Monday, May 20, 2019

Tanzania na Uholanzi zazindua Mradi wa Kukua na Kuku



Dodoma, 20 Mei 2019

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Tanzania na Uholanzi zazindua Mradi wa Kukua na Kuku

Ubalozi wa Tanzania nchini Uholanzi kwa kushirikiana na Baraza la Biashara la Uholanzi na Africa (Netherlands – Africa Business Council - NABC) hivi karibuni waliongoza ujumbe wa Makampuni 7 kutoka Uholanzi yaliyobobea katika Sekta ya Ufugaji wa Kuku kwenda Mkoani Kilimanjaro kuzindua Mradi maalum wa ufugaji utakaoendeshwa na Makampuni hayo nchini Tanzania maarufu kama “Kukua Na Kuku (Growing with Chicken) Impact Cluster”.
      Mradi wa “Kukua Na Kuku” ni matokeo ya makubaliano ya kuanzisha ubia kati ya Tanzania na Uholanzi yanayolenga kuboresha Sekta ya Ufugaji Kuku nchini Tanzania na kuifanya kuwa endelevu kwa kutumia teknolojia ya kisasa kutoka Uholanzi. Makampuni hayo yatatoa mafunzo kwa lengo la kuwajengea uwezo wafugaji wazawa kwa kuboresha usimamizi wa kilimo cha ufugaji, afya ya wanyama, upatikanaji wa chakula (lishe) bora kwa ajili ya mifugo, vifaa muhimu vya kufugia, na hata utafutaji masoko.
Uzinduzi huo ulifanyika kwenye Chuo cha Kilimo na Ufugaji wa Mifugo Kilacha, Mkoani Kilimanjaro kwa kusaini Makubaliano ya Ushirikiano, na ukawa ndio mwanzo wa ushirikiano wa miaka 3 kati ya makampuni hayo 7, Serikali ya Uholanzi na wadau wazawa wa Tanzania. Chuo cha Kilimo na Ufugaji wa Mifugo cha Kilacha kinasimamiwa na Kituo cha Uzalishaji na Mafunzo kinamilikiwa na Kanisa Katoliki Mkoani humo.
Mgeni rasmi wakati wa sherehe za uzinduzi huo alikuwa Mhe. Anna Mgwira, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro. Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju, Kaimu Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania Bibi Lianne Houben, na Mkurugenzi wa Biashara na Kilimo wa NABC, Bw. Mackenzie Masaki.

Makampuni hayo kutoka Uholanzi ni pamoja na: Aeres University of Applied Sciences; Ebit+/I Grow Chicken; GD Animal Health; Impex; Hendrix Genetics; Koudijs de Heus; na Vencomatic Group.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Dkt. Anna Mngwira ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika hafla ya uzinduzi wa Mradi wa Kukua na Kuku akitoa neno katika sherehe za uzinduzi wa Mradi huo. Kushoto kwake ni Padri Paul Huria, Msaidizi wa Meneja Mkuu wa Kituo cha Uzalishaji na Mafunzo, Kilacha akimsikiliza kwa makini.
Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, Mhe. Irene Kasyanju (pichani juu) na Kaimu Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania, Bibi Lianne Houben (pichani chini) wakitoa hotuba fupi wakati wa Uzinduzi wa Mradi wa Kukua Na Kuku huko Kilacha, Moshi, Mkoani Kilimanjaro.
Kutoka kulia ni Padri Landelimi Makiluli, Meneja Mkuu wa Kituo cha Uzalishaji na Mafunzo, Kilacha; Padri (Monsignor) Paul Huria, Msaidizi wa Meneja Mkuu wa Kituo; Mhe. Dkt. Anna Mgwira, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro; Bibi Lianne Houben, Kaimu Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania; na mwishoni kushoto ni Mhe. Irene Kasyanju, Balozi wa Tanzania nchini Uholanzi wakijiandaa na uzinduzi wa Mradi wa Kukua na Kuku
Wawakilishi wa Taasisi zenye ubia katika Mradi wa Kukua na Kuku wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro wakiweka saini Makubaliano ya Ushirikiano tayari kuanza utekelezaji wa Mradi huo huko Kilacha, Mkoani Kilimanjaro
Picha ya pamoja baada ya kusainiwa Makubaliano ya Ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania, Serikali ya Uholanzi, Makampuni tajwa 7 yakiongozwa na Mkurugenzi wa Biashara na Kilimo kutoka NABC, Bw. Mackenzie Masaki (wa pili kutoka kushoto). Wa kwanza kushoto ni Bibi Theo Mutabingwa, Afisa Kilimo katika Ubalozi wa Uholanzi nchini Tanzania.
Balozi Irene Kasyanju akibadilishana mawazo na wawakilishi wa Kampuni ya Hendrix Genetics, Bw. Peter Arts (kushoto); na Ebit+/I Grow Chicken, Bw. Eric Mooiweer (kulia) mara baada ya uzinduzi wa Mradi wa Kukua na Kuku utakaoendeshwa na Makampuni tajwa 7 kutoka Uholanzi 









No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.