Saturday, April 26, 2014

Sherehe za miaka 50 ya Muungano zafana

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete akikagua  Gwaride Maalum lililoandaliwa kwa ajili ya sherehe za kilele cha maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika  na Zanzibar zilizofanyika kwenye Viwanja vya Uhuru jijini Dar es Salaam tarehe 26 Aprili, 2014.
Mhe. Rais Kikwete akisalimiana na Rais wa Uganda Kaguta Yoweri Museveni huku Mfalme Mswati wa Swaziland, Rais wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohammed Shein wakishuhudia tukio hilo. 
Mhe. Rais Kikwete akisalimiana na Rais wa Kenya, Mhe. Uhuru Kenyatta.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (aliyenyoosha kidole) akimwonesha kitu Waziri wa Mambo ya Nje wa Zimbabwe wakati wa sherehe za miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
 Kikosi cha Makomando wakionesha mbele ya Mhe. Rais, wageni waalikwa na wananchi mafunzo waliyopitia.
Moja ya zana za  kivita za kisasa zikipitishwa mbele  ya Mhe. Rais Kikwete na wageni waalikwa ikiwa ni moja ya kusherehea miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Ndege za kivita nazo zikipita angani .
Mwanajeshi akitua na mwanvuli kutoka angani mita 4000 kutoka usawa wa bahari
Watoto wa Halaiki wakionesha umbo la picha za Rais wa Kikwete na Rais Shein na maneno yanayosomeka Miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar
Watoto kutoka Tanzania Bara na Zanziba wakionesha utaalamu wa kucheza ngoma
Kikundi cha Wasanii mbalimbali wakiimba wimbo maalum wa pamoja kuhusu miaka 50 ya Muungano

Picha Reginald Philip.

Makamu wa Rais wa Nigeria awasili nchini kushiriki sherehe za muungano

Ndege iliyo mbeba Makamu wa Rais wa Nigeria Mhe. Mohammed Namadi Sambo ikiwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julias Nyerere

Makamu wa Rais wa Nigeria,  Mhe. Mohammed Namad Sambo akishuka katika ndege mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. Makamu huyo wa Rais ambaye alimwakilisha Rais wake ni miongoni mwa viongozi wengi watakaoshiriki sherehe za miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika  na Zanzibar.

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi akimpokea Makamu wa Rais wa Nigeria Mhe. Mohammed Namad Sambo  baada ya kuwasili  katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Makamu wa Rais wa Nigeria ni miongoni mwa viongozi wengi kutoka duaniani kote watakaoshiriki Maadhimisho ya kilele cha miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yatakayofanyika tarehe 26 Aprili, 2014.

Picha na Reginald Kisaka

Friday, April 25, 2014

Naibu Waziri ampokea Waziri Mkuu wa Rwanda atakayeshiriki sherehe za Muungano

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb.) akiongozana na Waziri Mkuu wa Rwanda, Mhe. Pierre Habumuremyi mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuhudhuria sherehe za kilele cha Maadhimisho ya Miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar hapo zitakazofanyika tarehe 26 Aprili, 2014.
Mhe. Habumuremyi kwa pamoja na Mhe. Mahadhi wakiangalia burudani iliyokuwa ikitolewa na moja ya kikundi cha ngoma Uwanjani hapo.
Mhe. Dkt. Maalim akizungumza na Mhe. Habumuremyi huku Balozi wa Rwanda hapa nchini Mhe. Dkt. Benjamin Rugangazi akisikiliza.
Mhe. Habumuremyi na Mhe. Dkt. Maalim wakimsikiliza Balozi Rugangazi wakati akiwaeleza jambo.

Naibu Spika wa China awasili kwa ajili ya kushiriki sherehe za Muungano


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb.) akiwa na Makamu Mwenyekiti wa Chama cha National People's Congress cha China na Naibu Spika, Mhe. Chen Changzhi wakimsikiliza Mkalimani wakati wa mazungumzo yao mara baada ya Mhe. Chen kupokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Mhe. Chen yupo nchini akimwakilisha Rais wa China kwenye maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar hapo tarehe 26 Aprili, 2014.
Mazungumzo yakiendelea. Kulia kwa Mhe. Chen ni Balozi wa China hapa nchini Mhe. Lu Youqing na kushoto kwa Mhe. Maalim ni Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Mbelwa Kairuki.

Katibu Mkuu azungumza na Naibu Katibu Mkuu wa Jimbo la Guangdong


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,  Mhe. John Haule akisalimiana na Naibu Katibu Mkuu wa Serikali ya Jimbo la Guangdong la nchini China, Mhe. Liu Xiaojie mara baada ya Naibu Katibu Mkuu huyo kuwasili Ofisini kwake kwa mazungumzo hivi karibuni. Anayeshuhudia katikati ni Bi. Bertha Makilagi, Afisa Mambo ya Nje katika Idara ya Asia na Australasia.
Mhe. Haule akizungumza na Mhe. Liu kuhusu ushirikiano kati ya Jimbo la Guangdong na Serikali ya Tanzania. Masuala ya ushirikiano yaliyozungumzwa ni pamoja na biashara, uwekezaji na utalii. Aidha, Mhe. Haule alimweleza azma ya Tanzania ya kufungua Ubalozi Mdogo mjini Guangzhou.
Mkurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Mbelwa Kairuki akiwa na mwakilishi kutoka Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) wakati wa mkutano wa Katibu Mkuu, Mhe. John Haule na Naibu Katibu Mkuu wa Serikali ya Jimbo la Guangdong.
Baadhi ya wajumbe waliofuatana na Mhe. Liu, Naibu Katibu Mkuu wa Jimbo la Guangdong la nchini China.
Katibu Mkuu, Mhe. Haule akifafanua jambo wakati wa mkutano wake na Mhe. Liu na ujumbe wake kama wanavyoonekana pichani.
Mhe. Liu nae akizungumza wakati wa kikao na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. John Haule (hayupo pichani).
Mhe. Haule na Mhe. Liu katika picha ya pamoja na wajumbe wengine kutoka China na Tanzania.
Mhe. Haule akiagana na mgeni wake Mhe. Liu mara baada ya mazungumzo yao.

Waziri Membe ampokea Mfalme Mswati III kwa ajili ya Muungano

Ndege iliyombeba Mfalme Mswati  III wa Swaziland ikiwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Mfalme Mswati ni miongoni mwa Viongozi kutoka mataifa mbalimbali duniani watakaoshiriki maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Mfalme Mswati III akishuka kwenye Ndege mara baada ya kuwasili nchini.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Bernard K. Membe (Mb) akiwa pamoja na Mke wake Mama Dorcas Membe (katikati) pamoja na Balozi wetu nchini Msumbiji ambaye anawakilisha pia Swaziland Mhe. Shamim Nyanduga wakishuhudia kuwasili kwa Mfalme Mswati IIi
Waziri Membe akisalimiana na Mfalme Mswati mara baada ya kuwasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius  Nyerere.
Waziri Membe akisalimiana na Mke wa Mfalme Mswati III.
Mfalme Mswati III akisalimiana na viongozi mbalimbali waliokuwepo Uwanjani hapo kwa mapokezi.
Mh. Membe akiongozana  na Mfalme Mswati III mara baada kumpokea
Mama Membe akiongozana na Mama Mswati III


Waziri Membe akizungumza na Mfalme Mswati III walipokuwa wakiangalia burudani iliyokuwa ikitolewa na kikundi cha matarumbeta (hakipo pichani).
Mfalme Mswati III pamoja na Waziri Membe wakiangalia burudani ya kikundi cha matarumbeta.


Picha na Reginald Philip.

Viongozi waanza kuwasili nchini kwa ajili ya Maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim  akimpokea Waziri Mkuu wa Msumbiji,  Mhe. Dr. Alberto Antonio Vaquina mara baada ya kuwasili  katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Waziri Mkuu huyo ambaye ameambatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Mhe. Eduardo Coloma ni miongoni mwa viongozi wengi kutoka duaniani kote watakaoshiriki Maadhimisho ya kilele cha miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yatakayofanyika tarehe 26 Aprili, 2014.
Mhe. Vaquina akiwa na mwenyeji wake Naibu Waziri Mambo ya Nje Dkt. Maalim wakitizama burudani ya ngoma iliokuwa ikitolewa Viwanjani hapo.
Mhe. Dkt. Maalim akizungumza na Dkt. Alberto Antonio Vaquina, Waziri Mkuu wa Msumbiji mara baada ya mgeni huyo kuwasili.

Picha na Reginald Philip.

Wednesday, April 23, 2014

Mhe. Naibu Waziri azindua Kambi ya Airtel Rising Stars International Soccer

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb.) akitoa hotuba wakati wa uzinduzi wa Kambi Maalum ya Kimataifa ya Mafunzo ya Mpira wa Miguu kwa vijana wa kike na kiume wenye umri chini ya miaka 17 kutoka nchi 12 za Afrika ikiwemo Tanzania. Uzinduzi huo ulifanyika Viwanja vya Azam vilivyopo Chamazi jijini Dar es Salaam tarehe 23 Aprili, 2014. Kambi hiyo inadhaminiwa kwa ushirikiano kati ya kati ya Kampuni ya Simu ya Airtel-Tanzania na Klabu ya Mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza.
Baadhi ya vijana hao wakimsikiliza kwa makini Mhe. Naibu Waziri (hayupo pichani).
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Simu ya Airtel-Tanzania, Bw. Sunil Colaso ambao ni wadhamini wa kambi hiyo kwa kushirikiana na Manchester United akizungumza wakati wa uzinduzi huo.
Mhe. Mahadhi akimsikiliza Bw. Colaso, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel-Tamnzania (hayupo pichani wakati wa uzinduzi huo.
Mmoja wa Walimu kutoka Manchester United Bw. Neil Scott akizungumza wakati wa uzinduzi huo.

Katibu wa Naibu Waziri, Bw. Adam Isara akiwa na mmoja wa wadau wa michezo wakati wa uzinduzi huo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Vijana kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Bw. Ayoub Nyenzi akizungumza wakati wa uzinduzi huo.
Mkurugenzi wa Airtel Tanzania, Bw. Sunil Colaso kwa pamoja na Walimu wa Vijana hao chini ya miaka 17 wakimsikiliza Bw. Nyenzi (hayupo pichani) kutoka TFF alipokuwa akizungumza. Kulia ni Bw. Andrew Stokes na katikati ni Bw. Neil Scott.
Wanamichezo na wageni waalikwa wakimsikiliza Mhe. Naibu Waziri.
Mshereheshaji Bw. Ephraim Kibonde akiendelea na kazi
Mhe. Maalim akipongezwa na Bw. Colaso baada ya kutoa hotuba.
Mhe. Maalim akielekea kuzindua rasmi kambi hiyo kwa kupiga mpira.
Mmoja wa vijana hao ambaye ni mlinda mlango akiwa tayari kudaka mpira kutoka kwa Naibu Waziri.

Mhe. Naibu Waziri akijiandaa kupiga mpira kuashiria kuzindua kambi hiyo ya vijana.
Mhe. Maalim akimsikiliza Naibu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo katika Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Bibi Juliana Yasoda ambaye pia alishiriki uzinduzi huo.

Mhe. Naibu Waziri akizungumza na Waandishi wa Habari
Vijana hao wakiwa kwenye mazoezi
Mhe. Naibu Waziri katika picha ya pamoja na viongozi walioambatana na wanamichezo.
Mhe. Maalim katika picha ya pamoja  na wanamichezo.
Picha na Reginald Philip




Naibu Waziri wa Mambo ya Nje azindua Airtel Rising Stars International Soccer

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mhe. Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb.) amezindua rasmi Kambi Maalum ya Kimataifa ya Mafunzo ya Mpira wa Miguu kwa vijana wa kike na wa kiume wenye umri chini ya miaka 17 kutoka nchi 12 za Afrika ikiwemo Tanzania.

Uzinduzi wa Kambi hiyo umefanyika katika Viwanja vya Azam vilivyopo Chamazi Jijiji Dar es Salaam tarehe 23 Aprili, 2014 na inadhaminiwa kwa ushirikiano kati ya Kampuni ya Simu ya Airtel-Tanzania na Klabu ya Mpira wa Miguu ya Manchester United ya Uingereza. 

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo Mhe. Dkt. Maalim amesema kuwa, kambi hiyo inalenga kuwapatia mafunzo maalum vijana hao wadogo ili kuwawezesha kuwa wachezaji mahiri katika mchezo huo ambao unapendwa na watu wengi duniani ikiwemo Tanzania.

“Mimi binafsi kama ilivyo kwa mamilioni ya Watanzania, mpira wa miguu una nafasi maalum katika mioyo yetu na tunazitambua na kuzipongeza jitihada zinazofanywa na Kampuni ya Simu ya Airtel kwa ushirikiano na Manchester United katika kusaidia maendeleo ya mchezo huo hapa Tanzania na sehemu nyingine za Bara la Afrika. Asanteni sana Airtel na Manchester United” alishukuru Mhe. Maalim.

Mhe. Maalim alieleza kuwa, mafunzo hayo ambayo yatasimamiwa na Waalimu kutoka Shule za Mpira wa Miguu za Timu kubwa ya Manchester United, yanalenga kuwaandaa vijana hao wadogo na kukuza vipaji vyao katika mafanikio ya mpira wa miguu Afrika kwani watu wanahitaji kuona mapinduzi katika mchezo huo na kuondokana na matokeo mabaya katika mashindano ya kimataifa.

“Ushiriki wa watoto wetu kwenye mafunzo haya ambayo yatajikita katika kuwajengea uwezo kiakili, kimwili na kisaikolojia, yatawasaidia kuwa na umoja, yatawapa kujiaamini na hatimaye kuwawezesha kufanya vizuri katika masomo yao kutokana na afya njema na pia kuwa wachezaji wa kulipwa Barani Afrika na duniani hapo baadaye”, alisema Mhe. Maalim.

Mhe. Maalim aliongeza kuwa, anaona fahari kubwa kama mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kuwepo kwenye uzinduzi huo ikiwa ni katika kuhamasisha Diplomasia ya Michezo ambayo kwa sasa ni muhimu katika kukuza urafiki, undugu, ushirikiano na uhusiano mzuri kati ya mtu mmoja mmoja kwa maana ya wachezaji na pia kwa nchi na nchi kama ilivyo kwa vijana hao ambao wametoka mataifa ya nje 11.

“Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa sasa inahamasisha Diplomasia ya Michezo ikiwa ni njia mojawapo za kuimarisha mahusiano na mataifa mengine kupitia michezo. Wizara inaunga mkono jitihada mbalimbali zinazofanywa na Wizara yenye dhamana ya michezo na Taasisi nyingine zote za michezo na kitendo cha mimi kuwepo hapa leo ni katika kuongeza nguvu kwenye jitihada hizo ili nchi yetu iendelee kimichezo,” alisisitiza Mhe. Maalim.

Awali akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Airtel-Tanzania, Bw. Sunil Colaso aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuweka mazingira mazuri ya kuwekeza kwenye michezo.

Nae Mwenyekiti wa Kamati ya Vijana ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Bw. Ayoub Nyenzi ambaye alimwakilisha Rais wa Shirikisho hilo,  alimshukuru Naibu Waziri kwa kuzindua Kambi hiyo ambayo ni ya pili kwa Tanzania baada ya ile ya mwaka 2011. Aidha, aliwaasa vijana hao kuzingatia mafunzo watakayopewa kwani ndio msingi wa maisha yao hapo baadaye.

Kwa upande wao Walimu wa vijana hao kutoka Manchester United Bw. Andrew Stokes na Bw. Neil Scott walisema kwao ni upendeleo wa pekee kufundisha vijana hao na kwamba Manchester United imedhamiria kushirikiana na Tanzania katika masuala ya kuendeleza michezo.

Kambi hiyo ambayo ipo kwa siku tano itahusisha vijana 74 kutoka mataifa 12 ya Afrika ikiwemo Tanzania. Jina la nchi na idadi ya vijana kwenye mabano ni kama ifuatavyo; Tanzania (19), Niger (17), Chad (4), Kenya (4), Malawi (4), Shelisheli (2) na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (6). Nchi nyingine ni Burkina Faso (4), Congo Brazaville (2), Gabon (4), Madagascar (2) na Siera Leone (6).

-Mwisho-