Monday, October 19, 2015

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI





Taarifa zaidi kuhusu Mahujaji kutoka Tanzania waliofariki na kujeruhiwa huko Saudi Arabia

Mahujaji wengine watatu kutoka Tanzania ambao walikuwa hawaonekani tokea ajali ya kukanyagana kwa mahujaji ilipotokea Makkah nchini Saudi Arabia tarehe 24 Septemba 2015 wametambuliwa kuwa, ni miongoni mwa mahujaji waliofariki  dunia. Kutambuliwa kwa mahujaji hao kunafanya idadi ya mahujaji wa Tanzania waliopoteza maisha katika ajali hiyo kufikia ishirini na tano (25). Majina kamili ya mahujaji hao ni Bi. Faiza Ahmed Omar na Bi. Rehema Ausi Rubaga kutoka kikundi cha Khidmati Islamiya pamoja na Bw. Masoud Juma Khamis kutoka Kikundi cha Ahlu Dawaa.

Hadi sasa mahujaji kumi na tano (15) kutoka Tanzania bado hawajulikani walipo na jitihada za kuwatafuta bado zinaendelea. Aidha, miili ya mahujaji kumi na tisa (19) kutoka Tanzania tayari imeshazikwa nchini Saudi Arabia.
 
Serikali ya Saudi Arabia inaendelea kutoa taarifa zaidi za kuwatambua mahujaji waliofariki dunia au kujeruhiwa katika ajali hiyo na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa itaendelea kutoa taarifa kwa umma kuhusu wahanga wa ajali hiyo kadri itakapokuwa inazipokea.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa,
Dar es Salaam
19 Oktoba, 2015

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.