Friday, March 15, 2013

Rais Kikwete atuma Salamu za Pongezi kwa Rais wa China



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za pongezi Mheshimiwa Xi Jinping kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China.

Rais Jinping alichaguliwa Jumanne wiki hii kuwa Rais wa China kuchukua nafasi ya Mheshimiwa Hu Jintao ambaye amemaliza muda wa uongozi wa miaka 10.
Katika salamu zake za pongezi, Rais Kikwete amemwambia Rais Jinping: “Naomba uniruhusu nitumie nafasi hii kukupongeza kwa dhati kutokana na ushindi wako mkubwa na uliostahiki wa kuwa Rais wa taifa lako kubwa.”

“Kama unavyojua China na Tanzania zimekuwa na mahusiano maridadi kwa zaidi ya miaka 50 kwa sasa. Tunawashukuru waanzilishi ya mataifa yetu: Mwenyekiti Mao Tse Tung na Waziri Mkuu Chou En Lai kwa upande wa China na Rais Julius Kambarage Nyerere kwa upande wa Tanzania. Urafiki huu umedumu na kuhimili muda wote, umekuwa wa kudumu kwa hakika wakati wote umedumishwa, umelelewa na kuendelezwa na vizazi vilivyofuatia vya viongozi wa nchi zote mbili, “ amesema Rais Kikwete na kuongeza:

“Mataifa yetu mawili rafiki yanashirikiana kwenye masuala mengi yanayohusu mataifa yetu yenyewe mawili, masuala ya kikanda na yale ya kimataifa, na wakati wote tumeungana mkono katika uwanja wa kimataifa. Napenda kukuhakishia utayari wangu binafsi na ule wa Serikali yangu kufanya kazi nawe katika kuendeleza uhusiano huu na kuufikisha kwenye hatua kubwa zaidi.”

Amesisitiza Rais Kikwete: “Sisi katika Tanzania tunajiandaa kwa ari kubwa na matarajio makubwa kukupokea Mheshimiwa baadaye mwezi huu kwenye ziara yako ya kwanza ya Kiserikali katika Tanzania. Hakuna shaka kuwa siyo tu kwamba ziara yako itakuwa ya kihistoria bali pia itasaidia kuimarisha mahusiano ya nguvu na ya karibu sana ya urafiki na uhusiano ambayo umedumu kwa furaha baina ya mataifa yetu mawili na watu wake, pamoja na Afrika kwa jumla.”

Amemalizia Rais Kikwete katika salamu zake za pongezi: “Nakutakia Mheshimiwa kila la heri na kila aina ya mafanikio wakati unajiandaa kuanza kazi na wajibu wako wa heri wa kuongoza taifa lako kubwa na wananchi rafiki wa China ili kuwaelekeza kwenye hatua kubwa zaidi ya maendeleo.”


Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu.

Dar es Salaam.

15 Machi, 2013




No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.