Monday, October 17, 2016

Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi za Umoja wa Afrika wapitisha Mkataba wa Afrika wa Usalama wa Usafiri Baharini na Maendeleo ya Afrika.

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi za Umoja wa Afrika wapitisha Mkataba wa Afrika wa Usalama wa Usafiri Baharini na Maendeleo ya Afrika.

Mkataba wa Afrika wa Usalama wa Usafiri Baharini na Maendeleo (The African Charter on Maritime Security, Safety and Development) umepitishwa katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi za Afrika (The AU Extraordinary Summit) uliofanyika tarehe 15 Oktoba, 2016 Lome, Togo. Kupitishwa kwa Mkataba huu kumefuatia makubaliano yaliyofikiwa katika Mikutano ya Kilele ya Wakuu wa Nchi za Afrika iliyofanyika Younde Juni, 2013 na Visiwa vya Shelisheli Februari,2015

Tanzania imewakilishwa katika Mkutano huo na Mhe. Balozi. Dkt. Augustine P. Mahiga (MB), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye hakuweza kuhudhuria Mkutano huu kwa sababu ya Majukumu mengine ya Kitaifa.

Akihutubia Mkutano huo Balozi Dkt. Mahiga alisema, Mkataba huo ni kati ya nyaraka muhimu zitakazoelimisha kuhusu kutunza amani ya Dunia, usalama na maendeleo katika karne hii ya 21. Alisisitiza kwamba Bara la Afrika liko kati ya bahari kuu mbili yaani Atlantic na Hindi ambazo ni kati ya bahari zilizo na shughuli nyingi sana za usafirishaji duniani. Tanzania ikiwa katika nusu ya ukanda wa pwani ya Mashariki na pwani ya Magharibi ya Bahari ya Hindi yenye urefu wa Kilomita 1400, Mkataba huu ambao Balozi Mahiga ametia sahihi kwa niaba ya Tanzania ni muhimu sana hivyo amewasihi wanachama wengine kuhakikisha wanafanya hivyo.

Sambamba na hilo Balozi Dkt. Mahiga amesema Mkataba huu si muhimu tu kwa Afrika kulinda bahari na rasilimali zake bali ni muhimu kwa dunia nzima. Balozi. Dkt. Mahiga ameomba Nchi zote na Mashirika ya Kimataifa kuunga mkono utekelezaji wa mkataba huu. Kufuatia kupitishwa kwa mkataba huu ameiomba Sekretariati ya Umoja wa Afrika kupeleka Mkataba huu kwenye Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na katika Jumuiya ya Kimataifa ili kuweza kutambuliwa.

Aidha, Balozi Mahiga amesisitiza kuwa bahari ni hadhina muhimu si tu ya samaki na gesi bali rasilimali nyinine za thamani kama vile madini ambazo zimekaa tu chini ya bahari hivyo ni jukumu la kila mwana Afrika kuhakikisha analinda rasilimali muhimu tulizo nazo zikiwemo hizi ambazo zinapatikana baharini.

Akimalizia hotuba yake Balozi. Dkt. Mahiga alisisitiza “Hivi karibuni bahari hizi ( Atlantic na Hindi) zitakuwa chanzo muhimu cha nishati, hivyo kusaidia jitihada za kuleta maendeleo kupitia rasilimali za bahari, naamini mkataba huu utakuwa ni silaha muhimu katika kulinda rasilimali hizi za bahari kwa ajili ya sasa na vizazi vijavyo”. Balozi. Dkt. Mahiga ameusihi Umoja wa Afrika na Wanachama wote kuendelea kuuboresha Mkataba huu na kupitisha viambasho muhimu na hatimaye kuharakisha kuuridhia Mkataba huu ili utekelezaji wake uanze bila kuchelewa.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Dar es Salaam, 16 Oktoba, 2016

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.