Thursday, August 8, 2024

MAKATIBU WAKUU WA SADC WAKUTANA JIJINI HARARE

Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamekutana Harare, Zimbabwe kwa ajili ya maandalizi ya Mkutano wa 44 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya husika utakaofanyika tarehe 17-18 Agosti, 2024.

 

Mkutano huo unatarajia kujadili masuala mbalimbali ikiwemo, hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Maendeleo wa SADC, usalama wa chakula na lishe kwenye kanda na Utekelezaji wa Mpango wa Manunuzi ya Pamoja ya Huduma za Afya ya SADC unaoratibiwa na Bohari ya Dawa (MSD) ya Tanzania.

Aidha, hafla ya ufunguzi wa mkutano huo imewezesha makabidhiano ya nafasi ya unyekekiti katika ngazi ya Mkutano wa Makatibu Wakuu ambapo Mwenyekiti aliyemaliza muda wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Angola, Balozi Nazaré José Salvador amekabidhi nafasi hiyo kwa mwenyekiti mpya, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Biashara ya Kimataifa wa Jamhuri ya Zimbambwe, Balozi Albert Ranganai Chimbindi akisisitiza kumpa ushirikiano katika nafasi hiyo.

 

Naye Balozi Chimbindi amemshukuru Mwenyekiti aliyemaliza muda wake kwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu. Pia ameahidi kuzingatia ushauri aliokuwa akiutoa kwa Sekretariet ya SADC na kufanya kazi pamoja ili kuyafikia malengo ya jumuiya hiyo kwa maslahi  jumuishi.

 

“Tumepiga hatua lakini bado tuna kila sababu ya kuweka bidii kwenye ujenzi wa miundombinu, usafiri na hatimaye tuweze kuifikia SADC tunayoitaka. Niwahakikishie kuwa Zimbabwe ipo tayari kufanya kazi pamoja nanyi kwa kufuata malengo, kanuni na mikataba ya SADC'', Balozi Chimbindi.

 

Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali SADC utatanguliwa na mikutano ya awali kwa ajili ya maandalizi ambayo ni: Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Asasi ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC (SADC Organ on Politics, Defence and Security) utakaofanyika tarehe 16 Agosti 2018 ambao utapitia na kujadili hali ya siasa, ulinzi na usalama katika kanda kwa kipindi cha Agosti 2023 hadi Agosti 2024. Mkutano huu utahusisha nchi tatu za SADC Organ TROIKA na wajumbe wake ambao ni Angola (Mwenyekiti wa sasa wa Asasi ya SADC ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama), Zambia (Makamu Mwenyekiti wa Organ) na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (Mwenyekiti wa Organ aliyemaliza muda wa uenyekiti wa Asasi).

 

Mikutano mingine ni: Mkutano wa Mawaziri utakaofanyika kuanzia tarehe 13 hadi 14 Agosti 2024 pamoja; na Mkutano wa Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo ya kusini mwa Afrika utakaofanyika kuanzia tarehe 8 hadi 11 Agosti, 2024. 

===================================

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu Mwamba ameshiriki katika Kikao cha Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) ambacho ni sehemu ya vikao vya maandalizi ya Mkutano wa 44 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya hiyo utakaofanyika tarehe 17 na 18 Agosti, 2024 Harare, Zimbabwe. Kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini nchini Zimbabwe, Mhe. IGP (RTD) Simon Sirro.

Mkurugenzi Idara ya Ushirikikiano wa Kikanda kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Talha Waziri akifuatilia hafla ya ufunguzi katika mkutano huo wa Mkatibu Wakuu ulioanza leo tarehe 8 Agosti, 2024 Harare, Zimbambwe.

Kushoto ni Afisa Sheria Mkuu kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bi. Felister Lero na Afisa Msimamizi wa Fedha Mkuu kutoka Wizara ya Fedha, Bw. Joseph Haule wakifatilia mkutano.

Picha ya pamoja: Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) baada ya ufunguzi wa Mkutano wa 44 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC uliofanyika tarehe 8 Agosti, 2024 Harare, Zimbabwe.

 

Mwenyekiti aliyemaliza muda wake, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Angola, Balozi Nazaré José Salvador amekabidhi nafasi hiyo kwa mwenyekiti mpya, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Biashara ya Kimataifa wa Jamhuri ya Zimbambwe, Balozi Albert Ranganai Chimbindi ambapo amesisitiza kumpa ushirikiano katika nafasi hiyo.

Habari katika picha 









No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.