Sunday, February 23, 2020

UNESCO YATAMBUA KISWAHILI KAMA LUGHA ITAKAYOSAIDIA KUKUZA UTANGAMANO BARANI AFRIKA

Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu katika UNESCO, Mhe. Samwel Shelukindo akizungumza kwenye Mjadala kuhusu "Fursa na Changamoto za Kukitambua Kiswahili kama Lugha rasmi ya Bara la Afrika kwa ajili ya kukuza Utangamano. Mjadala huo uliandaliwa na Ubalozi wa Tanzania kwa kushirikiana na UNESCO wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Lugha Mama yaliyofanyika jijini Paris, Ufaransa hivi karibuni.
Sehemu ya Wataalam wa Lugha ya Kiswahili akiwemo Prof. Aldin Mutembei (wa pili kushoto) kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakishiriki kwenye mjadala kuhusu Lugha ya Kiswahili wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Lugha Mama yaliyofanyika Paris, Ufaransa hivi karibuni
Sehemu ya washiriki wa Mjadala huo wakifuatilia kama wanavyoonekana katika picha


Mhe. Balozi Shelukindo (wa pili kushoto) akiwa na baadhi ya Wajumbe kutoka UNESCO  wakiangalia machapisho mbalimbali ya Lugha ya Kiswahili yaliyoandaliwa  na Ubalozi baada ya kushiriki mjadala kuhusu Lugha ya Kiswahili ulioandaliwa na Ubalozi kwa kushirikiana na UNESCO.
===========================================================================

UNESCO YATAMBUA KISWAHILI KAMA LUGHA ITAKAYOSAIDIA KUKUZA UTANGAMANO BARANI AFRIKA

Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) limeitambua Lugha ya Kiswahili kama lugha itakayosaidia kukuza utangamano Barani Afrika wakati wa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Lugha Mama yenye kaulimbiu “Lugha Bila Mipaka” iliyofanyika jijini Paris, Ufaransa hivi karibuni.

Katika kuadhimisha siku hiyo, Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa kwa kushirikiana na UNESCO uliandaa mjadala kuhusu "Fursa na Changamoto za Kukitambua Kiswahili kama Lugha rasmi ya Bara la Afrika kwa ajili ya kukuza Utangamano".

Akizungumza wakati wa Mjadala huo, Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa na Mwakilishi wa Kudumu katika UNESCO, Mhe. Samwel Shelukindo pamoja na mambo mengine, alieleza hatua iliyochukuliwa na Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) chini ya Mwenyekiti wake, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kukifanya Kiswahili kuwa moja ya lugha zitakazotumika katika Jumuiya hiyo.

Aidha, Mhe. Balozi Shelukindo alizipongeza nchi za Afrika  Kusini na Namibia kwa kuwa nchi za kwanza Kusini mwa Afrika  zilizoamua kuanzisha ufundishwaji wa lugha ya Kiswahili katika shule mbalimbali. Mjadala huo uliwashirikisha Wataalam mbalimbali akiwemo Prof. Aldin Mutembei kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,

Kufanyika kwa mjadala huo katika UNESCO ni moja ya juhudi zinazofanywa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kupitia Ubalozi wa Tanzania nchini Ufaransa za kukifanya Kiswahili kuwa moja ya lugha zitakazotumika katika UNESCO. 


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.