Monday, March 16, 2020

TEKNOLOJIA YAWEZESHA MKUTANO WA MAAFISA WAANDAMIZI WA SADC KUEPUKA CORONA ( COVID-19)

Mkutano wa Maafisa Waandamizi ambao ni mkutano wa awali wa maandalizi ya Baraza la Mawaziri la nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) unaotarajia kufanyika tarehe 18 Machi 2020 umefunguliwa rasmi katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini  Dar es Salaam.

Akifungua mkutano huu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafisa Waandamizi wa SADC, Balozi Kanali Wilbert Ibuge amewashukuru wajumbe wote kutoka nchi wanachama pamoja na wataalamu wa TEHAMA kwa jitihata walizoonesha kuhakikisha mkutano huu kwa mara ya kwanza unafanyika kwa mfumo wa Video. “ Hii ni uthibitisho siyo tu wa namna ambavyo Teknolojia ya Habari na Mawasilisno imebadilisha na itaendelea kutubadilisha namna tunavyowasiliana bali pia ambavyo matishio ya majanga ya kidunia kama ugonjwa wa Virusi vya CORONA (COVID 19) yanavyotulazimisha kutafuta mbinu mbadala za kufanya mambo yetu kikanda na kidunia pamoja na kuendelea kuimarisha ushirikiano bila kuonana ana kwa ana” alisema Balozi Ibuge
Mkutano huu unahudhuriwa na Maafisa Waandamizi kutoka nchi 16 za Jumuiya ya Maendeleo kusini mwa Afrika (SADC) wenye dhamana ya masuala ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Fedha, Uchumi, Mipango pamoja na Viwanda na Biashara.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huu unaongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Masharikia na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafisa Waandamizi wa SADC, Balozi Kanali Wilbert Ibuge ambaye ameambatana na maafisa wengine waandamizi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Fedha na Mipango Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Wizara ya Viwanda na Biashara Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Maafisa wengine waandamizi walioshiriki ni pamoja na maafisa kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya Mambo ya Ndani. Vilevile mkutano huu umehudhuriwa na baadhi ya Mabalozi wa Tanzania wanaowakilisha katika nchi za SADC ambao ni pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Jamhuri ya Afrika Kusini.

Mkutano huu utajadili ajenda chache za muhimu kwa wakati huu ambazo ni: Taarifa ya Maandalizi ya Dira ya SADC ya 2050; Mpango Mkakati wa Maendeleo wa SADC 2020-2030; Maadhimisho ya miaka 40 ya SADC tangu kuanzishwa kwake mwaka 1980; Utekelezaji wa maazimio ya vikao vilivyopita; Hali ya michango na kifedha kwa ujumla ya SADC; na Kupokea taarifa ya ukaguzi wa shughuli mbalimbali za Sekretarieti SADC.


Awali mkutano katika ngazi ya Maafisa Waandamizi ulipangwa kufanyika kuanzia tarehe 12 hadi 14 Machi 2020 na kufuatiwa na Mkutano wa Baraza la Mawaziri tarehe 17 na 18 Machi 2020. Hata hivyo, kufuatia ushauri na mapendekezo yaliyotolewa na Mawaziri wa Afya kutoka Nchi Wanachama wa SADC walipokutana kwa dharura tarehe 9 Machi, 2020. Mkutano huo ulijadili na kupendekeza kwa Nchi Wanachama namna ya kuzuia maambukizi ya mlipuko wa ugonjwa hatari wa virusi vya Corona (COVID 19) unaosambaa kwa kasi na kuleta athari kubwa duniani tangu kubainika kwakwe mwezi Desemba.

===================================================================


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafisa Waandamizi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Balozi Kanali Wilbert Ibuge, akifungua mkutano wa Maafisa Waandamizi ambao ni mkutano wa awali wa maandalizi ya Mkutano wa Baraza la Mawaziri wa SADC utakaofanyika Machi 18, 2020, katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, Tanzania.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafisa Waandamizi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Balozi Kanali Wilbert Ibuge, akifungua mkutano wa Maafisa Waandamizi wa SADC unaofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, Tanzania. Ufunguzi wa Mkutano huo umefanyika kwa njia ya video kuepuka maambukizi ya Virusi vya ugonjwa CORONA (COVID 19)

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa Kamati ya Maafisa Waandamizi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Balozi Kanali Wilbert Ibuge, akitoa hotuba ya ufunguzi ambapo alitumua nafasi hii kueleza agenda zitakazojadiliwa na wajumbe wa mkutano kutoka nchi wanachama. Pia aliishukuru Sekretariet ya SADC,wajumbe kutoka nchi wanachama, wataalamu wa TEHAMA kutoka nchi za SADC pamoja, na wajumbe wengine kwa ushirikiano wao uliowezesha kufanyika kwa mkutano huo kwa njia ya video. Kulia ni Katibu Mtendaji wa Sekretariet ya SADC, Dr. Stergomena Tax.

Maafisa Waandamizi wa nchi za SADC  wakifuatilia ufunguzi wa mkutano huo uliokuwa ukiendelea kupitia mfumo wa video, unaofanyika katika kituo cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam, Tanzania 

Maafisa Waandamizi wa nchi za SADC  wakifuatilia hafla ya ufunguzi wa mkutano kutokea nchini Tanzania kupitia mfumo wa video  

Mkutano ukiendelea.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.