Friday, April 5, 2019

Waziri Kabudi aongoza kumbukumbu za Wataalam wa Kichina waliokufa wakati wa ujenzi wa Reli ya TAZARA

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Palamagamba John Kabudi (Mb.),  akiweka shada la Ua kwenye mnara uliopo kwenye makaburi ya wataalam 70 kutoka China waliokufa wakati wa ujenzi wa Reli ya Tazara, wakati wa maadhimisho ya utamaduni wa Wachina na kuwakumbuka wataalam hao yaliyofanyika kwenye eneo la makaburi walikozikwa wataalam hao lililopo Gongo la mboto, Dar es Salaam. Maadhimisho hayo yalihudhuriwa pia na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari, Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Hassan Abbas na Kurugenzi wa Idara ya Asia na Australasia wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Bw. Caesar C. Waitara na viongozi mbalimbali wa serikali
 Prof. Palamagamba Kabudi pamoja na Viongozi mbalimbali kutoka Serikalini wakitoa heshima zao kwa kuinamisha vichwa kama ishara ya kuwakumbuka wataalam hao kutoka China. 
 
 Prof. Palamagamba pamoja na Mhe. Wang Ke wakiweka maua katika moja ya kaburi la wataalam hao.
 Bw. Caesar Waitara akiweka Ua katika moja ya kaburi la wataalam hao.
 Prof. Palamagamba John Kabudi(Mb.), akihutubia katika hafla hiyo mara baada ya kumaliza zoezi la kuweka maua kwenye makaburi ya wataalam wa kichina waliokufa wakati wa ujenzi wa reli ya Tazara. Katika Hotuba hiyo waziri Kabudi aliendelea kuusifu ushirikiano wa Tanzania na China katika sekta mbalimbali ambapo  Ujenzi wa reli ya Tazara ulipelekea kuanzishwa kwa  viwanda mbalimbali.
Aidha,  alieleza kuwa kutoka na Ushirikiano ulipo Tanzania inatarajia kufungua ubalozi mdogo katika mji wa Guangzhou pamoja na kuanzisha Safari ya Ndege za Shirika la Tanzania (ATCL) kuelekea moja kwa moja Guanghzou ambapo utapelekea kuongeza watalii kutoka China kuja kutembelea vivutio vilivyopo nchini Tanzania.
Balozi Wang Ke naye akitoa hotuba yake wakati wa hafla hiyo.

 Sehemu ya wageni waalikwa wakisikiliza kwa makini hotuba zilizo kuwa zikiendelea kutolewa na Prof. Palamagamba John Kabudi na Balozi Wang Ke (hawapo pichani) 
 Prof. Palamagamba John Kabudi akiweka saini kwenye kitabu cha kumbukumbu ya vifo vya wataalam hao.

 Prof. Palamagamba John Kabudi akizungumza na waandishi wa Habari mara baada ya kumaliza hafla hiyo.
Prof. Palamagamba John Kabudi pamoja na Balozi Wang Ke wakiwa katika picha ya pamoja na wageni engine waliohudhuria tulip hilo.

Thursday, April 4, 2019

Nafasi ya kazi katika Jumuiya ya Madola


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

NAFASI YA AJIRA KATIKA JUMUIYA YA MADOLA, LONDON, UINGEREZA.

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, inawahamasisha Watanzania wenye sifa kuomba nafasi ya ajira katika Jumuiya ya Madola, London, Uingereza.

Nafasi hiyo ni Afisa Rasilimali Watu Msaidizi atakayefanya kazi katika kitengo cha Rasilimali Watu na Usimamizi wa Miundombinu. Taarifa zote muhimu kuhusu fursa hiyo ya ajira zinapatikana kwa kupitia tovuti http://thecommonwealth.org.jobs.

Kwa kuzingatia sera ya Jumuiya ya Madola ya usawa wa kijinsia, Sekretarieti ya taasisi hiyo inawahimiza wanawake wengi zaidi wenye vigezo kuomba nafasi hizo. Mchakato wa kumpitisha mtaradhia wa nafasi hiyo utazingatia uwiano wa kikanda hususan kwa nafasi za maafisa waandamizi.

Mwisho wa kutuma maombi kwa nafasi hizo ni Ijumaa tarehe 12 Aprili, 2019.

 Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma
4 Aprili, 2019.

Wednesday, April 3, 2019

Jaji Mstaafu Mark Bomani awataka Watanzania Kuchangia fursa katika Sekta ya Madini

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba John Kabudi (Mb.) akimsikiliza kwa makini mgeni wake Jaji Mstaafu Mark Bomani alipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba John Kabudi (kushoto) akiwa na mgeni wake Jaji Mstaafu Mark Bomani alipomtembelea ofisini kwake jijini Dar es salaam.

==========================
Mwanasheria mkuu wa kwanza Tanzania Jaji Mstaafu Mark Bomani, amewataka watanzania kuchangamkia fursa ya mabadiliko ya sheria katika sekta za maliasili na madini yaliyofanyika hivi karibuni,kutokana na sheria hizo kuweka mazingira ya usawa (win - win situation)tofauti na sheria zilizokuwepo awali kutoa kipaumbele kwa wawekezaji kutoka Nje ya nchi.

Jji Mstaafu Mark Bomani ameyasema hayo alipomtembelea ofisini kwake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba John Kabudi (Mb.) kwa lengo la kubadilishana mawazo kuhusu sekta ya madini nchini na kuongeza kuwa Tanzania ina utajiri mkubwa wa madini unaotosha kuendesha Nchi  ukiachilia mbali maliasili nyingine zilizopo tatizo ni kuwa madini hayo hayakulinufaisha Taifa.

Mabadiliko ya sheria waliyoyafanya yatasaidia sana,sasa ni jukumu letu sisi Watanzania kuichangamkia fursa hiyo na tusisubiri kulalamika kama ilivyo kawaida yetu,tfanye kazi kwa bidii maana utajiri huu wa madini tuutumie na kujiletea maendeleo binafsi na yanchi kwa ujumla kwa kuwa sasa sheria hizi mpya zimeweka uwanja sawa”

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba Kabudi mbali na kumshukuru Jaji Mstaafu Mark Bomani kumtembelea ofisini kwake ameongeza kuwa mabadiliko yaliyofanyika katika sheria za madini yametokana kwa kiasi kikubwa na ripoti ya tume iliyoundwa kuchunguza sekta ya madini ikiongozwa na Jaji Mstaafu Mark Bomani.

“Haya yoote tuliyoyabaini na kuyaeleza kama upungufu yamo kwenye ripoti ya Bomani ingawa kuna mengine tuliyoyaongeza kama vile mrahaba ulio chini,kutolipa kodi na mengine mengi na kwakuwa Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli ameutangaza mwaka 2019 kuwa mwaka wa uwekezaji,Mzee Bomani amekuja ili tubadilishane mawazo tuone namna ya kuuboresha mwaka huu wa uwekezaji”

Ameongeza kuwa wamezungumzia namna ya kuweka mikakati ya kuwavutia wawekezaji wenye tija kuja nchini kuwekeza ili Taifa liweze kunufaika na madini kupitia kodi,ajira kwa vijana na kwamba ujio wa Jaji Mstaafu Mark Bomani ofisini kwake umemjengea ari na nia ya kuonana na viongozi wengine waliolitumikia Taifa kwa tija ili aweze kupata maoni yao ya namna ya kuendesha shughuli za serikali katika wizara aliyopangiwa kazi na Rais Dkt John Pombe Magufuli.


Ujumbe wa Libya wakutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje Prof. Palamagamba Kabudi

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof Palamagamba John Kabudi akiwa katika mazungumzo na Kiongozi wa Ujumbe kutoka Libya Mhe. Jamal El Barak


=======================================

Tanzania na Serikali ya Umoja ya Libya, zimekubaliana kuingia katika mazungumzo ya kina yenye lengo la kupitia miradi yote na uwekezaji,  iliyokuwa ikifanywa na Serikali ya Libya hapa nchini kabla ya machafuko nchini humo na pia kuangalia maeneo mapya ya uwekezaji ambayo Libya imeonesha nia ya kutaka kuwekeza chini ya Kamati ya pamoja baina ya nchi hizo mbili.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba John Kabudi ameyasema hayo jijini Dar es salaam wakati wa mazungumzo na Kiongozi wa Ujumbe kutoka Libya na kuongeza kuwa baada ya hali ya Libya kutengemaa na Amani kuongezeka wamekubaliana kuingia katika uwekezaji.

“Nimemueleza mgeni wangu kuwa mwaka huu wa 2019 Tanzania tumeutangaza kuwa ni mwaka wa uwekezaji na yeye ameonesha nia ya nchi yake na makampuni ya Libya kutaka kuja kuwekeza hapa nchini,tumejadili pia jinsi ya kufufua kamati ya pamoja kati ya Libya na Tanzania kwakuwa mkutano wa mwisho ulifanyika mwaka 2000 baada ya Kamati hiyo kukutana sasa tutajadili miradi mbalimbali ambayo Libya imewekeza,mitaji iliyoiwekeza lakini pia tutaangalia maeneo mapya wanayopendekeza kuwekeza”

Aidha Profesa Palamagamba John Kabudi amefafanua kuwa lengo jipya katika sheria za uwekezaji Tazania ni kuhakikishia Nchi inakuwa na mfumo wa sheria na uwekezaji ambao kila upande unapata tofauti na mfumo wa zamani ambao wawekezaji walikuwa wakinufaika na nchi inanyonywa.

Kwa upande wake Kiongozi wa Ujumbe kutoka Libya Mhe. Jamal El Barak amesema wamekuja dhumuni la ujumbe wao kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli ni kumjulisha kuwa Serikali ya Umoja wa Libya iko tayari kufufua na kuendeleza mahusiano ya kidiplomasia baina ya nchi hizo baada ya hali ya Amani kutengemaa nchini Libya kutokana na mahusiano ya Tanzania na Libya kuwa ya kihistoria.

Mbali na hayo Mhe Jamal El Barak ameongeza kuwa Libya iko tayari kushirikiana na Tanzania katika sekta mbalimbali za uwekezaji kwa kuwa wanatambaua mazingira ya uwekezaji Tanzania ni mazuri hasa baada ya kuhakikishiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki kuwa mazingira ya uwekezaji yameboreshwa.

Si mara yetu ya kwanza kuwekeza hapa nchini,kabala ya machafuko nchini mwetu tulikuwa tumewekeza katika sekta mbalimbali na sasa tutaangalia maeneo mapya ya uwekezaji”

Thursday, March 28, 2019

TANGAZO LA MAFUNZO YA KILIMO NCHINI ISRAEL


28 Machi 2019

TAARIFA KWA UMMA

TANGAZO LA MAFUNZO YA KILIMO NCHINI ISRAEL

UTANGULIZI

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inatangaza ufadhili wa mafunzo katika Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi nchini Israel. Mafunzo hayo ni ya miezi 11 kuanzia mwezi Septemba, 2019 ikiwa ni utekelezaji wa ahadi iliyotolewa na Serikali ya Israel kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mafunzo hayo yatahusisha pia vitendo (field attachment) kwenye mashamba makubwa ya mazao mbali mbali yakiwemo ya matunda, mbogamboga, ufugaji, uvuvi na mazao mengine ya biashara kwa ujira maalum.

SIFA NA VIGEZO VYA MWOMBAJI

  1. Awe ni raia wa Tanzania mwenye umri wa kati ya miaka 20-35 pamoja na cheti cha kuzaliwa na Kitambulisho cha Uraia.  
  2.  Awe amehitimu mafunzo ya Kilimo katika ngazi ya shahada ya Chuo Kikuu,Stashahada au Astashahada ya Vyuo vya kilimo vinavyotambulika nchini.
  3.  Awe na afya njema.  
  4.  Awe na ujuzi wa kuandika na kuongea lugha ya Kiingereza.   
  5. Awe na uwezo wa kufanya kazi na watu wa tamaduni mbalimbali.  
  6.  Awe tayari kurejea nchini baada ya mafunzo yake.         

UTARATIBU WA KUFANYA MAOMBI

Maombi yote yatumwe kwa Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki yakiwa yameambatishwa na nakala za nyaraka zifuatazo:


     i.     Cheti cha kuzaliwa na uraia.  

   ii.      Vyeti vya kitaaluma.

 iii.        Hati ya Kusafiria au uthibitisho wa maombi ya pasipoti.

  iv.      Cheti cha kuthibitisha afya kutoka hospitali inayotambulika.

    v.    Barua ya kuonesha sababu za kushiriki mafunzo hayo  (Motivation letter) kwa lugha           ya Kiingereza.

  vi.        Wasifu (Curriculum Vitae).

 vii.        Picha mbili ndogo (Passport size).

viii.        Majina na anwani za wadhamini watatu wanaoishi nchini akiwemo mwalimu wa                 Chuo ulichohitimu.

Maombi yote yatumwe kupitia anwani ifuatayo: -

Katibu Mkuu,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Jengo la LAPF
Ghorofa ya 6,
Barabara ya Makole,
S.L.P   2933,
DODOMA.

Au kwa baruapepe; mafunzo.israel@nje.go.tz 

Mwisho wa kupokea maombi ni tarehe 12 Aprili, 2019

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma.

Fursa za ajira.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

NAFASI ZA AJIRA KATIKA SEKRETARIETI YA JUMUIYA YA MADOLA, LONDON, UINGEREZA.

Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, inawahimiza Watanzania wenye sifa kuomba nafasi za ajira katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, London, Uingereza.

Ajira hizo ni kama ifuatavyo:-

1.           Mshauri wa masuala ya Miundombinu na Usanifu wa Majengo        (Advisor Infrustructure and Architecture);
2.           Mkurugenzi wa masuala ya Uchumi, Vijana na Maendeleo      Endelevu (Senior Director, Economic, Youth and Sustainable         Development) na
3.           Mshauri  na Mkuu wa Kitengo cha Biashara na Ushindani (Advisor and Head,   Trade and Competitiveness section).

Watanzania wenye sifa wanahamasishwa kuomba nafasi hizo hasa ikizingatiwa kuwa, nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola ambazo hazina watumishi wengi katika ngazi ya maafisa waandamzi watapewa  kipaumbele ili kuimarisha uwiano wa kikanda katika nafasi hizo za ajira.
Kwa kuzingatia sera ya Jumuiya ya Madola ya usawa wa kijinsia, Sekretarieti ya taasisi  inawahimiza wanawake wengi zaidi wenye vigezo kuomba nafasi hizo.
Taarifa zote muhimu kuhusu fursa hizo za ajira zinapatikana kwa kupitia tovuti http://thecommonwealth.org.jobs.
Mwisho wa kutuma maombi kwa nafasi hizo ni tarehe 10 Aprili, 2019; tarehe 16 Aprili, 2019 na tarehe 17 Aprili, 2019, mtawalia.

 Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dodoma
28 Machi, 2019.



Balozi Seif Ali Iddi akutana na Rais wa Bunge la Cuba.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yake na Rais wa Bunge la Cuba, Mhe. Esteban Lazo Harnandez, mjini Havana, Cuba.
Mhe. Harnandez kulia akipokea zawadi ya mlango wa mji Mkongwe kutoka kwa Balozi Seif kama ishara ya kufunguliwa milango ya kuitembelea Zanzibar.

 Mhe. Harnandez akimtembeza Mhe. Balozi Iddi katika sehemu mbalimbali za jengo la Bunge ya Cuba lenye historia ya muda mrefu ambazo zimewekwa kama kumbukumbu ya taifa hilo.
Mhe. Balozi  Iddi wa pili kutoka kulia na ujumbe wake akifanya mazungumzo na uongozi wa Wizara ya Afya mjini Havana, Cuba.

=====================================


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, amelitembelea Bunge la Cuba na kukutana na kufanya mazungumzo na Rais wa bunge la nchi hiyo, Mhe. Esteban Lazo Harnandez.  
Katika mazungumzo baina ya viongozi hao wawili, Mhe. Harnandez ameahidi kuwa, Cuba itaendelea kudumisha ushirikiano wake wa kidiplomasia na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika kuendeleza wananchi wake licha ya taifa hilo la Caribean kupita katika mabadiliko ya kisiasa, uchumi na utamaduni. 
Mhe. Harnandez alieleza kuwa, kutokana na mabadiliko yaliyopo sasa katika mfumo wa dunia  katika masuala ya uchumi, siasa na utamaduni Jamhuri ya Cuba imelazimika kufanya mabadiliko ya katiba yake ili yalingane na mfumo huo wa dunia inayoizunguka.
Alifafanua kuwa, tayari Bunge la Cuba limeshafanya marekebisho katika katiba yake kutoa nafasi kwa wananchi wake kuwa na uwezo na uhuru wa kumiliki nyumba, ardhi pamoja na uwepo wa waziri mkuu atakayekuwa na mamlaka ya kusimamia utendaji wa serikali.
Mhe. Harnandez alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, kwamba katika vikao vya bunge hilo vinavyotarajiwa kuanza wiki ijayo baada ya kukamilika kwa uchaguzi wa wabunge, serikali ya nchi hiyo itakuwa imepiga hatua kubwa zaidi ya maendeleo kutokana na mabadiliko hayo.
Rais huyo wa Bunge la Cuba alisisitiza kwamba taasisi za kifedha zitalazimika kuzingatia ukusanyaji bora zaidi wa mapato katika maeneo yote ya uchumi ili kuimarisha ushiriki wa wananchi waliowengi katika mfumo huo.
Mhe. Harnandez alihitimisha kwa kumuhakikishia Balozi Seif kwamba,  uhusiano wa muda mrefu uliopo kati ya pande hizo mbili utaendelea kuimarishwa na kukuzwa katika muda wote.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Balozi Iddi alimpongeza Mhe. Harnandez kwa kuchaguliwa tena kuliongoza bunge hilo na kueleza kuwa, hatua hiyo inaonesha wazi ishara halisi ya kukubalika vyema na wananchi wa nchi hiyo kupitia viongozi wake.
Halikadhalika, Mhe. Balozi Iddi alieleza kuwa, kwa ujumla Zanzibar itaendelea kufuatilia mabadiliko ya Cuba na kuangalia endapo inaweza kuiga mabadiliko hayo ili kuimarisha uchumi na ustawi wa wananchi walio wengi.
Mhe. Balozi Iddi na ujumbe wake ulihitimisha ziara yake  nchini humo kwa kufanya mazungumzo na uongozi wa Wizara ya Afya ya Cuba uliokuwa ukiongozwa na Naibu Waziri, Mhe. Bibi Marcia Cobas,  katika makao makuu ya wizara hiyo yaliyopo Havana, Cuba.
Katika mazungumzo hayo ya ushirikiano wa kindugu, Balozi Iddi alisema matunda ya darasa la madaktari wazalendo waliosimamiwa na wataalamu pamoja na wahadhiri wa nchi ya Cuba yameanza kutoa matumaini.Alifafanua kuwa, kitendo cha Serikali ya Cuba kukubali kupunguza gharama kubwa ya kuwaendeleza madaktari hao wazalendo wapatao 15 katika shahada ya juu ya udaktari wa uzamili nchini humo kinaendelea kuleta faraja kubwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, pamoja na watu wake.
Alisema wakati Zanzibar ikiendelea kutekeleza sera ya afya ya kuwa na miuondombinu ya huduma za afya katika umbali usiozidi kilomita tano kundi hilo na madaktari linaloendelea kuongezeka kila mwaka litakuwa mkombozi wa utekelezaji wa sera hiyo muhimu.
Naye Kaibu Mkuu Wizara ya Afya Zanzibar, Bibi Asha Ali Abdullah, aliueleza uongozi huo wa Wizara ya Afya Cuba kwamba, hivi sasa Zanzibar  inapita katika kipindi cha kujiimarisha kwenye mapambano yake dhidi ya maradhi yasiyoambukiza.
Bibi Abdullah alisema maradhi yasiyoambukiza kama Kisukari pamoja na Shindikizo la Damu hivi sasa yamekuwa yakiathiri wananchi walio wengi na kuleta vifo vingi. Hata hivyo, jitihada zinachukuliwa ili kupunguza kasi  ya athari za maradhi hayo na kuimaliza kabisa kadhia hiyo kabisa.
Alibainisha kuwa, maradhi ya Malaria hivi  sasa yamepungua kutokana na kampeni kubwa iliyofanywa na serikali kwa kushirikiana na taasisi na mataifa wahisani katika kuangamiza vilui lui vya maradhi hayo.
Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Afya Zanzibar alimuhakikishia Naibu Waziri wa Afya wa Cuba kwamba ushauri wote walioupata katika ziara yao kwenye taasisi za Afya nchini Cuba likiwemo suala la upatikanaji wa dawa litazingatiwa na iwapo linaweza kuleta afueni ya gharama kwa Zanzibar litachukuliwa hatua mara moja.

Mhe. Dkt. Ussi atembelea Shamba Asilia nchini Cuba

Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili, Ufugaji na Uvuvi Zanzibar, Mhe. Dkt. Makame Ali Ussi,  ametembelea shamba la mimea asilia ( organic farm ) nchini Cuba, ambapo alipata maelezo juu ya uzalishaji wa mazao mbalimbali bila kutumia kemikali ambapo  mradi huo umeweza kuajiri wafanyakazi takribani 200 wakiwemo wazee na vijana. Wa pili kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Shamba hilo, wa pili kutoka kulia ni mkalimani Bi. Beatriz Soto na wa kwanza kushoto ni Afisa kilimo, Bw. Jose Antonio. 
 Mhe. Dkt. Ussi akiendelea kupata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa shamba hilo, Bw.Miguel Angel Lopez, wa kwanza kulia ni Afisa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Mohamed Kamal Mohamed, akisikiliza kwa makini maelezo yaliyokuwa yakitolewa. 
 Mhe. Dkt. Ussi akiendelea kupata maelezo juu ya kilimo cha miwa.
Juu na chini  Mhe. Dkt.  Ussi akipata maelezo namna ya utengenezaji wa mbolea isiyokuwa na kemikali yeyote.







Bw. Lopezi akimwonyesha Mhe.Dkt. Ussi teknolojia ya kifaa cha kupandia mazao.
 Mhe. Dkt. Ussi akizungumza na mmoja wa wakulima kwenye shamba hilo, aliyeonekana kufurahishwa na ujio wa Watanzania.
Sehemu ya mazao yanayopatikana kwenye shamba hilo.


Mhe. Balozi Seif ahudhuria maonesho ya kilimo Cuba.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Balozi Seif Ali Iddi,  na Naibu Waziri wa Kilimo, Maliasili, Ufugaji na Uvuvi Zanzibar, Mhe. Dkt. Makame Ali Ussi, wakikaribishwa na Naibu Waziri wa Kilimo wa Cuba Mhe. Jose Miguel Rodriquez De Armas, kwenye Maonesho ya Kimataifa ya 22 ya Kilimo yaliyofanyika jijini Havana, Cuba.  Mhe. Balozi Seif Ali Iddi alialikwa kama mgeni rasmi kwenye maonyesho hayo yaliyofanyika mnamo tarehe18 Machi, 2019. Maonesho hayo yalihudhuriwa na wananchi zaidi ya  3000. 

Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, akitizama kikundi cha wakulima waliokuwa wameandaliwa kutoa burudani kwenye maonyesho hayo.
Burudani zikiendelea kutolewa na vikundi mbalimbali vya wakulima.

Naibu Waziri wa Kilimo wa Cuba Mhe. Jose Miguel Rodriquez De Armas, akihutubia kwenye ufunguzi wa maonyesho hayo.
Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, akitembelea na kujionea mazao mbalimbali yanayolimwa nchini Cuba kwenye mabanda ya makampuni mbalimbali ya wafanyabiashara na yawakulima.



Balozi Seif Ali Iddi afanya mazungumzo na Waziri wa Kilimo wa Cuba.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, amekutana na kufanya mkutano na Naibu Waziri wa Kilimo wa Cuba, Mhe. Guastavo Rodriguez Roller. Mkutano huo ulijikita katika kuwajengea uwezo wakulima kwenye mazao ya kimkakati, ikiwemo kilimo cha pamba, miwa na maembe.


Mkutano ukiendelea kati ya ujumbe kutoka Tanzania ukiongozwa na Mhe. Balozi Seif Ali Iddi na ujumbe wa Cuba ukioongozwa na Mhe. Guastavo Rodriguez Roller.
Mhe. Balozi  Iddi, akimkabidhi Waziri wa Kilimo wa Cuba, Mhe. Guastavo Rodriguez Roller, zawadi ya mlango wa mji Mkongwe ikiashiria ukaribisho wa ushirikiano mpya wa sekta ya kilimo kati ya Tanzania na Cuba.

==================================


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, ameipongeza Serikali ya Cuba kupitia Wizara ya  Kilimo na Mifugo kwa mtazamo wake wa  kuanzisha ushirikiano mpana zaidi baina ya  Zanzibar na Tanzania katika sekta hiyo muhimu.

Akizungumza na Waziri wa Kilimo wa Jamhuri ya Cuba, Mhe. Guastavo Rodriguez Roller, katika makao makuu ya wizara hiyo mjini Havana, Balozi Seif  alieleza kuwa, Zanzibar na Cuba zimekuwa na ushirikiano ya karibu katika sekta za afya na elimu kwa kipindi kirefu sasa suala ambalo limeleta mafanikio makubwa.

Balozi Seif alibainisha kuwa, kwa kuwa maonyesho ni moja ya njia ya kubadilishana mawazo kitaaluma alimuomba Waziri wa Kilimo wa Cuba kutenga muda wa kushiriki katika Maonyesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Tanzania yanayofanyika  mwezi  Agosti wa kila mwaka nchini.

Kwa upande wake,  Mhe. Roller alibainisha kwamba, Cuba imebarikiwa kuwa na hekta milioni 10,000,000 ambazo zinatoa ajira kwa wakulima zaidi ya  5,000.Alifafanua kuwa, asilimia 70% ya ardhi hiyo ina maliasili, asilimia 3.5 inatumika kufuga na zaidi ya asilimia 60 inatumika katika uzalishaji wa bidhaa zinazotokana na kilimo pekee.