Tuesday, November 19, 2019

UTURIKI KUWEKEZA UJENZI WA VIWANDA VYENYE THAMANI YA DOLA MILIONI 50 SIMIYU

. Kawasaki kutoka Japan nayo yaonesha nia ya kuanzisha kiwanda kitakachohudumia soko la Afrika na Nje ya Afrika

Katika kutekeleza Diplomasia ya Uchumi, Ubalozi wa Tanzania nchini Uturuki umeambatana na wawekezaji kutoka nchini humo kwa ajili ya kuwekeza katika viwanda mkoani Simiyu ambavyo vinatarajiwa kutoa ajira zaidi ya 2000.

Uwekezaji huo utajumuisha kiwanda cha nguo pamoja na kiwanda cha kutengeneza vyombo vya majumbani ambao una thamani ya dola za kimarekani milioni 50. Viwanda hivyo vitajengwa katika eneo la Isanga Mjini Bariadi Mkoani Simiyu na vinatarajiwa kuanza uzalishaji mwaka 2020.

Akizungumza na vyombo vya habari katika eneo ambalo linatarajiwa kujengwa viwanda hivyo mkoani Simiyu, mwekezaji huyo kutoka Uturuki, Bw. Mustafa Albayram ameahidi kujenga viwanda viwili kimojawapo kikiwa ni cha nguo na kingine cha kutengeneza vyombo vya nyumbani ikiwemo vikombe, sahani na glasi.

Bw. Albayram amesema ameridhishwa na mazingira ya uwekezaji baada ya kutembelea maeneo mbalimbali kwa lengo la kuangalia mazingira wezeshi kwa uwekezaji wa viwanda, akiwa ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Prof. Elizabeth Kiondo mkoani Simiyu.

Aidha ameitaka serikali kutatua baadhi ya changamoto ili kuuwezesha uwekezaji huo kufanyika ikiwa ni pamoja na miundombinu yote muhimu hususani ya umeme ili uwekezaji huo uanze mara moja baada ya kukamilisha taratibu zote muhimu zinazohitajika ikiwa ni pamoja na usajili wa kampuni na kutafuta hati miliki ya ardhi.

“Tumeamua kuwekeza Simiyu, kila kitu kikienda sawa kiwanda cha nguo kinaweza kujengwa na kufanya kazi ndani ya miezi tisa mpaka mwaka mmoja, kiwanda cha vyombo vya nyumbani miezi nane baada ya usajili wa kampuni nitarudi tena Simiyu kukamilisha masuala ya hati miliki ya ardhi, sitaki kumuangusha Mhe. Balozi maana amefanya mengi kwa ajili yetu,” alisema Albayram.

Nae Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Prof. Elizabeth Kiondo amesema mwekezaji ameridhishwa na eneo hilo na kuushukuru uongozi wa Mkoa wa Simiyu kwa kutoa ardhi ya kujenga viwanda hivyo huku akibainisha kuwa ombi kubwa la mwekezaji ni upatikanaji wa nishati ya kutosha kwa kuwa viwanda hivyo hutumia umeme mwingi.

Balozi Kiondo ameongeza kuwa, hayo ni matokeo ya utekelezaji wa diplomasia ya uchumi kwa vitendo, hivyo Ubalozi utaedelea kuhamasisha wawekezaji wengine zaidi kuja kuweza nchini, hatimaye kufanikisha azma ya uchumi wa viwanda.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka alimhakikishia mwekezaji huyo upatikanaji wa mahitaji yote muhimu na kuahidi kushirikiana na taasisi za Serikali zinazohusika kuhakikisha anapata huduma zote kwa wakati na pasipo urasimu wowote.

Kuhusu suala la Umeme Mtaka amesema katika Bajeti ya mwaka 2019/20 Wizara ya Nishati kupitia Shirika la umeme TANESCO imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kupozea umeme (substation) ambacho kitajengwa karibu na eneo la uwekezaji huo.

Mtaka ameongeza kuwa mtazamo wa mkoa wa Simiyu ni kuwa na viwanda vichache vitakavyoajiri maelfu ya watanzania badala ya kuwa na viwanda vingi vinavyoajiri watu wachache ili kuwezesha watanzania wengi kupata ajira.

Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa alitoa wito kwa wakulima wa pamba kulima pamba kwa wingi kwa kuwa kiwanda cha nguo kitakuwa mkombozi wa kuongeza thamani ya zao la pamba na itauzwa kwa bei ya uhakika.

Naye Katibu wa Chama cha Wanunuzi wa pamba nchini, Bw. Boaz Ogola amesema kujengwa kwa kiwanda cha nguo mkoani Simiyu kutasaidia wakulima wa pamba kupata soko la uhakika kuondoa changamoto ya bei ya pamba kwa kuwa kitapanua wigo wa soko la pamba, ambapo pamba inayotumika ni chini ya asilimia 20 - 25 ya pamba yote inayozalishwa nchini.

Katika tukio jingine kampuni ya Kawasaki Heavy Industries Ltd kutoka Japan imeonesha nia ya kuanzisha kiwanda nchini ambapo kiwanda hicho kitahudumia soko la Afrika na Nje ya Afrika.

Kawasaki Heavy Industries Ltd ni kampuni nchini Japan ambapo imewekeza katika sekta mbalimbali kama vile sekta ya usafiri (anga, reli na majini)  nishati (cogeneration, energy plants, gas tuibines, gas engines), vifaa vya viwandani (hydraulic components and systems, robotics, industrial plants, environmental and recycling), pamoja na leisure (motorcycle, off-road four wheel,JET SKI).

Naibu Meneja wa Idara ya Mkakati wa Kimataifa, Kitengo cha Biashara cha Kampuni ya Kawasaki Bw. Michio Kambe anatarajia kufanya ziara nchini Tanzania kuanzia tarehe 21 hadi 26 Novemba 2019 ambapo atakutana na kufanya mazungumzo na Kituo cha Uwekezaji Tanzania, Ofisi ya Waziri Mkuu - Uwekezaji na Waziri wa Viwanda na Biashara.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka akioneshwa pamba inavyochambuliwa na mwekezaji kutoka Uturuki, Bw. Mustafa Albayram (mwenye shati jeusi) wakati walipotembelea kiwanda cha kuchambua pamba cha Alliance Ginnery Ltd mkoani Simiyu

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka (katika) akiwa na mwekezaji kutoka Uturuki, Bw. Mustafa Albayram (mwenye shati jeusi) pamoja na maafisa wa serikali pamoja na baadhi ya wafanyakazi wakitembea ndani ya kiwanda cha kuchambua pamba cha Alliance Ginnery Ltd mkoani Simiyu


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka (katika) akiwa na mwekezaji kutoka Uturuki, Bw. Mustafa Albayram (mwenye shati jeusi) na Balozi wa Tanzania nchini Uturuki, Prof. Elizabeth Kiondo (mwenye gauni la kijivu) wakati walipotembelea kiwanda cha kuchambua pamba cha Alliance Ginnery Ltd mkoani Simiyu. Wengine ni maafisa wa serikali pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa kiwanda hicho.



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.