Friday, February 7, 2020

Tanzania yaibuka mshindi wa kwanza Tuzo ya Utalii nchini India

Balozi wa Tanzania nchini India, Mhe. Baraka Luvanda (wa tatu kulia) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Maonesho ya Kimataifa ya Utalii baada ya kupokea Tuzo ya ushindi wa kwanza kwenye kipengele cha Banda Bora la Maonesho lililopambwa kwa unadhifu na kuvutia watu wengi (The Winner of Best Decoration Award) katika maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya mwaka 2020 jijini Mumbai, India tarehe 5 Februari 2020
Balozi Luvanda akiwa na wadau kwenye Banda la Tanzania
Mhe. Balozi Luvanda akiwa na wadau mbalimbali walioshiriki maonesho ya Utalii jijini Mumbai
Wageni wakiwa wamefurika kwenye Banda la Tanzania kwa ajili ya kupata maelezo kuhusu masuala ya utalii
Picha ya pamoja
========================================================


Tanzania yashinda kwa mara ya pili Tuzo ya Maonesho ya Kimataifa ya Utalii, India.
Tanzania imeibuka mshindi wa kwanza wa Banda Bora katika maonesho ya Kimataifa ya Utalii yajulikanayo kama Outbound Travel Mart 2020 (OTM 2020) yaliyofanyika nchini India hivi karibuni.
Ubalozi wa Tanzania, New Delhi, Taasisi za Serikali na kampuni binafsi mbalimbali za utalii nchini zimeshiriki Maonesho hayo kwa lengo la kutangaza na kutafuta fursa mpya za soko la utalii nchini humo.
Maonesho hayo maarufu na makubwa katika ukanda wa Asia na Pasifiki ambayo hufanyika kila mwaka jijini Mumbai na kuzishirikisha taasisi mbalimbali za utalii duniani, yamefanyika kuanzia tarehe 3 hadi 5 Februari, 2020.
Wakati wa maonesho hayo, Banda la Tanzania limeibuka tena Mshindi wa Kwanza kwa upande wa Banda bora lilopambwa kwa unadhifu na kuvutia watu wengi (The winner of Best Decoration Award). Tanzania imeshinda tuzo hiyo kwa mara ya pili mfululizo ambapo katika maonesho ya mwaka 2019, Tanzania pia ilishinda tuzo hiyo.
Akizungumzia maonesho hayo, Balozi wa Tanzania nchini India Mhe. Baraka Luvanda amesema kuwa maonesho hayo ni fursa nyingine adhimu kwa nchi kutangaza vivutio vya utalii ambapo wafanyabiashara wapatao 15,000 wanaojishughulisha na masuala ya utalii walishiriki kutoka katika mataifa zaidi ya 50 duniani. Aidha alisema kuwa, Washiriki wamepata fursa ya kupeana taarifa muhimu kuhusu mwelekeo na maendeleo ya biashara ya utalii katika maeneo mbalimbali duniani, vivutio vipya pamoja na kufanya biashara.
Kadhalika, Balozi Luvanda ameeleza kuwa, maonesho yalisaidia washiriki wa Tanzania kukutana na wadau na kuanzisha uhusiano wa kibiashara unaotarajiwa kufungua soko la utalii nchini baada ya wadau hao kupata maelezo ya kutosha kuhusu vivutio vilivyopo nchini na faida zake. 

“Nachukua fursa hii kwa dhati kuwapongeza sana Maafisa wote walioshiriki katika Banda letu la Tanzania la Maonesho kwa kazi nzuri ya kutangaza vivutio vya utalii nchini iliyowezesha tupate ushindi mwingine katika maonesho haya kwa mara ya pili kwa upande wa Banda bora lilopambwa kwa unadhifu na kuvutia watu wengi (The winner of Best Decoration Award)”, alisema Balozi Luvanda.

Kwa ujumla, India ina soko kubwa la utalii. Idadi ya watalii kutoka India wanaokwenda Tanzania sasa imeongezeka mara dufu baada ya kuanza kwa safari za ndege za Shirika la Ndege la Tanzania (Air Tanzania) moja kwa moja kutoka Tanzania kuja India na katika hilo alitoa wito kwa wafanyabiashara hao kuendelea kutumia fursa hiyo kuongeza idadi ya watalii wa India kutembelea Tanzania.

Taasisi za Serikali ya Tanzania zilizoshiriki ni pamoja na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA), Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na Shirika la Ndege la Tanzania (Air Tanzania). Kampuni binafsi zilizoshiriki ni pamoja na Zara Tours, Mount Meru Hotel na Nature’s Land Safaris & Rentals.




No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.