Tuesday, June 13, 2023

SHIRIKA LA NDEGE LA UFARANSA LAANZA SAFARI ZA MOJA KWA MOJA KUTOKA PARIS HADI DAR

Shirika la Ndege la Ufaransa yaani Air France limezindua safari yake ya kwanza kutoka Paris Charles de Gaulle hadi jijini Dar es Salaam tarehe 12 Juni 2023.

 

Uzinduzi wa safari hizi ni mwendelezo wa huduma za Shirika hilo baada ya kuazisha safari zake za moja kwa moja kutoka Paris hadi Zanzibar mwaka 2021.

 

Kuanzishwa kwa safari hii mpya na Shirika hilo ni matokeo ya jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kuhamasisha utalii, biashara na uwekezaji nchini . Lakini pia zinatokana na ushirikiano na uhusiano mzuri wa kidiplomasia uliopo baina ya Tanzania na Ufaransa.

 

Aidha, inatarajiwa kuwa kuanzishwa kwa safari hizi kutasaidia kuongeza idadi ya watalii, wawekezaji na wafanyabiashara watakaotembelea nchini na hatimaye kukuza uchumi wa nchi.

 

Huduma za usafiri kupitia Air France  zitafanyika mara tatu kwa wiki katika siku za Jumatatu, Jumatano na Jumamosi ambapo Shirika hilo litatumia ndege aina ya Boeing 787-9.

 

Viongozi wa Serikali wakiongozwa na Mhe. Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi walishiriki kwenye mapokezi hayo ambayo pia yalimshirikisha Balozi wa Ufaransa nchini, Mhe. Nabil Hajlaoui huku Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma M. Rajab akimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Dkt. Stergomena Tax kwenye mapokezi hayo.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Prof. Makame Mbarawa (wa nne kushoto) akiwaongoza viongozi wengine kukata utepe kuashiria mapokezi ya ndege ya Shirika la Air France iliyoanza rasmi safari zake kutoka Paris hadi Dar es Salaam tarehe 12 Juni 2023. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma M. Rajab aliyemwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax kwenye mapokezi hayo
Ndege ya Shirika la Air France ikipokelewa kwa kumwagiwa maji baada ya kuwasili kwa mara ya kwanza katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam ikitokea Paris, Ufaransa. Ndege hiyo itafanya safari zake jijini Dar es Salaam mara tatu kwa wiki katika siku za Jumatatu, Jumatano na Jumamosi
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Fatma M. Rajab akizungumza wakati wa hafla fupi iliyoandaliwa  na Ubalozi wa Ufaransa nchini. Hafla hiyo ilifanyika kabla ya mapokezi rasmi ya Ndege ya Air France.
Hafla ikiendelea
Balozi Fatma na Viongozi wengine wakiwemo Mabalozi na Wawakilishi wa Ubalozi wa Ufaransa nchini wakikata keki kuashiria kukaribisha safari za Ndege za Shirika la Air France kutoka Paris kuja Dar es Salaam. Hafla hiyo ilifanyika kabla ya ndege hiyo kuwasili
Picha ya pamoja














 

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.