Sunday, March 10, 2024

MAWAZIRI WA SADC WAWASILISHA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA


Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamewasilisha salamu za rambirambi kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia kifo cha Rais wa pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati  Ali Hassan Mwinyi katika  Baraza la Mawaziri la Jumuiya hiyo lililoanza leo tarehe 10 Machi 2024  jijini Luanda, Angola  

Wakati wa ufunguzi wa Baraza hilo, Waziri wa Mambo Nje wa Angola na Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa SADC, Mhe. Balozi Tete António pamoja na Mawaziri wengine wa nchi za SADC walitoa salamu hizo na kusifu uongozi mahiri na mchango wa Hayati Mzee Ali Hassan Mwinyi katika kuchangia maendeleo ya Tanzania na Kanda ya SADC hususan pindi alipokuwa Mwenyekiti wa iliyokuwa Jukwaa la Uratibu wa masuala ya nchi za Kusini mwa Afrika (SADCC) mwaka 1989 - 1990 na pia aliongoza mchakato wa kubadili Jukwaa hilo kuwa SADC. 

Kwa muda wa siku mbili  Baraza hili litajikita kupitia, kujadili na kuridhia Bajeti ya SADC kwa mwaka wa fedha wa 2024/25. Vile vile, Baraza litajadili hatua iliyofikiwa katika kugharamia utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Maendeleo wa SADC wa 2020–2030, Taarifa ya Kamati ya Rasilimali Watu na Utawala na hatua iliyofikiwa katika kutafsiri nyaraka muhimu za SADC kwa lugha ya Kiswahili.

Ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Baraza la Mawaziri la SADC umeongozwa na Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.)   ambaye ameambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Ikulu, Zanzibar, Mhe. Ali Suleiman Ameir (Mb.) na viongozi wengine waandamizi wa Serikali.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akiongoza ujumbe wa Tanzania katika Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) linaloendelea jijini Luanda, Angola tarehe 10 – 11 Machi, 2024.

Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa Kikanda katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrka Mashariki, Bi. Talha Waziri akiteta jambo na Balozi Mbarouk wakati wa  Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) linaloendelea  jijini Luanda, Angola tarehe 10 – 11 Machi, 2024.
Waziri wa Mambo Nje wa Angola na Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa SADC, Mhe. Balozi Tete António akifungua Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) linaloendelea  jijini Luanda, Angola tarehe 10 – 11 Machi, 2024

Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, Bw. Elias Magosi akihutubia wakati wa ufunguzi wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) linaloendelea jijini Luanda, Angola tarehe 10 – 11 Machi, 2024

Meza kuu ikiongoza  Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) linaloendele jijini Luanda, Angola tarehe 10 – 11 Machi, 2024

Picha ya pamoja ya wakati wa hafla ya ufunguzi wa Baraza la Mawaziri wa SADC



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.