Tuesday, September 27, 2022

SERIKALI, SEKTA BINAFSI WAKUBALIANA KUBORESHA MIFUMO KUWAFIKIA DIASPORA

Mkurugenzi anayeshughulikia masuala ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi James Bwana ameeleza kuwa Serikali imejidhatiti kufanya maboresho ya mifumo ya Tehama katika sekta za umma na sekta binafsi ili kuhakikisha fursa mbalimbali zinazopatikana nchini zinawafikia diaspora kwa wakati.

Hayo yameelezwa katika siku ya pili ya mkutano wa wadau wa sekta za umma na binafsi uliojadili masuala mbalimbali kuhusu ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo ya Taifa uliomalizika leo tarehe 27 Desemba 2022 Jijini Dodoma.

Wadau wa mkutano huu wamepata fursa ya kushirikishana na kupeana uzoefu juu ya huduma mbalimbali wanazozitoa kwa diaspora, kutoa maoni ya namna bora ya kuboresha huduma na umuhimu wa taasisi kushirikiana ili kurahisisha utoaji wa huduma” alisema Balozi James

Miongoni mwa maeneo yaliyopendekezwa na wadau kwa ajili ya maboresho ni pamoja na: kuongeza kazi ya ukamilishwaji wa mapendekezo ya kupatikana kwa hadhi maalum kwa Diaspora, Uandaaji na ukamilishaji wa Sera na sheria ya Diaspora ya Tanzania, taasisi za fedha kuwa na huduma rafiki na zenye riba nafuu kwa Diaspora na ukamilishaji wa mfumo wa kidigitali wa kuhifadhi taarifa muhimu za watanzania wanaoishi na kufanya kazi nje ya nchi, ujulikanao kama “Diaspora Digital Hub”. Mfumo huu utawezesha kuwatambua Diaspora na mahitaji yao pamoja na kuongeza ubunifu katika utoaji huduma.

Maeneo mengine ni uharakishwaji wa mchakato wa kuwapatia Diaspora vitambulisho vya Taifa, kuwepo kwa siku maalum ya Diaspora ili kuwajengea uzalendo, Balozi za Tanzania nje ya nchi kusimamia kwa karibu changamoto mbalimbali za Diaspora, wadau kuwekeza zaidi katika kupata uzoefu kutoka mataifa mengine yaliyofanikiwa katika masula ya Diaspora, maboresho katika taratibu na sheria za ununuzi na umiliki wa ardhi na majengo, kuanzishwa kwa madawati maalum yanayohudumia Diaspora katika sekta za Umma na Binafsi hususan huduma za kidigitali.

Akifunga mkutano huo Naibu Mkurugenzi Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Diaspora, Ofisi ya Rais – Ikulu Zanzibar, Bi. Maryam Ramadhan Hamoud amewahakikishia wadau kuwa Serikali ya mapinduzi Zanzibar itaendelea kutoa ushirikiano na uzoefu wake katika hatua mbalimbali za uandaji wa sera na sheria ya Diaspora kwa upande wa Tanzania bara kwa kuwa tayari Tanzania-Zanzibar ilishakamilisha taratibu hizo.

Mkurugenzi wa masuala ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi James Bwana akiongea na wadau kwenye mkutano wa kujadili masuala ya ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliomalizika tarehe 27 Septemba 2022 jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa masuala ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi James Bwana akifurahia jambo wakati wa mkutano wa kujadili masuala ya ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliokuwa ukiendelea jijini Dodoma.
Mkurugenzi wa masuala ya Diaspora katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi James Bwana akifuatilia jambo wakati wa mkutano wa kujadili masuala ya ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliokuwa ukiendelea jijini Dodoma.

Afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Semeni Nandonde akichangia jambo kwenye mkutano uliokuwa ukijadili masuala ya ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliokuwa ukiendelea jijini Dodoma.
Mwakilishi kutoka Benki ya CRDB Bw. Joseph Haule akichangia mada kwenye mkutano wa kujadili masuala ya ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliokuwa ukiendelea jijini Dodoma.
Mwakilishi kutoka Exim Bank Bi. Mtenya Cheya akiwasilisha mada kwenye mkutano wa kujadili masuala yaushirikishwaji wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliokuwa ukiendelea jijini Dodoma.
Mwakilishi kutoka Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora Bi. Victoria Saria akiwasilisha mada kwenye mkutano wa kujadili masuala yaushirikishwaji wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini uliokuwa ukiendelea jijini Dodoma.
Mkutano wa kujadili masuala ya ushiriki wa Diaspora katika shughuli za maendeleo nchini ukiendelea.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.