Saturday, September 7, 2013

Waziri Membe aelezea kuhusu Mkutano wa ICGLR


Mhe. Bernard K. Membe (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa jana alikutana na waandishi wa habari katika ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje mjini Dar es Salaam.  Katika mazungumzo yake, Mhe. Waziri Membe alielezea yaliyojiri katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi wa Sekretarieti ya Maziwa Makuu (ICGLR) uliofanyika mjini Kampala, Uganda hivi karibuni.  

Waandishi wa habari wakimsikiliza Mhe. Waziri Membe wakati wa mazungumzo nao jana.

Mhe. Waziri Membe akiendelea kuongea na waandishi, wakati Balozi Vincent Kibwana, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa akisikiliza kwa makini.  

Mhe. Waziri Membe akiongea na waandishi wa habari.


Picha zote na Tagie Daisy Mwakawago 



Waziri Membe aelezea kuhusu Mkutano wa ICGLR
Na Zainabu Abdallah
Wakuu wa Nchi wa Sekretarieti ya Maziwa Makuu (ICGLR) wamemaliza kikao chao kilichofanyika Jijini Kampala, Uganda 05/9/2013. Kikao hicho  kilijadili hali ya kuzorota kwa amani Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) kutokana na mashambulizi yanayoendelea kufanywa na M23 katika mji wa Goma.
Akioengea na Waandishi wa Habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam 06 Septemba, 2013, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Mheshimiwa  Bernard Membe (Mb) alisema kuwa Wakuu wa Nchi walifikia maamuzi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kulaani vikali mashambulizi  ya M23 katika mji wa Goma yaliyosababibisha vifo na majeruhi kwa raia na askari wa kulinda amani.
 Aidha, Wakuu wa Nchi na Serikali walitoa pole kwa Umoja wa Mataifa na Tanzania kutokana na kifo cha Meja  Khatibu Mshindo, mwanajeshi wa Tanzania aliyeuwawa katika shambulio lililofanywa na Kikundi cha Waasi cha M23. Katika shambulio hilo pia wanajeshi watano walijeruhiwa na hali zao zinaendelea vizuri.
Vile vile, Mhe. Membe alisema kuwa ujumbe wa Umoja wa Mataifa ukiongozwa na Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa Nchi za Maziwa Makuu, Mhe. Marry Robinson upo Goma kuangalia hali ya usalama
Katika hatua nyingine, Wakuu wa Nchi waliagiza Serikali ya DRC na M23 kufanya mazungumzo ili kumaliza mgogoro huo kwa amani na kutoa siku 17 kukamilisha zoezi hilo.   Siku tatu kati ya hizo ni kwa ajili ya maandalizi na siku kumi na nne ni kwa ajili ya majadiliano na makubaliano ya kufikia muafaka wa kumaliza mgogoro huo.
Kando ya mkutano huo, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete alipata fursa ya kuongea na  Rais Paul Kagame wa Rwanda. Katika mazungumzo hayo, Viongozi hao waliazimia kudumisha na kukuza uhusiano wa kihistoria kati ya Tanzania na Rwanda.




No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.