Monday, June 21, 2021

MAANDALIZI YA MKUTANO WA 14 WA MAWAZIRI WA EAC WA SEKTA YA KILIMO NA USALAMA WA CHAKULA YAANZA JIJINI ARUSHA

Mkutano wa 14 Baraza la Kisekta la Mawaziri wa Kilimo na Usalama wa Chakula wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa Ngazi ya Wataalam umeanza leo tarehe 21 Juni 2021 jijini Arusha ukiwashirikisha Wataalam wa Kilimo kutoka Nchi Wanachama wa Jumuiya hiyo.


Mkutano wa Wataalam utafuatiwa na Mkutano wa Makatibu Wakuu utakaofanyika tarehe 24 Juni 2021 na kuhitimishwa na Mkutano wa Mawaziri utakaofanyika tarehe 25 Juni 2021.


Lengo la Mkutano wa 14 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wa Kilimo  na Usalama wa Chakula pamoja na mambo mengine ni kupitia na kujadili utekelezaji wa maamuzi na maelekezo ya Baraza la Mawaziri wa Jumuiya pamoja na kupitia na kujadili masuala mbalimbali  muhimu ya kisera, kikmkakati, miradi na program zinazotekelezwa katika sekta ya kilimo.


Kadhalika agenda muhimu zitajadiliwa wakati wa mkutano huo ambazo ni pamoja na Taarifa ya Usalama wa Chakula ya Jumuiya ya Afrika Mashariki; Taarifa kuhusu Mradi wa Afrika wa Kilimo cha Ushindani cha Mpunga kwa Kanda ya Afrika Mashariki; Taarifa kuhusu Maendeleo ya Mifugo; Taarifa kuhusu Mradi wa Kuzuia na Kudhibiti Sumukuvu; Taarifa kuhusu Maendeleo ya Uvuvi; na Taarifa kuhusu Uhamasishaji wa Uchangiaji Rasilimali.


Awali akifungua Mkutano huo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dkt. Peter Muthuki, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo anayeshughilikia Sekta za Uzalishaji na Jamii, Mhe. Christophe Bazivamo amezitaka Nchi Wanachama kujikita kwenye kilimo cha ushindani na kuboresha viwango vya mazao yanayozalishwa na nchi zote wanachama ili kupata soko la ndani na nje ya jumuiya la mazao hayo kwa manufaa ya wananchi wa jumuiya.


Pia amesisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuendelea kuwajengea uwezo wakulima katika maeneo yao kwa kutoa elimu ya kilimo bora na chenye manufaa ili kupata mazao bora yenye viwango vinavyokubalika ndani na nje ya mipaka ya nchi wanachama.


“Napenda kuzihimiza nchi wanachama kutoa elimu ya kilimo bora kwa wakulima wao pamoja na kuwajengea uwezo ili kuwawezesha kuzalisha mazao bora na yenye viwango vinavyokubalika ndani ya jumuiya na nje ili hatimaye wunufaike na soko la ndani na nje ya jumuiya” alisisitiza Dkt. Muthuki kwenye hotuba yake.


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mkutano huo wa Ngazi ya Wataalam, Bw. Julius Mwabu kutoka Jamhuri ya Kenya aliwataka wajumbe wa mkutano huo kujadili na kutoa mapendekezo yenye tija kuhusu Sekta ya Kilimo na Usalama wa Chakula kwani ni miongoni mwa sekta muhimu zinazotegemewa na wananchi wote wa nchi wanachama wa Jumuiaya ya Afrika Mashariki.


Aliongeza kuwa, mbali na changamoto ya ugonjwa wa corona uliozikumba nchi mbalimbali duniani zikiwemo zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki, yapo mafanikio kadhaa yaliyopatikana katika sekta ya kilimo na usalama wa chakula na kuwaomba wajumbe kujadili na kutoa mapendekezo ya namna ya kukabiliana na changamoto hiyo ili kuziwezesha nchi wanachama kutotetereka katika kipindi hiki ambacho ugonjwa huo bado haujatokomezwa.


Ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Ngazi ya Wataalam umeongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Kilimo, Bw. Gungu Mibavu na kuhudhuriwa pia na Maafisa Waandamizi kutoka Sekta mbalimbali zinazojishughulisha na masuala ya kilimo na usalama wa chakula hapa nchini. 

Kaimu Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Kilimo, Bw. Gungu Mibavu akizungumza kama kiongozi wa ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Wataalam uliofanyika jijini Arusha tarehe 21 Juni 2021 ikiwa ni maandalizi ya awali ya Mkutano wa 14 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wa Kilimo na Usalama wa Chakula wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika jijini hapa tarehe 25 Juni 2021. Mkutano wa ngazi ya wataalam utafuatiwa na Mkutano wa Makatibu Wakuu tarehe 24 Juni 2021.
Mwenyekiti wa Mkutano wa Ngazi ya Wataalam, Bw. Julius Mwabu kutoka Kenya akiwa na Mkurugenzi wa Sekta ya Uzalishaji katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bw.Jean Havugimana (kulia) pamoja na Katibu wa Mkutano huo kutoka Burundi

Mwenyekiti wa Mkutano wa Ngazi ya Wataalam, Bw. Mwabu akizungumza wakati wa mkutano huo
Mkurugenzi wa Sekta ya Uzalishaji kutoka Sekrtarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bw. Havugimana naye akizungumza wakati wa mkutano wa wataalam

Ujumbe wa Kenya ulioshiriki mkutano wa wataalam
Sehemu nyingine ya ujumbe wa Kenya ukifuatilia mkutano
Mjumbe wa Burundi naye akishiriki mkutano wa wataalam
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Biashara, Uwekezaji na Sekta za Uzalishaji katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Benjamin Mwesiga akishiriki mkutano wa wataalam
Ujumbe wa Tanzania ukiwa kwenye mkutano wa wataalam
Sehemu nyingine ya ujumbe wa Tanzania kutoka sekta mbalimbali zinazojishughulisha na kilimo wakifuatilia mkutano wa wataalam
Mkutano ukiendelea
Wajumbe kutoka Taasisi mbalimbali zilizo chini ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wakishiriki mkutano wa wataalam
Ujumbe wa Tanzania katika mkutano
Sehemu ya ujumbe wa Tanzania katika mkutano
Mkutano ukiendelea
Mshiriki mwingine wa mkutano kutoka Tanzania

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.