Sunday, March 15, 2020

KAMATI YA BUNGE YA NJE, ULINZI NA USALAMA YATEMBELEA OFISI ZA WIZARA YA MAMBO YA NJE ZILIZOPO MTUMBA JIJINI DODOMA

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU), Mhe. Victor Mwambalaswa (Mb.) akizungumza wakati wa ziara ya Wajumbe wa Kamati hiyo walipotembelea Jengo la Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki lililopo Mtumba jijini Dodoma tarehe 15 Machi 2020. Lengo la ziara hiyo lilikuwa ni kukagua miradi inayosimamiwa na Kamati hiyo
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb.) akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama walipofanya ziara ya kikazi kwenye Jengo la Wizara lililopo Mtumba jijini Dodoma tarehe 15 Machi 2020
Mhe. Prof. Kabudi akifafanua jambo kwa Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya NUU
Wajumbe wa Kamati ya NUU akiwemo Mhe. Vuai Nahodha (kulia) wakimsikiliza Prof. Kabudi (hayupo pichani). Kushoto ni Mhe. Augustino Masele.
Wajumbe wengine wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama Mhe. Bonnah Kaluwa na Sophia Mwakagenda nao wakimsikiliza Mhe. Prof. Kabudi ambaye hayupo pichani
Mhe. Masoud Abdalla Salim, Mjumbe wa Kamati akichangia hoja wakati wa ziara yao kwenye Ofisi za Wizara zilizopo Mtumba, Dodoma
Mhe. Prof. Kabudi akimsikiliza Mjumbe wa Kamati, Mhe. Silafu Maufi alipotoa ushauri kwa Wizara kuhusu kuboresha maeneo kadhaa ya Jengo walilotembelea
Mhe. Almas Maige, Mjumbe wa Kamati naye akizungumza. Kulia ni Mhe. Ruth Mollel na Mhe. Mhandisi Gerson Lwenge (kushoto)
Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Issa Ng'imba akitoa taarifa kwa Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama (hawapo pichani) kuhusu ujenzi wa Jengo la Wizara lililopo Mtumba
Sehemu ya Wakuuu wa Idara na Vitengo wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wakimsikiliza Bw. Ng'imba ambaye hayupo pichani
Msimamizi wa Miradi ya Majengo ya Wizara, Mhandisi John Kiswaga  akijibu hoja kadhaa zilizowasilishwa na Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama wakati wa ziara yao Wizarani
Mhe. Mwakagenda akizungumza wakati wa ziara yao 
Mhe. Prof. Kabudi akiwaeleza jambo Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama walipotembelea chumba cha ofisi yake wakati wa ziara yao kwenye jengo la Wizara lililopo Mtumba jijini Dodoma


Mhe. Prof. Kabudi akimwonesha Mhe. Mwambalaswa mandhari ya nje ya jengo akiwa ndani ya ofisi yake
Mhe. Prof. Kabudi akiwaonesha Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama chumba cha wageni mashuhuri kilichopo kwenye Jengo la Wizara lililopo Mtumba

Wajumbe wa Kamati wakipita pembeni mwa eneo la kiwanja cha Wizara kama inavyoonekana
Mhe. Prof. Kabudi akiwaonesha eneo la nje la Jengo la Wizara
Mhe. Mwambalaswa akimweleza jambo Mhe. Prof. Kabudi
Jengo la Wizara kama linavyoonekana
Mhe. Prof. Kabudi akiwaongoza Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama kurejea ndani mara baada ya kutembelea eneo la nje la Jengo la Wizara lililopo Mtumba jijini Dodoma
Mhe. Prof. Kabudi akijadiliana jambo na  Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama mara baada ya kukamilisha ziara yao.
Mhe. Prof. Kabudi akiagana na Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama mara baada ya kukamilisha ziara yao kwenye Jengo la Wizara lililopo Mtumba jijini Dodoma
====================================================


WAJUMBE WA KAMATI YA BUNGE YA  NJE, ULINZI NA USALAMA WATEMBELEA JENGO LA WIZARA LILILOPO MTUMBA

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama (NUU) wakiongozwa na Mhe. Victor Mwambalaswa (Mb.), Mwenyekiti wa Kamati hiyo wamefanya ziara ya kikazi kwenye Jengo la Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki lililopo kwenye Mji wa Serikali wa Mtumba jijini Dodoma leo tarehe 15 Machi 2020.

Wajumbe hao ambao wapo kwenye program ya kukagua miradi iliyopo kwenye Wizara zinazosimamiwa na Kamati hiyo, wamepokelewa na mwenyeji wao Mhe. Prof. Palamagamba John Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki mara baada ya kuwasili.

Wakizungumza wakati wa ziara hiyo, baadhi ya Wajumbe hao, wameipongeza Wizara kwa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo kwa wakati ikiwa ni utekelezaji wa azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kuhamia Dodoma. Pia wameishauri Wizara kuendelea kuboresha maeneo kadhaa katika jengo hilo ikiwa ni pamoja na kuweka uzio kuzunguka jengo hilo na kukamilisha mfumo wa TEHAMA kwa ajili ya kuboresha mawasiliano. Vilevile, Wajumbe wa Kamati hiyo wameitaka Wizara kuzingatia kanuni za ujenzi wa majengo ya Ofisi za Mambo ya Nje pale Wizara itakapoanza ujenzi wa jengo lake la kudumu katika siku zijazo.

Kwa upande wake, Mhe. Prof. Kabudi aliahidi kutekeleza ushauri uliotolewa na Wajumbe wa Kamati hiyo na kuwahakikishia kuwa, mapungufu kadhaa yaliyopo yatafanyiwa kazi haraka iwezekanavyo.

Aidha, akitoa taarifa fupi kuhusu ugonjwa wa Corona kwa Wajumbe wa Kamati hiyo, Mhe. Prof. Kabudi alisema kuwa, Serikali ya Tanzania imechukua hatua madhubuti kwa ajili ya kukabiliana na ugonjwa huo endapo utaingia nchini. Hatua hizo ni pamoja na mikutano ya kikanda kuanza kufanyika kwa njia ya video ukiwemo Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) utakaofanyika nchini kuanzia tarehe 16 hadi 18 Machi 2020.

Pia Kamati ya Kitaifa inayojumuisha Sekta mbalimbali imeundwa kwa ajili ya kuandaa mikakati mbalimbali ya kukabiliana na ugonjwa huo. Kadhalika vifaa, wataalam na maeneo ya karantini tayari yametengwa kwa ajili ya kukabiliana na ugonjwa huo.

“Tanzania inaendelea kuchukua tahadhari mbalimbali kuhusu ugonjwa wa Corona ambao hadi sasa haujaingia nchini. Hatua hizo ni pamoja na kuandaa mikutano ya kikanda ambayo itafanyika kwa njia ya video. Katika kutekeleza hilo, Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa SADC unaoanza tarehe 16 Machi mwaka huu utafanyika kwa njia ya video na utafuata taratibu zote za mikutano ya kikanda wakati wa ufunguzi” alisisitiza Prof. Kabudi.

Jengo la Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambalo lipo Mtumba jijini Dodoma lina ukubwa wa Mita za Mraba 1,002 na vyumba 17 vyenye matumizi mbalimbali zikiwemo Ofisi. Jengo hilo lilianza kujengwa mwezi Desemba 2018 na kukamilika mwezi Machi 2019.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.