Wednesday, August 22, 2018

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Ushirika wa Uganda, Balozi Julius Onen akisoma hotuba ya ufunguzi katika Mkutano wa Jukwaa la Biashara kati ya Tanzania na Uganda uliofanyika Kampala siku ya Jumatano tarehe 22 Agosti 2018.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mhandisi Deusdedit Kakoko akichangia mada katika mkutano huo ambapo alisema kuwa Mamlaka ya Bandari imeboresha kwa kiasi kikubwa huduma zake

Mkurugenzi wa Shirika la kukuza Biashara katika nchi za Afrika Mashariki kwa upande wa Uganda (Trademark East Africa), Bibi Dawali Ssali akieleza mikakati ya inayofanywa na shirika hilo katika kuboresha mazingira ya biashara katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. mikakati hiyo ni pamoja na kushirikiana na nchi za EAC kujenga vituo vya kutoa huduma kwa pamoja mipakani.


Wajumbe wa Uganda na Tanzania wakijadili mikakati ya kukuza na kuimarisha biashara kati ya nchi zao.


Tanzania na Uganda za azimia kukuza biashara kati yao

Tanzania na Uganda zimeazimia kuondoa vikwazo vya kibiashara ili kukuza kiwango cha biashara kati yao ambacho kwa takwimu zilizopo sasa zinaonesha kipo chini mno.

Hayo yalibainishwa katika mkutano wa Jukwaa la biashara kati ya Tanzania na Uganda uliofanyika leo kando ya Mkutano wa pili wa Tume ya Kudumu ya Pamoja ya Ushirikiano (JPC) unaofanyika kwa silku tatu jijini Kampala tokea tarehe 21 Agosti 2018.

Mgeni Rasmi katika mkutano huo ambaye alikuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Ushirikia ya Uganda, Balozi Julius Onen alieleza kuwa Tanzania na Uganda zina nafasi kubwa ya kukuza biashara endapo njia za usafiri zitaboreshwa, vikwazo visivyo vya kibiashara vitaondolewa pamoja na kuwa na mikakati ya pamoja ya kuweka viwango vya ubora vinavyotambulika katika nchi zote na kanda nzima kwa ujumla.

Mkutano huo ambao ulihudhuriwa na wawakilishi mbalimbali wa Tanzania akiwemo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Mhandisi Deusdedit Kakoko alisema kuwa Mamlaka ya Bandari imeboresha kwa kiasi kikubwa huduma zake ikiwemo kuanza upya kwa njia ya Dar Es Salaam- Mwanza hadi bandari ya Bell nchini Uganda. Alisema kufunguliwa kwa njia hiyo kumepunguza idadi ya siku za kusafirisha mizigo kutoka Dar Es Salaam hadi Uganda ambapo kwa sasa mizigo inasafirshwa kwa siku nne  na kwa kiwango kikubwa na gharama nafuu.

Jambo hilo liliungwa mkono na wafanyabiashara wa Uganda walioshiriki mkutano huo ambapo waliipongeza TPA kutokana na hatua inazozichukua kuboresha huduma katika Bandari ya Dar Es Salaam na walikiri kuwa kufunguliwa kwa njia ya Dar Es Salaam-Mwanza hadi Bandari ya Bell kumepunguza kwa kiasi kikubwa gharama za kufanya biashara pamoja na muda wa kusafirisha bidhaa zao.

Balozi Onen aliendelea kueleza kuwa licha ya changamoto zilizopo za kufanya biashara kati ya Uganda na Tanzania lakini vihatarishi vya kufanya biashara na Tanzania ni vichache ukilinganisha na nchi nyingine.  Hivyo, aliwsihi wafanyabiashara wa Uganda na Serikali kwa ujumla kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na nchi hiyo.

Alibainisha kuwa Tanzania na Uganda zinaweza kufaidika zaidi kibiashara kutokana na nchi zote kuwa kwenye eneo la Maziwa Makuu ambalo lina soko kubwa kutokana na idadi kubwa ya watu katika eneo hilo. Hivyo alizihimiza Serikali zaTanzania na Uganda kufanya uwekezaji mkubwa katika ushoroba wa kati (central corridor) ili kukuza biashara.

Mkutano wa JPC unatarajiwa kufungwa rasmi Alhamisi kwa kikao cha ngazi ya Mawaziri ambapo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Dkt. Augustine Mahiga (Mb), Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. William Lukuvi (Mb), Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi. Isack Kamwele (Mb) na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Subira Mgalu (Mb) watashiriki mkutano huo.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Kampala
22 Agosti 2018

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.