Wednesday, February 24, 2016

Tanzania na Uturuki kuimarisha ushirikiano katika sekta mbalimbali

Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akisalimiana na Mhe. Mevlut Cavusoglu, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki alipowasili nchini humo kwa ziara ya kikazi ya siku mbili kwa madhumuni ya kukuza ushirikiano baina ya Tanzania na Uturuki.
Mhe. Dkt. Mahiga na Mhe.Cavusoglu wakiwa katika mazungumzo ya kuimarisha ushirikiano baina ya Tanzania na Uturuki
Mazungumzo yakiendelea
===========================================

Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dr. Augustine Mahiga amefanya ziara ya kikazi nchini Uturuki tarehe 23 na 24 Februari, 2016.

Wakati wa ziara hiyo Mhe. Mahiga alikutana kwa mazungumzo na Mhe. Mevlut Cavusoglu, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki pembeni mwa Mkutano wa Mawaziri kuhusu Somali, uliofanyika mjini Istanbul Uturuki tarehe 23na 24 Februari, 2016. 

Katika mazungumzo, Mawaziri hao walikubaliana kukuza mahusiano mazuri yaliyopo baina ya Tanzania na Uturuki kwa kutilia mkazo mahusiano ya kibiashara na uwekezaji. Aidha, Mhe. Waziri Mahiga aliwakaribisha Waturuki kuja nchini kwa ajili ya kuwekeza katika sekta ya kilimo hususan kuanzisha viwanda vya kuongeza thamani mazao ya kilimo. 

Vilevile, aliwakaribisha kuweka program za kubadilishana uzoefu kwenye sekta ya kilimo baina ya wataalam wa Uturuki na Tanzania. 

Kwa upande wake, Mhe. Cavusoglu alieleza kwamba Uturuki inaipa Tanzania kipaumbele kama nchi ambayo ingependa kukuza mahusiano nayo ya kibiashara na uwekezaji. Pia alimkaribisha Mhe.  Waziri Mahiga na Tanzania kushiriki katika maonyesho ya biashara ya Expo 2016 pamoja na maonyesho ya Soko la Afrika, hapo baadae mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.