Tuesday, May 13, 2014

Waziri Membe awasili Malawi kumwakilisha Mhe. Rais Kikwete kwenye mazishi ya aliyekuwa Balozi wa Malawi nchini

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Blantyre nchini Malawi kwa ajili ya kushiriki mazishi ya aliyekuwa Balozi wa Malawi nchini Tanzania, Marehemu Flossie Gomile-Chidyaonga aliyefarikii dunia tarehe 09 mei, 2014 Jijini na Dar es Salaam na anatarajiwa kuzikwa tarehe 14 Mei, 2014. Mhe. Membe anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kwenye mazishi hayo.
Balozi wa Tanzania nchini Malawi,  Mhe. Patrick Tsere akimweleza jambo Mhe. Membe wakati wa mapokezi.
Mhe. Membe akijaribu kumwelezea Rais wa Malawi, Mhe. Joyce Banda namna alivyozipokea taarifa za kifo cha Balozi Flossie. Kushoto kwa Mhe. Rais Banda ni mume wake Jaji Mkuu Mstaafu Banda na kulia kwa Mhe. Membe ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Malawi, Mhe. Ephraim Chiume.
Baadhi ya Wananchi wa Blantyre na sehemu nyingine za Malawi wakiwa uwanjani hapo wakati wa mapokezi ya Mwili wa aliyekuwa Balozi wa Malawi nchini Tanzania, Marehemu Flossie Gomile-Chidyaonga.
Mhe. rais Banda akisalimiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. John Haule.
Mhe. Rais Banda akisalimiana na Balozi Vincent Kibwana, Mkurugenzi wa Idara ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Mhe. Rais Banda akisalimiana na Mwakilishi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) nchini Tanzania pamoja na Mabalozi wengine waliofutana na Mhe. Membe nchi Malawi kwenye mazishi ya Marehemu Balozi Flossie.
Mhe. Rais Banda akimtambulisha kwa Mhe. Membe Mtoto pekee wa Marehemu Balozi Flossie-Gomile-Chidyaonga.

Mhe. Rais Banda, Mhe. Membe, Mhe. Chiume na Wajumbe wengine wakisubiri jeneza lililobeba mwili wa marehemu Balozi Flossie kuteremshwa kwenye ndege kwa ajili ya taratibu zingine.
Jeneza lililobeba mwili wa Marehemu Balozi Flossie likiwa limeteremshwa kwenye ndege.
Mhe. Rais Banda akihutubia mara baada ya mapokezi ambapo alitoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano.
Mhe. Membe nae akizungumza machache.
Wananchi wakifuatilia hotuba.
Mwakilishi wa Familia ya  Marehemu Balozi Flossie nae akizungumza kwa niaba ya familia hiyo.
Kwaya ikiimba wakati wa shughuli hizo.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb.) amemtaja aliyekuwa Balozi wa Malawi nchini Tanzania Marehemu Flossie-Gomile Chidyaonga kama Malkia wa Amani kwa vile alikuwa mstari wa mbele katika vikao vya usuluhishi na kutafuta amani kwenye Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) Malawi ikiwa ni Mwenyekiti wa jumuiya hiyo.
Mhe. Membe aliyasema hayo wakati wa mapokezi maalum ya Marehemu Balozi Chidyaonga yaliyofanyika katika Uwanja wa Ndege wa Blantayre nchini Malawi na kuhudhuriwa na Rais wa Malawi, Mhe. Joyce Banda, Viongozi wa Serikali ya Malawi, Familia ya Marehemu, Taasisi za Dini, Mabalozi na Wananchi kutoka sehemu mbalimbali za mji huo.

Mhe. Membe ambaye anamwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Kikwete kwenye mazishi ya Marehemu Balozi Flossie Gomile-Chidyaonga alisema kwamba Tanzania, Malawi, nchi za SADC na dunia kwa ujumla imempoteza mwanadiplomasia mahiri ambaye aliujua na kutekeleza wajibu wake ipasavyo.

“Kwa niaba ya Mhe. Rais Kikwete, Watanzania wote na mimi binafsi nakuomba Mhe. Rais Banda na Wananchi wa Malawi mpokee salamu zetu za pole kwa kumpoteza Balozi Flossie ambaye alikuwa mstari wa mbele katika masuala ya amani kwa Kanda ya SADC na ninamwita Malkia wa Amani kwa juhudi hizo alisema Mhe. Membe”.

Mhe. Membe aliongeza kusema kwamba kutokana na kufanya kazi kwa kujituma na kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Malawi, Marehemu  Balozi Flossie alikubalika Serikalini, kwa Mabalozi wenzake na hata katika Taasisi za Elimu ya Juu kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambako alishiriki katika kutoa mihadhara mara kwa mara.

Katika hotuba yake wakati wa mapokezi hayo, Rais wa Malawi Mhe. Joyce Banda alisema kuwa wameupokea msiba huo wa ghafla kwa majonzi makubwa ambapo kwa namna ya pekee aliishukuru Serikali ya Tanzania hususan Rais Kikwete kwa ushirikiano wa hali ya juu aliouonesha tangu msiba utokee na kutuma ujumbe mzito uliioongozwa na Waziri Membe kumsindikiza Marehemu Flossie nchini Malawi.

“Mimi binafsi na wananchi wa Malawi tunatoa shukrani za dhati kwa ndugu zetu Watanzania hususan  Mhe. Rais Kikwete kwa ushirikiano walioonesha katika kipindi hiki kigumu kwetu. Mhe. Rais Kikwete aliwasiliana na mimi akiwa safarini mara tu msiba ulipotokea. Alielezea kushtushwa na msiba huo wa ghafla kama mimi nilivyoshtushwa. Nilimweleza azma ya Serikali yangu kuhusu kutuma ndege kwa ajili ya kuufuata mwili wa ndugu yetu Flossie lakini alisema nimwachie  hilo ni jukumu lake na amelitekeleza kikamilifu kama tunavyoona” alisema kwa masikitiko Mhe. Banda.

Awali akizungumza kwa niaba ya Familia ya Marehemu Balozi Flossie, Msemaji wa Familia hiyo Bw. Andrew  naye aliishukuru Serikali ya Tanzania na kusema kuwa ushirikiano uliooneshwa katika kipindi hiki kigumu kwao unadhihirisha undugu mkubwa uliopo kati ya Tanzania na Malawi.

Baadhi ya Viongozi wa Serikali na Mabalozi waliofuatana na Mhe. Mhe. Membe kwenye msiba huu ni pamoja na Bw. John Haule, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikano wa Kimataifa, Balozi Vincent Kibwana, Mkurugenzi wa Idara ya Afrika, Kaimu Mkuu wa Mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania ambaye pia ni Balozi wa Zimbabwe, Balozi wa Zambia nchini, Mhe. Judith Kangoma, Balozi wa Norway nchini na Maafisa wa Ubalozi wa Malawi nchini.

Marehemu Balozi Flossie Gomile-Chidyaonga ambaye alifariki dunia katika Hospitali ya Aga Khan Jijini Dar es Salaam tarehe 09 Mei, 2014 anatarajiwa kuzikwa katika Mji wa Blantyre nchini Malawi tarehe 14 Mei, 2014.



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.