Friday, August 24, 2018

Mikutano ya JPC ni Injini ya Maendeleo ya kiuchumi

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Tanzania na Uganda zimepata mafanikio makubwa kupitia Mikutano ya Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) iliyofanyika Arusha Aprili 2017 na sasa wa Kampala unaohitimishwa leo.

Kauli hiyo ilitolewa kwa pamoja na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Mhe .Dkt. Augustine Mahiga (Mb) na mwenzake wa Uganda, Mhe. Sam Kutesa walipokuwa wanasoma hotuba za ufunguzi wa mkutano huo.

Mafanikio yaliyoelezwa ni pamoja na kusainiwa kwa Mikataba ya Makubaliano tisa ikiwemo Mikataba ya kushirikiana katika uendelezaji wa bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka Dar Es Salaam hadi Uganda na ushirikiano katika masuala ya elimu na mafunzo iliyosainiwa leo katika mkutano wa Kampala.

Mkutano huo ulijulishwa kuwa utekelezaji wa mikataba hiyo unaridhisha na inalenga kurahisisha ukuaji wa uchumi wa nchi hizo ili kutimiza azma ya viongozi wake, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mhe. Yoweri Museveni wa Uganda ya kukuza biashara kati ya nchi hizo.

Mikataba iliyosainiwa  inahusu uendelezaji wa miradi ya miundombinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na nishati ya Umeme, barabara hususan za mipakani, bandari, reli na usafiri wa anga.

Kufuatia mikataba hiyo miradi mbalimbali ipo katika hatua tofauti za utekelezaji ikiwemo mradi wa kuzalisha umeme wa Kikagati/ Murongo uliopangwa kukamilika mwaka 2020. Aidha, Shirika la Ndege la Tanzania litaanza safari za moja kwa moja kutoka Dar Es Salaam hadi Entebbe mwishoni mwa mwezi huu kufuatia kusainiwa kwa mkataba wa masuala ya anga katika mkutano wa Arusha mwezi Aprili 2018

Miradi mingine ni ya ukarabati wa bandari za Bell na Bukasa na ukarabati wa meli za Kagawa na Pamba kwa upande wa Uganda ambayo italeta muunganiko mzuri katika usafirishaji hasa baada ya Reli ya Kisasa ya kiwango cha kimataifa inayojengwa na Tanzania itakapokamilika.

Waheshimiwa Mawaziri walisisitiza umuhimu wa Serikali za Tanzania na Uganda kuwekeza ipasavyo katika ushoroba wa kati ili kuleta muunganiko kwa ajili ya kukuza biashara. Aidha. Walisisitiza umuhimu wa kuondoa vikwazo visivyo vya kibiashara na kushughulikia changamoto za mipakani kwa haraka kadri zinavyojitokeza

Kutokana na umuhimu wa utekelezaji wa miradi inayoafikiwa katika mikutano hiyo, pande zote mbili ziliwakilishwa na viongozi wa ngazi ya juu wakiwemo Mawaziri na Makatibu Wakuu. 

Kwa upande wa Tanzania, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. William Lukuvi. Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwele, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Subira Mgalu walishiriki mkutano huo.


Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Kampala
23 Agosti 2018

Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda, Mhe. Sam Kutesa akisoma hotuba katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Uganda uliofanyika Kampala kwa siku tatu kuanzia tarehe 21 hadi 23 Agosti 2918.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akisoma hotuba katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Uganda uliofanyika Kampala kwa siku tatu kuanzia tarehe 21 hadi 23 Agosti 2018.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. William Lukuvi akichangia jambo katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Uganda.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwele akichangia jambo katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Uganda.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage akichangia jambo katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Uganda.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji akichangia jambo katika mkutano wa pili wa JPC kati ya Tanzania na Uganda.


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Subira Mgalu akichangia jambo katika Mkutano wa Pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC0 kati ya Tanzania na Uganda.

Sehemu ya Waheshimiwa Mawaziri kutoka Uganda wakiwa katika mkutano huo.

Kaimu Mkurugenzi wa Afrika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Salvator Mbilinyi akichangia jambo katika mkutano huo.

Wajumbe wa Tanzania na Uganda wakiendelea na mkutano.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga (kulia) na Waziri wa Maendeleo ya Madini wa Uganda, Mhe. Peter T. Lokeris wakiweka saini Mkataba wa Makubaliano (MoU) wa kuendeleza ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi asilia kutoka Dar Es Salaam hadi Uganda. Aliyesimam kushoto kwa Mhe. Mahiga ni Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Subira Mgalu.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akibadilishana Mikataba na  Waziri wa Maendeleo ya Madini wa Uganda, Mhe. Peter T. Lokeris baada ya kusainiwa.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga na Waziri wa Elimu ya Juu wa Uganda, Mhe. J.C Muyingo wakiweka saini Mkataba wa Makubaliano (MoU) wa kushirikiana katika masuala ya Elimu na Mafunzo.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga na Waziri wa Elimu ya Juu wa Uganda, Mhe. J.C Muyingo wakibadilishna Mkataba wa Makubaliano (MoU) wa kushirikiana katika masuala ya Elimu na Mafunzo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda, Mhe. Sam Kutesa akimkabidhi Hati za Viwanja va Ubalozi wa Tanania nchini Uganda Mhe. Dkt. Augustine Mahiga.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Uganda, Balozi Patrick Mugoya (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan Mwinyi wakibadilishana taarifa ya masuala yote yaliyoafikiwa katika mkutano huo.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.