Tuesday, November 19, 2019

USHIRIKIANO KATI YA TANZANIA NA SHIRIKA LA AALCO KUENDELEA KUIMARIKA

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Baraka Luvanda akizungumza wakati hafla ya Maadhimisho ya Miaka 63 ya kuanzishwa kwa  Shirika la Mashauriano ya Kisheria ya Nchi za Asia na Afrika (AALCO) yaliyofanyika jijini New Delhi tarehe 15 Novemba 2019.
Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Baraka Luvanda [kushoto] akiwa katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Shirika la Mashauriano ya Masuala ya Kisheria ya Nchi za Asia na Afrika [AALCO], Prof. Kennedy Gastron wakati wa hafla ya maadhimisho ya miaka 63 ya kuanzishwa kwa shirika hilo, Jijini New Delhi tarehe 15 Novemba 2019
Mhe. Balozi Luvanda akiwa  katika meza moja na viongozi mbalimbali wakati wa maadhimisho ya miaka 63 tangu kuanzishwa kwa Shiriko la AALCO
Wageni waalikwa wakiwa kwenye maadhimisho
Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Baraka Luvanda akiwa katika picha ya pamoja na Mabalozi pamoja na Maafisa Ubalozi  wa nchi wanachama wa AALCO  walioshiriki hafla ya  maadhimisho ya miaka 63 ya kuanzishwa kwa shirika hilo, Jijini New Delhi tarehe 15 Novemba 2019.
=======================================================

Ushirikiano kati ya Tanzania na Shirika la Mashauriano ya masuala ya Kisheria ya Nchi za Asia na Afrika (AALCO) kuendelea kuimarika

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Balozi Baraka Luvanda amemwakilisha Mhe. Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Katiba na Sheria na Rais wa sasa wa Shirika la Mashauriano ya Kisheria ya Nchi za Asia na Afrika (Asia-Africa Legal Consultative Organization-AALCO) kwenye sherehe ya miaka 63 ya kuanzishwa kwake. Sherehe hiyo imefanyika Jijini New Delhi tarehe 15 Novemba 2019 na kuhudhuriwa na nchi wanachama wageni waalikwa, wenyeji na mashirika ya kimataifa yaliyopo New Delhi.

Akisoma hotuba kwa niaba ya Mhe. Mahiga, Balozi Luvanda alielezea uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na AALCO na kueleza kuwa utaendelea kudumishwa kwa manufaa ya pamoja.

AALCO ilianzishwa tarehe 15 Novemba 1956 kwa lengo la kuwa chombo cha ushauri na ushirikiano katika masuala ya sheria za kimataifa kwa nchi za Asia na Afrika. Toka kuanzishwa kwake AALCO imewezesha nchi wanachama kushirikiana na kubadilishana uzoefu katika masuala mbalimbali ya sheria za kimataifa na imechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya sheria za kimataifa.

Ushirikiano kati ya Tanzania na shirika hilo ulianza tangu mwaka 1965 ambapo Tanzania ilishiriki katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa AALCO kama nchi Mwangalizi na baadaye mnamo mwaka 1973 kama nchi mwanachama rasmi. 

Mpaka sasa Tanzania imeshaandaa Mikutano mikubwa 3 ya Mwaka ambapo Mkutano wa 25 wa AALCO ulifanyika mwaka 1986 jijini Arusha, Mkutano wa 49 ulifanyika Jijini Dar es Salaam mwaka 2010 na Mkutano wa 58 ulifanyika hivi karibuni, jijini Dar es Salaam tarehe 21 hadi 25 Octoba 2019.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.