Thursday, May 26, 2016

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Maadhimisho ya Siku ya Umoja wa Afrika
Tanzania inaungana na nchi nyingine za Bara la Afrika kusherehekea Siku ya Afrika inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 25 Mei.
Sherehe hizo hufanyika kuadhimisha siku ya kuundwa  kwa Muungano wa Nchi za Afrika (OAU) Mwaka 1963 na baadaye Umoja wa Afrika (AU) mwaka 2002 pamoja na maendeleo ya demokrasia, amani na utulivu wa kisiasa, uchumi na kijamii yaliyopatikana tokea kuanzishwa kwa umoja huo.
Wakati wa kuadhimisha miaka 50 ya kuzaliwa kwa Umoja huo tarehe 25 Mei 2013 mjini Addis Ababa, Ethiopia Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika katika tamko lao waliahidi kumaliza kabisa vita ifikapo mwaka 2020 (Silencing the Guns by 2020).
Aidha, Umoja wa Afrika ulipitisha Agenda 2063 yenye kutaka Afrika yenye Amani, Maendeleo na utangamano (Afrika tunayoitaka ifikapo 2063 -Africa we want - 2063). Katika kutekeleza Agenda hiyo Umoja wa Afrika umeandaa mpamgo wa kwanza wa miaka kumi ya utekelezaji wa miradi ya kwanza muhimu iliyojikita kwenye sekta za nishati, usafirishaji, usafiri wa anga, sayansi na teknolojia pamoja na kukuza utangamano barani Afrika.
Kwa muktadha huo, Tanzania inatumia siku hii kuuhakikishia Umoja wa Afrika na Bara la Afrika kwa ujumla kuwa, itaendelea kuwa mwanachama mwaminifu na kuendelea kushirikiana na nchi nyingine katika kutekeleza malengo yake makubwa hususan Dira ya Maendeleo ya Afrika hususani Agenda 2063 na mpango wake huo wa kumaliza vita Barani Afrika ifikapo mwaka 2020.
Itakumbukwa kwamba, Tanzania imechangia kwa kiasi kikubwa kupigania uhuru wa nchi za Afrika, hususan Kusini mwa Afrika pamoja na kuendelea kutatua migogoro iliyopo Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Sudan Kusini, Darfur, Sudan na Burundi. Hivyo, kuadhimishwa kwa siku hii kunatoa fursa nzuri kama nchi kupitia upya nafasi yake katika Bara la Afrika na duniani kwa ujumla.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Dar es Salaam, 25 Mei, 2016.



No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.