Friday, August 17, 2018

Makamu wa Rais, Mhe Samia Suluhu Hassan aongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano wa Wakuu wa Nchi na Seriikali wa SADC wanaounda Utatu wa Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, ulinzi na Usalama.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa katika mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) wanaounda Utatu wa Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama uliofanyika mjini Windhoek, Namibia tarehe 16 Agosti 2018. 
Kutoka kushoto ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Adolf Mkenda wakifuatilia mkutano.

Mhe. Samia Suluhu Hassan amemuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli katika mkutano huu pamoja  na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC utakaofanyika tarehe 17 na 18 Agosti 2018.

Mkutano huu umehusisha Wakuu wa Nchi na Serikali wanaounda Utatu huo ambao ni Mheshimiwa João Manuel Gonçalves Lourenço, Rais wa Angola  na Mwenyekiti wa sasa wa SADC organ; Mheshimiwa Edgar Chagwa Lungu, Rais wa Jamhuri ya Zambia  na Makamu Mwenyekiti wa SADC Organ na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa SADC Organ aliyemaliza muda wake.

 Mkutano huu umejadili taarifa ya hali ya siasa, ulinzi na usalama katika kanda kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita wa Agosti 2017 hadi Agosti 2018.

Agenda nyingine zilizojadiliwa katika mkutano huo ni pamoja na; taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya SADC kuhusu kuimarisha hali ya siasa, ulinzi na usalama katika falme ya lesotho, hali ya siasa na usalama katika jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC),hali ya siasa na usalama nchini Madagasca,hali ya kidemokrasia katika kanda na taarifa ya uchaguzi mkuu kwa nchi wanachama ambao ni Madagasca, DRC na Eswatini.

vilevile mkutano huu umejadili kuhusiana na ujenzi wa sanamu ya Mwalimu Julius Nyerere iliyopendekezwa kujengwa katika jengo la Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika mjini Addis Ababa Ethiopia pamoja na majukumu ambayo serikali ya Tanzania imepewa katika kusimamia zoezi hilo linakamailika kwa wakati.

Makamu wa Rais. Mhe. Samia Suluhu Hassan akijadili jambo na Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kikanda wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Innocent Shiyo wakati wa hafla ya ufunguzi wa mkutano huo.

Wajumbe wa Serikali ya Tanzania na Zambia wakifuatitilia hafla ya ufunguzi wa mkutano. Kulia kwa Makamu wa Rais ni Rais wa Jamhuri ya Zambia, Mhe. Edgar Chagwa Lungu


Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika, Dkt. Stergomena L.Tax (kulia) akitoa hotuba ya ufunguzi wa mkutano. Kushoto ni Rais wa Jamhuri ya Namibia na Mwenyekiti wa Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama.

Mhe. Waziri Mahiga (kati) akijadili jambo na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Prof. Adolf Mkenda (kulia) na Balozi Shiyo (kushoto) 

Mhe. Makamu wa Rais akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Mhe. Joseph Kabila kabla ya kuanza kwa mkutano huo. 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.