezaji mbalimbali wanaohudhuria mkutano wa TICAD VI
Bi. Kigoda akimpatia Jarida Maalum lililoandaliwa na TIC kwa ajili ya kuvutia wawekezaji waliohudhuria mkutano wa TICAD VI
Bi. Kigoda akimpatia maelezo Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Kenya, Bi. Talha Waziri ambaye alikuwa amefuatana na Mhe. Naibu Waziri.
Mmoja wa wageni aliyetembelea bandani hapo akipata maelezo ya fursa za uwekezaji zilizopo nchini kutoka kwa Bi. Kigoda
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe.Dkt.  Susan Kolimba akipata maelezo kutoka kwa Bw. Lameck Borega, Meneja wa Uwekezaji wa EPZA.
Mhe. Dkt. Kolimba akimpatia ushauri wa namna ya kuwashawishi wawekezaji kuja nchini kuwekeza kupitia EPZA
Mhe. Naibu Waziri akiwa amewasili kwenye Banda la Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) na kupatiwa maelezo na Bi. Alistidia Karaze, Afisa Utafiti Mkuu kwenye Bodi hiyo
Mhe. Naibu Waziri akimpatia ushauri Bi. Karaze wa namna ya kuboresha huduma za utalii nchini ikiwemo maonesho ili kuvutia watalii wengi zaidi kutembelea nchini.

Friday, August 26, 2016

Mkutano wa Mawaziri wa TICAD wafanyika Jijini Nairobi

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba akiongoza ujumbe wa Tanzania kwenye kikao cha Mawaziri wa Mkutano wa Sita wa Kimataifa kuhusu Ushirikiano wa Maendeleo kati ya Japan na Afrika (Tokyo International Conference on African Development-TICAD VI)  uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Kenyatta (KICC) tarehe 26 Agosti, 2016. Kulia ni Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Khalid Salum Mohammed na kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbelwa Kairuki.
Balozi Mbelwa akitoa ufafanuzi kwa Mhe. Naibu Waziri kuhusu masuala yatakayojadiliwa kwenye Mkutano huo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Amina Mohammed akizungumza wakati wa Mkutano huo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan, Mhe. Fumio Kishida nae akizungumza wakati wa mkutano wa Mawaziri
Sehemu ya Wajumbe waliohudhuria mkutano huo
Sehemu nyingine ya wajumbe
Picha ya pamoja ya meza kuu.
=======================================

 MKUTANO WA MAWAZIRI WA TICAD WAFANYIKA JIJINI NAIROBI

Kikao cha Mawaziri kuandaa Mkutano wa Kilele wa Sita wa Kimataifa kuhusu Ushirikiano wa Maendeleo kati ya Japan na Afrika (Tokyo International Conference on African Development-TICAD VI) kimemalizika   Jijini Nairobi leo ambapo Mawaziri hao wameikubali kwa kauli moja Rasimu ya Azimio la Nairobi na Mpango Kazi  wake tayari kwa  kuwasilishwa kwa Wakuu wa Nchi na Serikali kwa ajili ya kupitishwa.

Akihitimisha Mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Mhe. Amina Mohammed amewashukuru Mawaziri wenzake, waandaaji wa kikao hicho na washiriki wote kwa kikao chenye mafanikio na kueleza kuwa ana matumaini makubwa kuwa agenda zilizojadiliwa zitapitishwa na Wakuu wa Nchi na Serikali kwenye Mkutano wao.

Aidha, alisema kuwa Rasimu hiyo ya Azimio ambalo linazungumzia agenda muhimu tatu ambazo ni Kuhamasisha mageuzi ya kiuchumi kupitia uendelezaji wa viwanda; Kuboresha sekta ya Afya kwa maisha bora na Kusaidia jitihada za kudumisha amani na utulivu katika jamii linalenga kutatua changamoto mbalimbali na kuiwezesha Afrika kufikia maendeleo endelevu.

Pia, aliishukuru Serikali ya Japan kwa kuendelea kuiunga mkono Afrika katika kukamilisha malengo yake ya maendeleo na kwamba mkutano huu wa 6 utaendelea kuimarisha na kudumisha ushirikiano uliopo kati ya nchi za Afrika na Japan.

“Mkutano huu una lengo kubwa moja la kuiwezesha Afrika kufikia maendeleo endelevu kwa kushirikiana na Japan. Hivyo nawapongeza waandaaji na washiriki wote kwa kufanikisha rasimu ya Azimio la Nairobi na ni imani yangu kuwa Azimio hili litapitishwa na Wakuu wa Nchi na Serikali katika mkutano wao” alisema Mhe. Mohammed.

Awali akizungumza wakati wa mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan, Mhe. Fumio Kishida alisema kuwa Afrika imeendelea kuwa mdau muhimu katika ushirikiano na Japan na kwamba nchi yake inaona fahari kuendeleza ushirikian huo ili kuziwezesha nchi za Afrika kufikia maendeleo endelevu. Pia aliishukuru Serikali ya Kenya kwa kuwa mwenyeji wa mkutano wa TICAD VI na ana matarajio makubwa kuwa utakuwa na tija.

Pia aliongeza kuwa Mikutano ya TICAD ni jukwaa muhimu linaloziwezesha nchi za Afrika na Japan kuangalia vipaumbele mbalimbali katika ushirikiano ili hatimaye kufikia malengo yaliyokusudiwa ikiwemo kuinua uchumi na kuboresha sekta mbalimbali ikiwemo afya.

Naye Waziri wa Uchumi na Mipango wa Chad, Mhe. Mariam Mahamat Nour ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa Umoja wa Afrika alisema kuwa mkutano wa 6 wa TICAD utatoa mwanga kwa changamoto mbalimbali zinazolikabili Bara la Afrika kupitia Azimio la Nairobi mara litakapotishwa na kuanza kutekelezwa.

Kwa upande wa Tanzania Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika, Mhe. Dkt. Susan Kolimba aliongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano huo wa Mawaziri. Wajumbe wengine waliohudhuria ni Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dkt. Khalid Salum Mohammed na Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia, Balozi Mbelwa Kairuki.

Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali unatarajiwa kufanyika tarehe 27 na 28 Agosti, 2016 ambapo moja ya agenda ni kupitisha Azimio la Nairobi. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa atamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. John Pombe Magufuli kwenye mkutano huo.

Mkutano wa Sita wa TICAD unalenga kuiwezesha Afrika katika sekta ya uchumi na uwekezaji ambapo utawashirikisha pia wadau kutoka sekta binafsi zikiwemo Kampuni binafsi zaidi ya 300 kutoka Japan ili kufikia lengo hilo.

-Mwisho-





Naibu Waziri akutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa China

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba  akisalimiana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. Zhang Ming walipokutana Nairobi  kwa mazungumzo ya kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na China.  Mhe. Dkt. Kolimba pamoja na Mhe. Zhang wapo mjini humo kwa ajili ya kuhudhuria Mkutano wa TICAD VI utakaofanyika tarehe 27 na 28 Agosti, 2016.
Mhe. Kolimba akimweleza jambo Mhe. Zhang wakati wa mazungumzo yao.
Mhe. Zhang na ujumbe wake wakati wa mkutano na Mhe. Dkt. Kolimba (hayupo pichani)
Mhe. Dkt. Susan Kolimba akiwa na Waziri wa Fedha na Uchumi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Khalid Salum Mohammed (kulia) pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbelwa Kairuki (wa pili kutoka kushoto) na Bw. Adam Isara, Msaidizi wa Naibu Waziri.
Mhe. Naibu Waziri na Mhe. Waziri Mohammed pamoja na wajumbe wengine wakimsikiliza Mhe. Zhang ambaye hayupo pichani. Kulia ni Bi. Bertha Makilagi, Afisa Mambo ya Nje. 








Naibu Waziri akutana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa China

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba  akisalimiana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa China, Mhe. Zhang Ming walipokutana Nairobi  kwa mazungumzo ya kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na China.  Mhe. Dkt. Kolimba pamoja na Mhe. Zhang wapo mjini humo kwa ajili ya kuhudhuria Mkutano wa TICAD VI utakaofanyika tarehe 27 na 28 Agosti, 2016.
Mhe. Kolimba akimweleza jambo Mhe. Zhang wakati wa mazungumzo yao.
Mhe. Zhang na ujumbe wake wakati wa mkutano na Mhe. Dkt. Kolimba (hayupo pichani)
Mhe. Dkt. Susan Kolimba akiwa na Waziri wa Fedha na Uchumi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Khalid Salum Mohammed (kulia) pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbelwa Kairuki (wa pili kutoka kushoto) na Bw. Adam Isara, Msaidizi wa Naibu Waziri.
Mhe. Naibu Waziri na Mhe. Waziri Mohammed pamoja na wajumbe wengine wakimsikiliza Mhe. Zhang ambaye hayupo pichani. Kulia ni Bi. Bertha Makilagi, Afisa Mambo ya Nje. 








Thursday, August 25, 2016

Mkutano wa TICAD kufanyika Afrika kwa mara ya kwanza

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Kenya, Balozi Monica Juma (mwenye nguo ya kijani) akifuatiwa na Bw. Takeshi Osuga, Balozi wa TICAD kutoka Japan na  Mhe. Cherif Mhamat Zene, Balozi wa Chad, Ethiopia wakiongoza moja ya vika vya Maafisa Waandamizi ikiwa ni maandalizi ya Mkutano wa Sita wa TICAD.
=====================================================================================

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mkutano wa  6 wa Kimataifa kuhusu Ushirikiano wa Maendeleo kati ya Japan na Afrika (Tokyo International Conference on African Development-TICAD VI) unatarajiwa kufanyika tarehe 27 na 28 Agosti, 2016 Jijini Nairobi, Kenya. Hii ni mara ya kwanza kwa mkutano huu kufanyika nje ya Japan tangu kuanzishwa kwake mwaka 1993.

Mkutano huu wa Sita ambao umetanguliwa na kikao cha Maafisa Waandamizi wakiwemo Makatibu Wakuu na Mabalozi tarehe 24 na 25 Agosti, 2016 utafuatiwa na kikao cha Mawaziri tarehe 26 Agosti, 2016 unatarajiwa kupitisha Azimio la Nairobi ambalo litajikita katika kushughulikia changamoto mbalimbali zinazolikabili Bara la Afrika katika kufikia maendeleo na ustawi.

Changamoto hizo ni pamoja na kuporomoka kwa bei za bidhaa zinazotegemewa na nchi za Afrika katika ustawi wake kama vile mafuta, gesi na madini na hivyo kupelekea kuathirika kwa ukuaji wauchumi katika nchi nyingi za Afrika; kulipuka kwa magojwa kama Ebola na kusababisha vifo vilivyopelekea kusitishwa kwa shughuli za kiuchumi na kupotea kwa nguvu kazi; na Kuongezeka kwa vitendo vya ugaidi.

Agenda nyingine zitakazojadiliwa ni pamoja na: Kuhamasisha mageuzi ya kiuchumi kupitia uendelezaji wa viwanda; Kuboresha sekta ya Afya kwa maisha bora na Kusaidia jitihada za kudumisha amani na utulivu katika jamii.

Vile vile Mkutano huu umetoa kipaumbele kwa ushiriki wa sekta binafsi hususan wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa kutoka Japan na Afrika. Hivyo mkutano utatoa fursa kwa taasisi zenye dhamana ya kuvutia uwekezaji, biashara na utalii nchini kutangaza fursa zilizopo kwa kampuni za Japan.

Mkutano huu wa 6 wa TICAD ambao unashirikiana kwa karibu na Kamisheni ya Umoja wa Afrika unalenga kuiwezesha Afrika kujitegemea katika kukua na kufikia maendeleo yaliyokusudiwa ikiwemo utekelezaji wa Agenda 2063 ambayo viongozi wa Afrika walikubaliana wakati wakuadhimisha miaka 50  ya Umoja wa Afrika. Agenda 2063  inalenga kuliunganisha Bara la Afrika katika masuala ya kukuza uchumi; kuhamasisha utawala bora na utawala wa sheria; kuhakikisha maendeleo kwa mtu mmoja mmoja; kuhakikisha amani na usalama unaimarika na kuiweka Afrika kwenye nafasi ya mchangiaji mkuu wa uchumi duniani.

Mkutano wa kwanza wa TICAD uliofanyika Jijini Tokyo mwaka 1993 ulijikita zaidi katika agenda ya kuongeza misaada kwa nchi za Afrika. Kufuatia mkutano huo misaada ya Japan kwa nchi za Afrika iliongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 0.6 mwaka 1993 na kufikia Dola bilioni 0.8 mwaka 1998. Hadi kufikia mwaka 2013 msaada wa Japan (ODA) kwa nchi za Afrika ulifikia Dola za Marekani bilioni 2.8.

Mkutano wa 6 wa TICAD ambao kwa mara ya kwanza katika historia unafanyika Afrika utawezesha majadiliano ya ana kwa ana kati ya Wakuu wa Nchi na Wawakilishi kutoka Sekta binafsi.

Kadhalika, mbali na mwenyeji wa Mkutano huu ambaye ni Rais wa Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta mkutano utahudhuriwa pia na Waziri Mkuu wa Japan, Mhe. Shinzo Abe, Viongozi Wakuu kutoka nchi 54 za Afrika pamoja na wawakilishi kutoka mashirika ya kimataifa na makundi mbalimbali.

Ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huu utaongozwa na Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.

-Mwisho-

 Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali
Wizara  ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
25 Agosti, 2016





Wanadiaspora watembelea miradi ya maendeleo Zanzibar

Wanadiaspora wakipata maelezo kutoka kwa mkandarasi wa mradi wa ujenzi wa nyumba zinazojengwa na ZSSF kwaajili ya makazi katika eneo la Mbweni Zanzibar 
Sehemu ya Wanadiaspora (watanzania waishio ughaibuni) wakitizama mradi wa nyumba za kisasa unaoendelea
Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa katika picha ya pamoja na Watanzania waishio Ughaibuni (Diaspora) waliohudhuria kongamano la tatu (3) la Diaspora lililofanyika katika Hotel ya Zanzibar Beach Resort.