Sunday, November 18, 2018

Dkt. Ndumbaro azungumzia ziara ya Kampuni kubwa kutoka Uturuki zenye nia ya kuwekeza nchini


Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb.) akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo) pichani kuhusu ziara ya ujumbe wa Makampuni 7 makubwa ya uwekezaji kutoka Uturuki itakayofanyika nchini kuanzia tarehe 18 hadi 24 Novemba, 2018. Ujumbe huo utatembelea mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma na Simiyu kwa ajili ya kuangalia fursa za uwekezaji katika ujenzi wa viwanda vya nguo, kiwanda cha kuongeza thamani bidhaa za kilimo, ujenzi wa maduka makubwa na hoteli za kimataifa. Mkutano huo na waandishi wa habari ulifanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam tarehe 18 Novemba, 2018.
Sehemu ya wanahabari kutoka vyombo mbalimbali vya habari wakinukuu taarifa kutoka kwa Mhe. Dkt. Ndumbaro (hayupo pichani)


Sehemu nyingine ya wanahabari wakiwajibika
Waandishi wa Habari wakifuatilia taarifa kuhusu ziara ya ujumbe wa Makampuni ya uwekezaji kutoka Uturuki iliyokuwa ikitolewa na Mhe. Dkt. Ndumbaro (hayupo pichani)


Balozi wa Uturuki nchini, Mhe. Ali Davutoglu (kushoto) akiwa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bw. Jestas Nyamanga (katikati) pamoja na Afisa kutoka Ubalozi wa Uturuki wakifuatilia mkutano kati ya Dkt. Ndumbaro na Waandishi wa Habari (hawapo pichani)
Mkutano ukiendelea
Mwandishi kutoka Gazeti la Nipashe, Bw. Gwamaka akimuuliza swali Dkt. Ndumbaro (hayupo pichani)
Balozi wa Uturuki nchini, Mhe. Davutoglu nae akizungumza wakati wa mkutano huo kuhusu ziara ya ujumbe kutoka Uturuki huku Mhe. Dkt. Ndumbaro akisikiliza
Sehemu ya Maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na JNICC wakimsikiliza Balozi Davutoglu (hayupo pichani)
Awali Bw. Hassani Mwamweta, Afisa Mambo ya Nje akieleza utaratibu kuhusu mkutano kati ya Mhe. Dkt. Ndumbaro na waandishi wa habari kabla ya mkutano huo kuanza.
Mhe. Naibu Waziri Dkt. Ndumbaro pamoja na Mhe. Balozi Davutoglu na wajumbe wengine akiwemo Bw. Nyamanga wakimsikiliza Bw. Mwamweta (hayupo pichani) akitoa utaratibu wa mkitano kabla ya mkutano kuanza
Kabla ya kushiriki mkutano na waandishi wa habari Mhe. Dkt. Ndumbaro alikutana na Balozi wa Uturuki nchini Mhe. Davutoglu 


Mhe. Dkt. Ndumbaro akizungumza na Mhe. Balozi Davutoglu
  
Mhe. Dkt. Ndumbaro akimweleza jambo Mhe. Balozi Davutoglu  huku mara baada ya kumaliza mkutano kati yake na waandishi wa Habari.  Pembeni ni Bw. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika
Mhe. Dkt. Ndumbaro akiagana na Mhe. Balozi Davutoglu

Mhe. Balozi Davutoglu akibadilishana mawazo na Bw. Nyamanga, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika pamoja na Bw. Mwamweta mara baada ya mkutano kati ya Dkt. Ndumbaro na waandishi wa habari kumalizika

======================================================

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

KUHUSU ZIARA YA UJUMBE WA MAKAMPUNI MAKUBWA YA UWEKEZAJI KUTOKA UTURUKI HAPA NCHINI

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro ameipongeza Serikali ya Uturuki kwa kuendelea kuimarisha ushirikiano na Serikali ya Tanzania hususan katika kukuza biashara, uwekezaji na utalii.

Mhe. Dkt. Ndumbaro ametoa pongezi hizo wakati wa mkutano  na Waandishi wa Habari uliofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam tarehe 18 Novemba 2018 kuhusu ziara ya ujumbe wa Makampuni 7 makubwa ya uwekezaji kutoka Uturuki.

Mhe. Dkt. Ndumbaro alisema kuwa, ziara ya ujumbe huo nchini ambayo itafanyika kuanzia tarehe 18 hadi 24 Novemba 2018 ni  mwendelezo wa jitihada za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa kushirikiana na Ubalozi wa Tanzania nchini Uturuki na wadau mbalimbali katika kutekeleza diplomasia ya uchumi ambayo pamoja na mambo mengine inalenga kwenye kutafuta na kuleta wawekezaji wenye nia ili wawekeze katika maeneo mbalimbali hapa nchini kwa lengo la kukuza uchumi na kuinua kipato cha wananchi.

Akielezea ziara hiyo, Dkt. Ndumbaro alieleza kuwa, ujumbe wa wawekezaji kutoka Makampuni hayo ya Uturuki hapa nchini utatembelea mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma na Simiyu. Alisisitiza kwamba ujumbe huo umechagua mikoa hiyo kwa malengo  mahsusi ya kuwekeza katika sekta ya viwanda ikiwemo Kiwanda cha nguo, kiwanda cha sukari, kiwanda cha saruji, kiwanda cha vifaa vya ujenzi, kiwanda cha kuongeza thamani bidhaa na uwekezaji kwenye sekta ya nishati kwa mkoa wa Simiyu.

Aidha, kwa mkoa wa Dodoma ujumbe huo una nia ya kuwekeza katika ujenzi wa maduka makubwa (shopping malls), ujenzi wa majengo mbalimbali (real estate) na ujenzi wa hoteli zenye hadhi ya kimataifa.

“Tunaishukuru kwa dhati kabisa Uturuki kwani imekuwa nchi ya kwanza kutekeleza azma ya Serikali ya kuhamia Dodoma kwa kuonesha nia thabiti ya kuwekeza kwenye sekta mbalimbali mkoani humo ikiwemo maduka makubwa ya biashara (shopping malls) na hoteli za kimaifa zenye hadhi ya nyota tano” alisema Dkt. Ndumbaro.

Mhe. Dkt. Ndumbaro aliongeza kusema kuwa, ushirikiano kati ya Tanzania na Uturuki umekuwa ukiongezeka mwaka hadi mwaka kutokana na jitihada zinazofanywa na Serikali ikiwemo kusainiwa kwa mikataba mbalimbali ya ushirikiano, kuboreshwa kwa mazingira ya uwekezaji na biashara hapa nchini na ufunguzi wa Balozi. Alieleza kuwa, kutokana na jitihada hizo Kampuni nyingi za Uturuki zimeonesha nia na shauku ya kuwekeza na kufanya biashara hapa nchini.

“Takwimu zinaonesha kwamba kutoka mwaka 1990 hadi mwezi Septemba mwaka 2018 jumla ya Kampuni 48 za Uturuki zimewekeza Tanzania. Uwekezaji huo unathamani ya Dola za Kimarekani milioni 324.46 na umezalisha ajira 3,455 kwa Watanzania katika maeneo mbalimbali” alisema Dkt. Ndumbaro.

Akizungumzia biashara kati ya Tanzania na Uturuki, Mhe. Dkt. Ndumbaro alieleza kuwa imeimarika kwa kiasi kikubwa katika miaka ya hivi karibuni ikilinganishwa na miaka kadhaa iliyopita.

Mhe. Dkt. Ndumbaro alieleza kuwa awali Tanzania ilikuwa ikiingiza zaidi bidhaa kutoka Uturuki kama zana za kilimo, bidhaa za ujenzi, nguo na bidhaa mbalimbali za plastiki. Hata hivyo, mwaka 2017 kumekuwa na mabadiliko makubwa kwa Tanzania kuuza zaidi bidhaa zake Uturuki kama pamba, mbegu za mafuta, korosho na tumbaku kuliko Uturuki ilivyouza bidhaa zake Tanzania.

“Kwa mfano wakati bidhaa zilizouzwa Tanzania kutoka Uturuki zikiwa na thamani ya shilingi bilioni 6.091 tu, Tanzania iliuza bidhaa Uturuki zenye thamani ya Shilingi bilioni 154.749. Mabadiliko haya chanya yamechochewa na sababu mbalimbali ikiwemo juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi wa Tanzania nchini Uturuki na Sekta Binafsi ya Tanzania kuchangamkia fursa mbalimbali za masoko zinazojitokeza Uturuki” aliongeza Dkt. Ndumbaro.

Mhe. Naibu Waziri alisema kuwa ujumbe wa Makampuni hayo makubwa kutoka Uturuki ni fursa muhimu kwa Tanzania hususan kwenye mikoa ambayo yameonesha nia ya kuwekeza. Aliongeza kuwa uwekezaji utakaofanywa na Makampuni hayo utatoa fursa kubwa kwa Watanzania ambapo inakadiriwa takribani ajira 1,400 zitatolewa na Makampuni hayo.

Kabla ya kuelekea Dodoma na Simiyu kwa ajili ya kuendelea na ziara, wawekezaji hao, watafanya mkutano na wadau muhimu wa masuala ya uwekezaji  jijini Dar es Salaam ambao  ni; Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Chama cha Wafanyabiashara, wenye Viwanda na Wakulima (TCCIA), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mamlaka ya Ukanda Maalum wa Uwekezaji Tanzania (EPZA), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Mkutano kati ya Dkt. Ndumbaro na Waandishi wa Habari ulihudhuriwa pia na Balozi wa Uturuki hapa nchini, Mhe. Ali Davutoglu ambaye nae alisisitiza nchi yake kuendelea kushirikiana na Tanzania katika masuala mbalimbali ikiwemo uwekezaji, utalii na biashara ili kuzililetea maendeleo nchi hizi mbili.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
Dar es Salaam.
18 Novemba 2018


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.