Saturday, March 23, 2024

WAHIMIZA UMOJA KUMALIZA CHANGAMOTO ZA KIUSALAMA MASHARIKI MWA DRC


Nchi wanachama za Jumuiya ya Maendeleo Kusini Mwa Afrika (SADC) zimekumbushwa kuwa ni jukumu lao kufanya kazi kwa pamoja ili kumaliza changamoto za kiusalama zinazozikabili Jimbo la Cabo Delgado nchini Msumbiji na Mashariki mwa Jamhuri ya Kidiplomasia ya Congo (DRC).

 

Ukumbusho huo umetolewa na Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC ambaye pia ni Rais wa Zambia, Mhe. Hakainde Hichelema wakati anafungua Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Utatu wa Asasi mbili za Jumuiya ya SADC uliohitimishwa jijini Lusaka, Zambia Machi 23, 2024.

 

Katika Mkutano huo ambapo Tanzania iliwakilishwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.  Philip Isdor Mpango pamoja na mambo mengine, ulilenga kutathimini hali ya usalama katika Kanda ya SADC. Ilielezwa kuwa hali ya usalama Mashariki mwa DRC bado hairidhishi, hivyo umetolewa wito kwa nchi wanachama na washirika wa maendeleo kuchangia rasilimali ili vikosi vya kulinda amani vilivyopo huko na vingine vitakavyopelekwa, viweze kutimiza majukumu yake ipasavyo.

 

Ilibainishwa kuwa suala la kutafuta amani katika Kanda ni suala la kimkataba wa jumuiya hiyo na Itifaki ya Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama, hivyo ni wajibu kwa mataifa hayo kuungana pamoja kukabiliana na changamoto za kiusalama.

 

Wachambuzi wa mambo wamesema kuwa mahudhurio mazuri ya viongozi katika ngazi ya Rais, Makamu wa Rais na Mawaziri Wakuu katika mkutano huo yanadhihirisha kuwa nchi za SADC zimedhamiria kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa changamoto ya usalama nchini Msumbiji na DRC.

 

Marais walioshiriki Mkutano huo ni Mhe. Hakainde Hichelema wa Zambia, Mhe. Emmerson Mnangwa wa Zimbabwe: Mhe. Félix Tshisekedi was DRC; Mhe. Lazarus Chakwera wa Malawi; Mhe. Filipe Nyusi wa Msumbiji na Mhe. João Lourenço wa Angola. Nchi za Tanzania na Namibia ziliwakilishwa na Makamu wa Rais, Lesotho, Waziri Mkuu na Afrika Kusini na Botswana ziliwakilishwa na Mawaziri wa Ulinzi

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.  Philip Isdor Mpango akisoma makabrasha ya Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Utatu wa Asasi mbili za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Lusaka, Zambaia Machi 23, 2024. Kushoto ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashaiki, Mhe. January Makamba (Mb)

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.  Philip Isdor Mpango, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (kulia) na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashaiki, Mhe. January Makamba wakiimba nyimbo za Taifa wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Utatu wa Asasi mbili za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Lusaka, Zambaia Machi 23, 2024.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.