Friday, March 24, 2017

Balozi Kairuki awasilisha Hati za Utambulisho

Balozi wa Tanzania nchini China, Mhe. Mberwa Kairuki akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Mhe. Xi Jinping wakati wa hafla ya kuwasilisha Hati za Utambulisho iliyofanyika  Ikulu kwenye Ukumbi wa Great hall of the people siku ya Ijumaa tarehe 17 Machi 2017.
Balozi Kairuki (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa China, Mhe. Xi Jinping
Balozi wa Tanzania katika Jamhuri ya Watu wa China Mhe. Mbelwa Kairuki amewasilisha rasmi Hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Mhe. Xi Jinping tarehe 17 Machi 2017. 

Hafla hiyo iliyofanyika katika Ikulu ya China (Great Hall of the People) ilihudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa China Mhe. Wang Yi na maafisa waandamizi wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China. 

Katika mazungumzo mafupi baada ya kuwasilisha hati, China na Tanzania zimekubaliana kukuza zaidi mahusiano ya kiuchumi kupitia mpango maalum wa China wa kuhamishia viwanda vyake nje ya China (Production Capacity Cooperation Programme) pamoja na programu ya kukuza ushirikiano wa biashara na ujenzi wa miundombinu ijulikanayo kama Maritime Silk Road initiative. 

Aidha, Tanzania imeihakikishia China kuendelea kuunga mkono sera yake ya ONE CHINA POLICY sambamba na kuunga mkono mtazamo wa China kuhusu mgogoro wa Bahari ya Kusini mwa China.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.