Thursday, April 19, 2018

Wizara ya Mambo ya Nje kutumia fursa za maadhimisho ya kitaifa katika kutekeleza Diplomasia ya Uchumi.

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan Mwinyi akizungumza katika ufunguzi wa kikao cha pamoja kati ya wafanyabiashara na kamati ya maandalizi ya wiki ya Tanzania nchini Kenya inayotarajiwa kufanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa (KICC) Jijini Nairobi, Kenya kuanzia tarehe 25 hadi 28 Aprili 2018 ambapo kilele cha wiki hiyo ni tarehe 26 April 2018 siku ya maadhimisho ya miaka 54 ya Muungano wa Tanzania.

Balozi Mwinyi alitumia fursa hiyo kuwaaga wafanyabiashara na wajumbe wa kamati wanaoenda nchini Kenya kuratibu wiki hiyo  ambapo alisisitiza umuhimu wa kutumia fursa hiyo muhimu katika kuliletea taifa maendeleo kwakua kukua kwa biashara nchini kutaleta ajira, kutakuza pato la taifa na mabadiliko katika ustawi wa maisha ya wananchi kwa ujumla.

Balozi Mwinyi akiwa na viongozi wa kamati ya maandalizi ya wiki ya Tanzania nchini Kenya, wa pili kushoto ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (TANTRADE) ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati, Bw. Edwin Rutageruka, wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni katibu wa kamati, Balozi Anisa Mbega, wa kwanza kulia  ni mwakilishi kutoka Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) ambaye pia ni mwenyekiti mwenza wa kamati hiyo, Bi. Lilian Ndosi na wa kwanza kushoto ni Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mashariki ya kati ambaye pia ni katibu msaidizi wa kamati, Bw. Suleiman Saleh. 

Sehemu ya wafanyabiashara waliothibitisha ushiriki katika maonesho ya bidhaa za Tanzania nchini Kenya wakifuatilia taarifa mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa na viongozi wa kamati.

Sehemu nyingine ya wajumbe wa kamati, wadhamini na wafanyabiashara watakaoshiriki katika maonesho  hayo wakifuatilia kikao.

Wajumbe wakifuatilia kikao.

Picha ya pamoja meza kuu na wajumbe wa kamati ya maandalizi ya wiki ya Tanzania nchini Kenya.

Picha ya pamoja meza kuu, wadhamini na wafanyabiashara watakaoshiriki katika wiki ya Tanzania nchini Kenya.

 

Wednesday, April 18, 2018

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU FURSA ZA MAFUNZO



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

FURSA ZA UFADHILI WA MASOMO

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imepokea fursa za mafunzo ya muda mrefu kutoka Kamisheni ya Umoja wa Afrika yatakayofanyika katika Chuo Kikuu cha Pan African (PAU).

Mafunzo hayo ambayo yapo kwa ngazi ya Shahada ya Uzamili na Shahada ya Uzamivu yatatolewa katika kozi mbalimbali zikiwemo Baiolojia, Hesabu, Uhandisi, Sayansi ya Afya, Usimamizi wa Mazingira, Sayansi ya Michezo, Mifugo, Uongozi na Mtangamano, Lugha, Ukalimani wa Mikutano na Ufasiri, Uhandisi wa Maji na Nishati.  

Kwa waombaji wa Shahada ya Uzamili wanatakiwa kuwa na  miaka isiyozidi  30 kwa waombaji  wanaume na miaka isiyozidi 35 kwa waombaji wanawake. Aidha, kwa waombaji wa Shahada ya Uzamivu wasiwe na miaka zaidi ya 35 kwa waombaji wanaume na miaka isiyozidi 40 kwa waombaji wanawake.

Maombi ya mafunzo haya yanatakiwa kufanyika kwa njia ya mtandao (online) kupitia anuani ya barua pepe ya pau-au.net. Mwisho wa kutuma maombi ya fursa hizi ni tarehe 20 Aprili, 2018. Maelezo ya ziada kuhusu mafunzo haya yanapatikana kupitia pau.scholarships@africa-union.org au www.pau-au.net. Mratibu wa Mafunzo haya ni Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje Na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam
18Aprili, 2018

Monday, April 16, 2018

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje akutana kwa mazungumzo na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Brazil

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Susan Kolimba (katikati) akizungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Brazil, Mhe. Balozi Fernando Jose Marroni de Abreu (hayupo pichani) walipokutana kwa Majadiliano ya Kisiasa yaliyofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam tarehe 16 Aprili, 2018. Majadiliano hayo yalifanyika wakati wa ziara ya kikazi ya siku mbili ya Mhe. Balozi Fernando hapa nchini. Pamoja na mambo mengine walijadiliana kuhusu namna ya kuboresha mashirikiano ya kidiplomasia baina ya nchi hizi mbili hususan katika eneo la biashara na uwekezaji. Pia Naibu Mawaziri hao walijadili namna ya kutekeleza kikamilifu Mradi wa Pamba kwenye eneo la Ziwa Victoria na matokeo ya kusainiwa kwa mkataba wa msamaha wa deni la Tanzania kwa Brazil pia lilijadiliwa. Aidha,  Brazil wameahidi kushirikiana na Tanzania kwenye sekta ya afya hususan katika kupambana na maradhi ya Selimundu (Sircle-cell) na kwa upande wa Zanzibar watashirikiana katika afya ya mama na mtoto hususan kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na watoto wachanga.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Brazil, Mhe. Balozi Fernando Jose Marroni de Abreu (katikati) nae akizungumza wakati wa majadiliano ya kisiasa kati yake na  Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Mhe. Dkt. Susan Kolimba (hayupo pichani). Wengine kwenye picha ni Balozi wa Brazil nchini, Mhe. Carlos Alfonso Iglesias Puente (kushoto) na Mkuu wa Idara inayoshughulikia masuala ya Kaskazini na Mashariki mwa Afrika kwenye Wizara ya Mambo ya Nje ya Brazil, Bw. Paulo Cypriano.
Mhe. Dkt. Susan Kolimba akimsikiliza kwa makini Mhe. Fernando de Abreu (hayupo pichani), Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Brazil wakati wa Majadiliano ya Kisiasa kati ya Tanzania na Brazil. Kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Brazil, Mhe. Dkt. Emmanuel Nchimbi na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Salvator Mbilinyi (kulia)
Mhe. Dkt. Kolimba na Ujumbe wake wakifuatilia mazungumzo hayo
Mhe. Fernando de Abreu na Ujumbe wake wakifuatilia mazungumzo
Mhe. Dtk. Kolimba kwa pamoja na Mhe. Balozi Fernando wakishuhudia uwekwaji saini wa Hati ya Makubaliano kuhusu kuanzishwa kwa Ushirikiano wa Kisiasa kati ya Tanzania na Brazil uliokuwa ukisainiwa na Balozi wa Tanzania nchini Brazil, Mhe. Dkt. Emmanuel Nchimbi na Balozi wa Brazil nchini, Mhe. Carlos Alfonso Iglesias Puente.
Hati ikisainiwa. Pembeni ya Balozi Nchimbi ni Bw. Mustafa M. Ussi, Afisa Mambo ya Nje kutoka Kitengo cha Sheria
Mhe. Balozi Nchimbi na Mhe. Balozi Puente wakibadilishana Hati hiyo mara baada ya kusaini huku Naibu Mawaziri wakishuhudia
Mhe. Dkt. Susan akiwa na Mhe. Balozi Fernando mara baada ya kukamilisha majadiliano
Mhe. Dkt. Kolimba (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Balozi Fernando (wa nne kushoto). Wengine katika picha ni Balozi wa Tanzania nchini Brazil, mhe. Emmanuel Nchimbi (wa pili kulia), Balozi wa Brazil nchini, Mhe. Carlos Iglesias Puente (wa tatu kushoto), Mkurugenzi wa Kanda ya Ziwa wa Taasisi ya  Utafiti wa Maendeleo ya  Kilimo, Dkt. Everina Lukonge (wa pili kushoto), Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Bw. Salvator Mbilinyi (kulia) na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Jestas Nyamanga
Picha ya pamoja kati ya Naibu Mawaziri na wajumbe wote wa Tanzania  na Brazil

Friday, April 13, 2018

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


ZIARA YA NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE WA BRAZIL NCHINI 14 – 17, APRILI, 2018

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Brazil, Mhe. Balozi Fernando Jose Marroni de Abreu anatarajia kufanya ziara hapa nchini kuanzia tarehe 14 hadi 17 Aprili, 2018.
Katika ziara hiyo, pamoja na mambo mengine, atafanya mazungumzo na mwenyeji wake Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt Susan Alphonce Kolimba tarehe 16 Aprili, 2018. Viongozi hawa watajadiliana namna ya kuboresha mahusiano na mashirikiano ya kidiplomasia baina ya Tanzania na Brazil, hususan katika eneo la uwekezaji na biashara.

Mhe. Dkt. Kolimba na Mhe. Balozi Fernando Jose Marroni de Abreu wanatarajiwa kushiriki kwenye majadiliano ya kisiasa, mambo makubwa yatakayojadiliwa ni; Ushirikiano wa kiuchumi na biashara ikiwemo, matokeo ya kusainiwa kwa mkataba wa msamaha wa deni la Tanzania kwa Brazil, pamoja na masuala mengine yenye maslahi kwa wote kiuchumi na kibiashara, taathmini ya utekelezaji wa Mradi wa Pamba Ziwa Victoria ‘Cotton Victoria Project’ na kuimarisha ushirikiano katika sekta ya mifugo nchini hususan kusaidia jitihada za Serikali za kuboresha ufugaji wa ng’ombe aina ya zebu.

Aidha, katika majadiliano hayo pia watazungumzia  kuhusu Masuala ya kimataifa hususan mageuzi ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, na Masuala ya Kikanda hasa Migogoro ya kisiasa nchini Sudan ya Kusini na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Burundi.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam
 13 Aprili, 2018



Naibu Waziri akutana na kufanya mazungumzo na Spika EALA

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Susan Kolimba na Spika wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Mhe. Martin Ngoga wakisalimiana walipokutana kwa mazumgumzo katika Ofisi za Wizara Dodoma.

Mhe. Ngoga alimtembelea Naibu Waziri Mhe. Dkt. Kolimba Ofisini kwake ambapo walifanya mazungumzo kuhusu masuala mbalimbali ya Jumuiya. Mhe. Dkt.Kolimba katika mazungumzo hayo amemwahidi Spika wa EALA kuwa Wizara na Serikali kwa ujumla itatoa ushirikiano wa hali ya juu kwa Bunge hilo katika utelezaji wa majukumu yake.

Aidha kwa upande wake Spika wa EALA amesema kuwa,kwa sasa wamejipanga vizuri katika kuhakikisha wanadumisha ushirikiano na Mabunge ya Nchi wanachama na kutoa mrejesho kwa Nchi wanachama kuhusu masuala mbalimbali ya yanayojili katika Bunge hilo.

Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki linafanya vikao vyake mjini Dodoma kuanzia tarehe 9 hadi 28 Aprili, 2018 

Spika wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Mhe. Martin Ngoga akisaini kitabu cha wageni mara baada kuwasili Wizarani Dodoma. 
Naibu Waziri Mhe. Dkt. Kolimba na Spika wa EALA Mhe. Dkt.Ngoga wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wabunge wa EALA na Maafisa kutoka Wizarani na Bunge la EALA 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Wafanyabiashara nchini kutafutiwa Soko Ufaransa

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kupitia Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), inaratibu ziara ya viongozi wa makampuni ya biashara zaidi ya 30 kutoka Ufaransa ambao ni wanachama wa Taasisi ya Sekta Binafsi ya Ufaransa (MEDEF) yenye mtandao wa makampuni zaidi ya 7100..

Ziara hiyo itakayofanyika kuanzia tarehe 15 – 18 Aprili 2018, inalenga kukuza ushirikiano wa biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Ufaransa; kutangaza fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo nchini Tanzania; kushawishi makampuni makubwa ya Ufaransa kuwekeza Tanzania katika sekta mbalimbali zikiwemo nishati, miundombinu, viwanda, maji n.k na kutoa fursa kwa wafanyabiashara kutoka Tanzania na Ufaransa kubadilishana  uzoefu na kuanzisha ushirikiano baina yao.

Ukiwa nchini, ujumbe huo utapata fursa ya kufanya mazungumzo na viongozi wakuu wa serikali na kushiriki katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji baina ya Tanzania na Ufaransa litakalofanyika tarehe 18 Aprili 2018, jijini Dar es Salaam.

Aidha, baada ya kongamano hilo, Wizara kupitia Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) itafanya mkutano na wafanyabiashara Wakitanzania wenye nia ya kutafuta masoko nchini Ufaransa, tarehe 20 Aprili 2018. Ubalozi utaelezea fursa zilizopo nchini Ufaransa na mikakati ya kufanya bidhaa za Tanzania hususan za kilimo ziweze kuuzwa nchini humo.

Wizara inatoa wito kwa Wafanyabishara wa Tanzania kushiriki kikamilifu na kuchangamkia fursa hii muhimu.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam
 13 Aprili, 2018

Balozi Adadi Ashiriki Mkutano wa Usalama barabarani jijini New York


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, Mhe. Balozi Adadi Rajab (Mb) akiwa katika mkutano wa kimataifa kuhusu kuimarisha usalama barabarani duniani unaofanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani. Kushoto ni Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Modest Mero. Mkutano huo ni kwa ajili ya kupitia Azimio la pamoja la kuimarisha usalama barabarani duniani ili kupunguza vifo na ulemavu unaosababishwa na ajali za barabarani. kwa nuhjibu wa ripoti iliyotolewa na WHO inakadiriwa watu milioni 1.3 wanakufa kila mwaka kwa ajali za barabarani.

Balozi Luvanda awasilisha Hati za Utambulisho kwa Rais wa Sri Lanka

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Baraka Luvanda (kushoto) ambaye anawakilisha pia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kisoshalisti ya Sri Lanka akiwasilisha Hati za Utambulisho kwa Mheshimiwa Maithripala SIRISENA, Rais wa nchi hiyo.

Balozi Luvanda akisalimiana na maafisa waandanizi wa Ikulu ya Sri Lanka 
Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Baraka Luvanda aliwasilisha Hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kisoshalisti ya Sri Lanka, Mheshimiwa Maithripala SIRISENA.

Hii ni hatua muhimu katika kuendeleza, kuimarisha na kukuza uhusiano wa kirafiki na ushirikiano mwema uliopo kati ya Tanzania na Sri Lanka ambao ulianza mnamo miaka ya tisini. Wakati huo, Sri Lanka ilikuwa inawakilishwa nchini Tanzania kupitia Ubalozi wake wa mjini Kampala, Uganda ambao baadaye ulifungwa na Tanzania ikiwakilishwa nchini Sri Lanka kupitia Ubalozi wake wa New Delhi. Kwa sasa Sri Lanka inakusudia kumteua Balozi wake mjini Nairobi ambaye pia ataiwakilisha nchi hiyo nchini Tanzania.

Katika hafla hiyo, Balozi Luvanda aliambatana na Mwambata Jeshi wa Tanzania nchini India, Col. Amri Salim MWAMI. Aidha, Balozi Luvanda alifanya mazungumzo na Mkuu wa Itifaki wa Sri Lanka pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Masuala ya Afrika, ambapo ameahidi kushirikiana kwa karibu na watendaji hao katika kudumisha uhusiano uliopo kati ya nchi hizi mbili na ambao utazinufaisha zaidi, hususan katika kuhakikisha uhaulishaji wa uzoefu, teknolojia na utaalam wa Sri Lanka kwa Tanzania kwenye sekta ya viwanda vya nguo, madini na vito mbali mbali na kilimo.

Sri Lanka ni nchi yenye uchumi unaoendelea ingawa imepitia kipindi kigumu cha vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa takriban miaka 25, vita ambavyo vilimalizika mwaka 2009.

Sekta binafsi Zanzibar yajadili mikakati madhubuti ya kufanikisha wiki ya Tanzania nchi Kenya

Waziri Wa Viwanda, Biashara na Masoko wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Balozi Amina Salum akizungumza katika ufunguzi wa mkutano na Wafanyabishara wa Zanzibar  uliofanyika katika Ofisi za Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko  tarehe 13 Aprili 2018. Kutoka kushoto ni Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Masoko wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Hassan Khamis Hafidh  na Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Katibu wa Kamati ya Taifa ya maandalizi ya maonesho ya bidhaa za Tanzania nchini Kenya, Balozi Anisa Mbega.

Katika ufunguzi huo Mhe. Waziri Amina aliwasisitiza wafanyabiashara hao kushiriki katika maonesho pamoja na umuhimu wa sekta binafsi kushirikiana na Serikali katika kutekeleza Diplomasia ya uchumi kwa vitendo.
Balozi Anisa Mbega akiwasilisha taarifa ya maandalizi ya maonyesho pamoja na kutoa ufafanuzi wa matukio mengine yatakayoambatana na maonyesho hayo kama vile kongamano la biashara, maadhimisho ya miaka 54 ya Muungano wa Tanzania.

Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Afrika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Suleiman Saleh akiwahamasisha wafanyabishara kushiriki maonesho hayo pamoja na kuhakikisha wanafanya maandalizi ili kuweza kukamilisha vigezo na masharti ya ushiriki.

Juu na chini ni sehemu ya washiriki wa mkutano huo wakifuatilia taarifa zilizokuwa zikiwasilishwa na viongozi.


Sehemu ya waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano.
Mkutano ukiendelea.


Thursday, April 12, 2018

Poland yafungua rasmi Ofisi za Ubalozi nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga kwa pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe. Prof. Jacek Czaputowicz wakikata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa Ofisi za Ubalozi wa Poland hapa nchini. Ufunguzi wa Ofisi za Ubalozi huo zilizopo Masaki, Jijini Dar es Salaam ulifanyika tarehe 12 Aprili, 2018. Ili kuimarisha na kukuza ushirikiano kati ya Tanzania na Poland, nchi hiyo ilifungua tena Ubalozi wake hapa nchini mwaka 2017 baada ya kuufunga mwaka 2008 na kabla ya uzinduzi wa ofisi hizi hapo nchi hiyo ilikuwa inawakilishwa kutokea Nairobi, Kenya.
Waziri Mahiga akimpongeza Waziri Czaputowicz kwa uamuzi wa nchi hiyo wa  kufungua Ofisi za Ubalozi hapa nchini.
Mhe. Waziri Mahiga kwa pamoja na Mhe. Waziri Czaputowicz wakizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu umuhimu wa ufunguzi wa ofisi za Ubalozi wa Poland nchini.
Mkutano kati ya Mhe. Waziri Mahiga na Mhe. Waziri Czaputowicza na waandishi wa habari ukiendelea.

Waziri Mahiga ampokea nchini Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe.Balozi Dkt. Augustine Mahiga akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe. Prof. Jacek Czaputowicz mara baada ya kumkaribisha rasmi Wizarani tarehe 12 Aprili, 2018. Katika mazungumzo yao walisisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano katika nyanja mbalimbali zikiwemo elimu, kilimo, utalii, biashara na uwekezaji. Mhe. Czaputowicz yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili ambapo pamoja na mambo mengine atazindua rasmi ubalozi wa nchi hiyo hapa nchini.
Mhe. Waziri Mahiga na Mhe. Waziri Czaputowicz wakionesha Mkataba wa Makubaliano kuhusu ushirikiano kati ya Tanzania na Poland.
Mkurugenzi na Mkuu wa Itifaki, Balozi Grace Martin (kulia)  kwa pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika, Bw. Salvator Mbilinyi (kushoto), Afisa Mambo ya Nje, Bi. Mona Mahecha (wa pili kushoto) na Afisa Mawasiliano, Bi. Robi Bwiru (wa pili kulia) wakifuatilia mazungumzo kati ya Waziri Mahiga na Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe. Czaputowicz (hawapo pichani).
Balozi wa Poland nchini, Mhe. Krzysztof Buzalski (kulia) akiwa na Wajumbe wengine kutoka Poland  wakifuatilia mazungumzo kati ya Mhe. Waziri Mahiga na Waziri wa Mambo ya Nje wa Poland, Mhe  Czaputowicz (hawapo pichani)
Picha ya pamoja.

Waziri Mahiga ahimiza wadhamini zaidi kujitokeza kufanikisha Wiki ya Tanzania nchini Kenya

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga (kulia) akiwa na  Mkurugenzi wa Idara ya Diaspora ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Maandalizi ya Maonesho ya Bidhaa za Viwanda vya Tanzania nchini Kenya, Balozi Anisa Mbega walipokutana na Wadhamini na Wajumbe wa Kamati ya maandalizi ya maonesho hayo (hawapo pichani) yanayotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 25 - 28 Aprili 2018 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Kenyatta (KICC) Jijini Nairobi, Kenya. 

Mazungumzo hayo yamefanyika leo tarehe 12 Aprili 2018 katika Ofisi za Wizara Jijini Dar es Salaam  na kuambatana na hafla ya kukabidhi udhamini kwa ajili ya  kufanikisha  maonesho hayo maarufu kama ''Wiki ya Tanzania nchini Kenya'' ambayo yataenda sambamba na sherehe za miaka 54 za Muungano wa Tanzania. 


Sehemu ya wadhamini na  wajumbe wa kamati ya maandalizi wakifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiongozwa na Mhe. Waziri Mahiga (hayupo pichani)
Viongozi wa Kampuni ya NIDA TEXTILE MILLS (T) wakimkabidhi Mhe. Waziri Mahiga mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi 22,700,000/- kwa ajili ya kudhamini maonesho ya didhaa za viwanda vya Tanzania nchini Kenya. Kushoto ni Meneja Mkuu wa Kampuni hiyo Bw. Muhammad Waseem.

Mhe. Waziri Mahiga akimshukuru Mwakilishi wa Kampuni ya Mohamed Enterprises, Bi. Barbara Gonzale baada ya kutoa ahadi ya udhamini wa kiasi cha shillingi millioni ishirini na tano (25,000,000) kwa ajili ya kudhamini maonesho hayo.
Mhe. Waziri Mahiga akimshukuru mwakilishi kutoka kampuni ya Tanzania Distilleries Ltd, Bw. Maleke Hans baada ya kutoa ahadi ya udhamini wa kiasi cha Dola za Marekani 5,000 (sawa na shilingi milioni kumi na moja  za Tanzania).
Mhe. Waziri Mahiga akisikiliza taarifa fupi ya udhamini na hatua ya maandalizi iliyofikiwa  kutoka kwa Katibu wa Kamati, Balozi Mbega, pembeni ni baadhi ya Wadhamini na Wajumbe wa Kamati.
Sehemu nyingine ya wajumbe wa kamati wakifuatilia ufafanuzi uliokuwa ukitolewa na Balozi Mbega kwa Mhe. Waziri Mahiga.
Picha ya pamoja.