Thursday, February 15, 2018

Waziri Mahiga afanya mazungumzo na Wabunge wa EALA

                         
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt.Augustine Mahiga akizungumza na Wabunge wa EALA (hawapo pichani).
Wabunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA)  leo wamekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Dkt.Augustine Mahiga Wizarani mjini Dodoma. Wabunge wa EALA wamewasili mjini Dodoma wakiwa katika ziara ya kutembelea miradi mbalimbali ya Jumuiya inayotekelezwa na nchi wanachama za Jumuiya ya Afrika Masharaiki. 

Katika ziara hii Wabunge wanatembelea miradi inayotekelezwa katika ushoroba wa kati (central corridor) sambamba na kubaini changamoto zinazoikabili miradi hiyo na namna inavyorahisha utoaji huduma kwa wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Katika mazungumzo yao na Waziri Mahiga, Wabunge wa EALA wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utekelezaji mzuri wa miradi inayotokana na makubaliano ya Jumuiya kama vile ujenzi wa mizani za kisasa sambamba  na kupunguza idadi ya mizani hiyo ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa, hudumu na watu ndani Jumuiya.

Hadi sasa Tanzania kwa upande wa ushoroba wa kati imefanikiwa kupunguza idadi ya vituo vya mizani kutoka  vituo saba hadi vitatu.

Kwa upande wake Waziri Mahiga, amewapongeza Wabunge wa EALA kwa kuona umuhimu wa kutembelea miradi ya Jumuiya inayotekelezwa na nchi Wanachama ambayo inagusa maisha ya wananchi moja kwa moja. Aidha amesema katika ziara hii Wabunge wataweza kubaini changamoto zinazowakabili wananchi, hivyo kuwa katika nafasi nzuri ya kuweza kutatua changamoto hizo wakati wa utekelezaji wa majukumu yao Bungeni.

Mbunge wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki kutoka Tanzania Mhe. Dkt. Ngwaru Maghembe (kushoto) akizungumza na Waandishi wa Habari walipotembelea ofisi za Wizara mjini Dodoma. Kulia ni  Mhe. Wanjiku Muhia  kutoka Kenya ambaye pia ni kiongozi wa msafara wa ziara hiyo
Mhe. Adam Kimbisa Mbunge wa EALA (Tanzania) akizungumza wakati wa Mkutano na Waandishi wa Habari



Mkutano ukiwa unaendelea

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.