Tuesday, November 5, 2019

MABALOZI WA NCHI ZA SADC, NEW DELHI WAENDELEA KUPAZA SAUTI KUPINGA VIKWAZO DHIDI YA ZIMBABWE

Balozi wa Tanzania nchini India na Mwenyekiti wa Kundi la Mabalozi wa Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Mhe. Baraka Luvanda, akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya SADC (SADC Day) yaliyofanyika Jijini New Delhi tarehe 02 Novemba 2019.
Wageni waalikwa wakimsikiliza Mhe. Balozi Luvanda (hayupo pichani) alipohutubia wakati wa hafla ya SADC Day
Mhe. Fortune Chasi, Waziri wa Nishati wa Zimbabwe na Mgeni Maalum akihutubia wakati wa hafla ya Siku ya SADC iliyofanyika nyumbani kwa Balozi wa Tanzania nchini, Jijini New Delhi tarehe 02 Novemba 2019

Mgeni rasmi wa hafla ya Siku ya SADC, Bwana Rajesh Swami, Mkurugenzi katika Wizara ya Mambo ya Nje ya India, Sehemu ya Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika akihutubia wakati wa hafla ya Siku ya SADC iliyofanyika nyumbani kwa Balozi wa Tanzania nchini India, Jijini New Delhi tarehe 02 Novemba 2019.
Mhe. Balozi Luvanda akiwa na Mabalozi na Viongozi mbalimbali waliohudhuria hafla ya Siku ya SADC

Balozi Luvanda akiwa katika picha ya pamoja na Mhe. Fortune Chasi, Waziri wa Nishati wa Zimbabwe ambaye alishiriki hafla ya Siku ya SADC kama Mgeni Maalum

Picha ya pamoja 
==================================================================

Mabalozi wa nchi za SADC, New Delhi waendelea kupaza sauti kupinga vikwazo dhidi ya Zimbabwe

Mabalozi wa Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) waliopo nchini India chini ya Uenyekiti wa Mhe. Baraka Luvanda, Balozi wa Tanzania nchini humo walikutana katika hafla ya Siku ya SADC (SADC Day), iliyofanyika nyumbani kwa Balozi Luvanda jijini New Delhi, India tarehe 2 Novemba 2019.

Wakati wa hafla hiyo, Mhe. Balozi Luvanda alitumia fursa hiyo kuelezea pamoja na mambo mengine, suala la kuondolewa vikwazo vya kiuchumi vilivyowekwa na nchi za Ulaya dhidi ya Zimbabwe. Alieleza kuwa Tamko dhidi ya vikwazo hivyo liliwasilishwa rasmi kwenye Mamlaka za Serikali ya India siku ya tarehe 25 Oktoba 2019 siku ambayo iliamuliwa na Viongozi Wakuu wa Nchi za SADC kuwa siku maalum ya kupaza sauti dhidi ya vikwazo hivyo.

Kwa upande wake, Mgeni rasmi katika shughuli hiyo, Mkurugenzi katika Wizara ya Nje ya India, Sehemu ya Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika, Bwana Rajesh Swami alieleza kuwa kwa miaka mingi uhusiano baina ya India na nchi za SADC umekuwa mzuri na kuwezesha biashara, uwekezaji, utalii, elimu, afya na uhusiano wa mtu na mtu kuimarika kwa kiwango cha juu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mgeni Maalum, Mhe. Fortune Chasi, Waziri wa Nishati wa Zimbabwe, alimshukuru Balozi Luvanda, Mwenyekiti wa Mabalozi wa Nchi za SADC nchini India na Mabalozi wote wa nchi za SADC nchini humo kwa kuandaa hafla hiyo na jinsi walivyosimamia suala la kupaza sauti kupinga vikwazo dhidi ya nchi yake na kuwaomba waendelee na juhudi hizo hadi vikwazo hivyo vitakapoondolewa.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.